Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba                                                                                                                            18.9.2015
---
VIONGOZI wa CCM Zanzibar wamewataka wananchi na wanaCCM kumpigia kura Dk. Ali Mohamed Shein ili aendelee kuiongoza Zanzibar katika miaka mitano ijayo kutokana na uwezo wake wa kuongoza na kutowapa kura viongozi wa upinzani kwani hawana sifa za kuongoza na Sera zao ni za ubabaishaji.

Maneno hayo waliyaeleza kwa nyakati tofauti katika mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM uliofanyika Chokocho, Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba uliohudhuriwa na maelfu ya wanaCCM na wananchi ambapo mgeni rasmi alikuwa mgombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohamed Shein.

Viongozi hao wa CCM walipata fursa ya kusalimiana na wananchi pamoja na WanaCCM waliohudhuria katika mkutano huo na kuwapongeza wananchi hao wa Pemba kwa kuonesha azma ya kuendelea kuiunga mkono CCM.

Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mhe. Pandu Ameir Kificho alitoa shukurani kwa uongozi bora wa Dk. Shein ambao umewafanya wanaCCM, wakerekwetwa na viongozi wa chama hicho wapenda amani kumshauri wakati wa ziara zake Unguja na Pemba na kumtaka achukue fomu ya kugombania tena nafasi ya Urais.

Alisema kuwa hatua hiyo imekuja kutokana na maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa yaliyoletwa na CCM katika uongozi wa Dk. Shein, na kueleza kuwa Dk. Shein hakutoa fedha ili achaguliwe katika kuwania nafasi hiyo kama wanavyofanya wagombea kutoka vyama vyengine lakini wao ndio waliomchangia fedha ili akachukue fomu ya kugombania nafasi hiyo.

Spika Kificho alisema kuwa hivi sasa kilichobaki ni kumpa zawadi Dk. Shein ambayo ni kumpa kura zote za ndio na kusema kuwa ili Dk. Shein afanye kazi vizuri pia, ni lazima wawapigie kura mgombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Magufuli na Mgombea Mwenza wake Mama Samia Suluhu Hassan, Wabunge,Wawakilishi na Madiwani wa CCM.

Nae Omar Yussuf Mzee, ambaye ni Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, alisema kuwa Ikulu haijaribiwi na kuwataka wananchi na wanaCCM wasimjaribu mtu ambaye hana sifa za kwenda Ikulu na kuwaeleza kuwa kuna kila sababu za kumchagua Dk. Shein.

Alisema kuwa Dk. Shein ni mwadilifu, muaminifu, si mbaguzi, anasimamia maendeleo Unguja na Pemba na kusisitiza kuwa jengo la uwanja wa ndenge atalifungua yeye sambamba na kuizindua  meli mpya ambayo inatarajiwa kuwasili mapema mwezi ujao.

Omar Yussuf alisisitiza kuwa sababu nyegine ya kumrejesha tena Dk. Shein madarakani ni kuwepo kwa amani na utulivu ambayo yeye ameweza ,kuisimamia vizuri na kueleza kuwa kazi iliyopo ni kumpigia kura Dk. Shein pamoja na  viongozi wote wa CCM.

"Walinikimbia siku niliyosoma Bajeti ya Serikali ambayo ni bajeti yetu sote na inayotusaidia katika mambo yetu mbali mbali ya maendeleo...msiwachague hawafai",alisema Omar Yussuf.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai, alitoa pongezi kwa wanaCCM wa Pemba kwa kuendelea kukiunga mkono Chama Cha Mapinduzi na kutoa pongezi kwa niaba ya wanaCCM kwa uwamuzi wake wa kuwaeleza wananchi kuwa mwaka wa kwanza atakapochaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar ataongeza mshahara hatua ambayo inatokana na Dk. Shein kuwajali na kuwapenda wananchi wake.

Pongezi kwa uwamuzi wake na kuwapenda watu kwa kumuagiza Waziri wa Fedha kuhakikisha kuwa meli mpya inanunuliwa na tayari hatua hiyo imechukuliwa na hivi karibuni meli hiyo itafika na itawasaidia wananchi wote wa Zanzibar katika sekta ya usafiri na usafirishaji.

Nae, Bi Zainab Omar Mohammed ambaye ni Waziri wa Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana , Wanawake na Watoto nae alieleza kuwa hana wasi wasi wowote kwani tayari Dk. Shein ameshashinda uchaguzi wa mwaka huu na kusisitiza kuwa siku ya kupiga kura  wawapigie kura viongozi wote wa CCM bila ya woga na wasi wasi wowote.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohammed Aboud alisema kuwa CCM haitoondoka madarakani kutokana na mazuri iliyoyafanya na kuwataka wanaCCM na wananchi kuendelea kuiunga mkono huku akieleza kuwa chama cha CUF tayari kimejipanga kuiba kura za Pemba kama ilivyo kawaida yao.

Aidha, alisema kuwa chama hicho cha CUF kina mpango wa kuwanunua mawakala na Maafisa wa Uchaguzi, na kutoa onyo kwa yeyote atakae nunuliwa na akanunulika hatua zinazofaa zitachukuliwa dhidi yake.

Alisema kuwa njama za chama hicho zinajulikana na kueleza kuwa maendeleo ya kweli ya Zanzibar yanaletwa na yataendelea kuletwa na CCM huku akishangazwa na Makamo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif kwa kutowasaidia ndugu zake wa Pemba hata kuwachimbia kisima.

Waziri Aboud alisema kuwa Dk. Shein ndio atakae ibadilisha Zanzibar, kwani nia yake ni kuimarisha uchumi kwa kasi kubwa zaidi ili kuondokana na umasikini na kuongeza ajira na kuwaeleza kuwa tayari Kisiwa Panza na Makoongwe umeme umeshafika ambazo hizo zote ni ahadi na juhudi za Dk. Shein.

Alieleza kuwa CCM haina wasi wasi kwani wanaenda kushindana na Ukawa sio vyama vya siasa, huku akisisitiza kuwa CCM ina Ilani yake inayoinadi na kuwataka kuwaacha wapinzani waendelee kupiga porojo na wao waendelee kutangaza Sera madhubuti za CCM pamoja na Ilani yake

Mapema Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mberwa Hamad Mberwa, akiwakaribisha viongozi na WanaCCM pamoja na wananchi katika Mkoa huo na wamelaani tabia za wapinzani za kuchana mabango na picha za wagombea wao zikiwemo picha za viongozi wanaogombania.

Alisema kuwa tayari kuna choyo zilizokuwepo kwa wanachama wa chama cha CUF hali ambayo inawapelekea kuanza kuzichana picha za wagombea wa CCM jambo ambalo linatokana na choyo hicho kwa kuona kuwa picha hizo ni nzuri, zinavutia wakiwemo wagombea wa chama hicho wakifananishwa na wengine.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.