Habari za Punde

Balozi wa PSPF mwanamitindo wa kimataifa Flaviana Matata akabidhi mabegi na madaftari kwa shule za msingi Dodoma na Singida




Balozi wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF, Flaviana Matata, akikabidhi begi kwa mwanafunzi wa Shule ya Msingi, Nyerere iliyoko Manispaa ya Singida, Oktoba 7, 2015. PSPF kupitia Sera yake ya kusaidia jamii imetoa msaada wa mabegi na madaftari kwa shule hiyo na ile ya Chididimo iliyoko nje kidogo ya Manispaa ya Dodoma


NA K-VIS MEDIA, DODOMA NA SINGIDA
BALOZI wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF, Flaviana Matata, ametoa wito kwa wanafunzi wa shule za msingi Chididimo iliyoko Manispaa ya mji wa Dodoma na ile ya Nyerere iliyoko mkoani Singida kuwahimiza wazazi wao kujiunga na Mfuko huo.
Balozi huyo ambaye pia ni Mwanamitindo wa Kimataifa anayefanyia kazi zake nchini Marekani, ameyasema hayo kwa nyakati tofauti, wakati akikabidhi vifaa vya shule kwa wanafunzi hao Oktoba 7, 2015.
“Mimi kama Balozi wa PSPF, ninatoa wito kwa wanafunzi mliopo hapa, kufikisha ujumbe huu kwa wazazi wenu, kwani kujiunga na PSPF kuna faida nyingi katika maisha ya sasa na ya baadae.” Alisema
Alisema, PSPF inatoa mikopo mbalimbali kwa wanachama wake kama vile ya viwanja, mkopo wa elimu, na mkopo wa kuanzisha maisha.
Lakini pia PSPF inatoa mafao mbalimbali kwa wanachama wa Mpango wa Uchangiaji wa Hiari, yaani (PSS), ikiwemo, Fao la Uzazi, Fao la Uzeeni, Fao la Elimu, Fao la Ulemavu na Fao la Ujasiriamali.
“Wazazi wenu wawe wakulima, wafanyakazi walioajiriwa au kujiajiri wanaweza kujiunga na PSPF kupitia mpango wa Uchangiaji wa Hiari.” Alifafanua Balozi huyo.
Naye Afisa Masoko Mwandamizi wa PSPF, Rahma Jemina Ngassa, alisema moja ya Sera za Mfuko huo ni kuchangia sekta ya Elimu na msaada huo ni utekelezaji wa Sera wa kusaidia jamii.


“PSPF inaamini vifaa hivyo vitapunguza kwa kiasi Fulani changamoto zilizokuwa zinawakabili wanafunzi hao na hivyo watakuwa kwenye nafasi nzuri ya ushiriki wa masomo kikamilifu.” Alisema.
Kwa upande wake, Kaimu Afisa Elimu Manispaa ya Dodoma, Christopher Ligonda, ameupongeza Mfuko huo kwa kuwajali wanafunzi ambao wazazi wao kwa namna moja au nyingine ni wanachama au wanachama watarajiwa na hata wanafunzi wenyewe.
Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Nyerere iliyoko mkoani Singida, Yesaya Ramadhani, ameushukuru uongozi wa PSPF kwa kuwafikiria wanafunzi wa shule hiyo katika kuwasaidia vifaa hivyo ambavyo ni mabegi na madaftari kuwa ni kitendo cha kweli katika kusaidia jamii ambayo inakabiliwa na changamoto mbalimbali.




No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.