Habari za Punde

CCM ndiyo pekee inayoweza kusimamia amani na utulivu

WANANCHI na WanaCCM wa Zanzibar wametakiwa kukichagua Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwani ndio chama pekee kinachoweza kusimamia amani na utulivu nchini sambamba na kuimarisha maendeleo kwa wananchi wote bila ya ubaguzi.

Viongozi wa CCM Zanzibar waliyasema hayo leo huko katika mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM uliofanyika uwanja wa Urafiki, Jimbo la Shaurimoyo, Mkoa wa Mjini Magharibi uliohudhuriwa na maelfu ya wanaCCM na wananchi ambapo mgeni rasmi alikuwa mgombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohamed Shein.

Viongozi hao wa CCM walipata fursa ya kusalimiana na wananchi pamoja na WanaCCM waliohudhuria katika mkutano huo na kuwaeleza haja ya  kuwachagua viongozi wa CCM ili waendelee kuwaletea maendeleo sambamba na kusimamia amani na utulivu iliyopo.

Dk. Hussen Mwinyi ambaye ni Waziri wa Ulinzi na (JKT) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alipata fursa ya kuwasalimia wananchi na wanaCCM na kupata fursa ya kumpongeza na kumshukuru Dk. Shein kwa kuendeleza amani na utulivu nchini na kusema kuwa Wizara ya ulinzi imerizika na hatua hiyo kwa Zanzibar.

Alisema kuwa ana matumaini makubwa hatua hiyo itaendelezwa hiyo ni kutokana na kuwa CCM itaendelea kuongoza na kuwataka wananchi na WanaCCM kuwachagua viongozi wa CCM ili amani na utulivu izidi kudumu.

Akieleza juu ya ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama, Dk. Mwinyi alisema kuwa kuna idadi maalum kwa kila mwaka iliyotengwa kwa ajili ya vijana wa Zanzibar na kuwataka wananchi kutopotoshwa na hilo.

Idadi hiyo inaletwa na kugaiwa kwa kupitia Wilaya zote za Zanzibar na kuahidi kuwa hatua hiyo itaendelezwa ili vijana wengi wazidi kupata ajira katika vyombo hivyo vya ulinzi.


Aliwataka wanaCCM kutobweteka na kuwataka wasikae majumbani siku ya kupiga kura na badala yake waende kupiga kura na kuwachagua viongozi wote wa CCM ili kuendeleza amani na utulivu iliyopo na kuimarisha maendeleo.

Maendeleo yote yaliopo nchini yameletwa na CCM hivyo kuna kila sababu ya kuwachagua viongozi wa CCM ili kuendeleza maendeleo hayo yaliofikiwa.

Nae Balozi Amina Salum Ali, alieleza kuwa alisema kuwa CCM haikotayari kutoa uongozi kwa chama chengine chochote kwani chama hicho ndicho pekee kinacholeta maendeleo na kuwajali wananchi wa rika zote, hali zote na jinsia zote.

Alieleza kuchukizwa na maneno ya viongozi wa upinzani kuwa hakuna maendeleo nchini na kusema kutokana na maendeleo makubwa yaliofikiwa katika nchi za Afrika hatua hiyo ilimfanya Rais wa Benki ya Dunia kusema kuwa maendeleo yanayopatikana hivi sasa yatapelekea mnamo mwaka 2020 umasikini kupungua kwa kiasi kikuhwa katika nchi za bara la Afrika.

Balozi Amina alisema kuwa maendeleo ya kiuchumi ndio yanayoimarisha uchumi na hatua hiyo ndio iliyofikiwa na Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein ambapo uchumi umekuwa kwa asilimia 7.

Alisema kuwa katika uongozi wa Dk. Shein mafanikio makubwa yamepatikana na kuwataka wananchi na wanaCCM kumpa kura Dk. Shein kwani amefanya mambo mengi na kueleza kuwa endapo watamchagua ataendeza palipofikia.

Nae Balozi Seif Idd aliwaambia wanaCCM wa Unguja na Pemba waanze kupamba kwani sababu za kushinda zipo kwani CCM imeamua na kusisitiza matawi yote yaanze kupambwa kwa ajili ya kusherrehekea ushindi wa CCM

Alisema kuwa cha cha CCM kitazidi kuimaimarika na kukua kwani ndicho kitakachokuwa kikiongoza Serikali baada ya kupata ushindi mkubwa katika uhaguzi wa mwaka huu.

Alisema kuwa wafusia wa chama cha CUF ni wabaguzi kwani hivi karibuni walifukia kaburi na kukataa kuzikwa maiti mwenye asili ya kimasai huko Kiwengwa kwa vile anatoka bara na kupelekea maiti ya marehemu huyo ikawie kuzikwa huku akisema kitendo hicho cha kumbagua maiti si cha kiungwana.

Alisema kuwa iwapo wakipewa nchi wanaweza kuwabagua Wazanzibari wote kwani tayari wameshaanza ubaguzi.

Haroun Ali Suleiman ambaye ni Waziri wa Nchi Afisi ya Rais Kazi na Utumishi wa Umma akizungumzia suala la ajira alisema kuwa tayari Sera ya Ajira imeshapitishwa na hivi sasa mipango imeshakamilika kwa kuandaa ajira mbali mbali, na kueleza kuwa Dk. Shein ameanzisha Mfuko Maalum wa Uwezeshaji kwa ajili ya kuwasaidia vijana waliokosa ajira Serikalini.

Waziri Haroun alisema kuwa Serikali imeanzisha kituo maalum katika Wizara ya Kazi, Uwezeshaji na Ajira kwa lengo la kupanua sekta ya ajira.

Alisema kuwa katika kipindi cha miaka minne Dk. Shein ameweza kufanya mabadiliko ya mishahara mara tatu.

Akieleza mafanikio katika sekta ya elimu, Haroun alisema kuwa wanafunzi wa darasa la sita hivi sasa wataingia kidato cha nne moja kwa moja na kueleza mipango ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuangalia maslahi ya waalimu.


Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai, alirudia kauli ya Dk. Shein ya kuongeza mshahara wa kima cha chini kufikia Shilingi laki tatu katika mwaka wake wa kwanza atakapoingia madarakani na kusisitiza kuwa hizo ndio ahadi za Dk. Shein zinazotekelezeka.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.