Habari za Punde

Mgombea udiwani atelekezwa na Viongozi wa juu chama cha NCCR Pemba

Masanja Mabula –Pemba
 MGOMBEA  wa nafasi ya  Udiwani Wadi ya Mchangamdogo Jimbo la Kojani Kisiwani Pemba  kwa tiketi ya NCCR Mageuzi Hassan Kombo Hasan hadi sasa ameshindwa kuanza kampeni kutokana na kutelekezwa na viongozi wa juu wa chama hicho .
Amesema kuwa tangu alipotakiwa kujaza fomu na uongozi wa Juu wa chama hicho  wakiwemo wa Jimbo , Wilaya na Mkoa  wameshindwa kumpa ushirikiano jambo linalo mfanya abakie njia panda kuhusiana na mustakabali wa kampeni kuelekea uchaguzi Mkuu .
Akizungumza na mwandishi wa habari huko Mchangamdogo , ametupa lawama kwa  viongozi wa Juu wa chama hicho ambao amedai kwamba wameacha kushughulikia masuala la chama chao na badala yake kushughulia masuala ya UKAWA.
Amesema kuwa kitendo cha viongozi wa juu wa chama hicho kukipa kisogo  , kwa sasa kinaendelea kupoteza hadhi yake siku hadi siku na kuongeza kwamba kuna uwezekano mkubwa wa chama hicho kutoweka .
“Licha ya kwamba uchaguzi umekaribia , mimi kama mgombea nimeshindwa kuanza kampeni kwani nimekosa ushirikiano kutoka kwa viongozi wangu  na hii ni kama nimetengwa vile ”alisema kwa masikitiko  .
Akizungumzia muungano wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA)  amesema kwamba umoja huo unaonekana kama sumu kwa vyama vya NCCR Mageuzi  na NLD kwani inaonyesha kuwa baada ya uchaguzi Mkuu vyama hivi vitamezwa na CHADEMA na CUF .
Amefahamisha kwamba hata uteuzi wa wagombea wa nafasi za uongozi  kuanzia Udiwani , Uwakilishi  na Ubunge  umekwenda kinyume na makubaliano yaliyomo kwenye waraka wa ushirikiano uliotiwa sahihi na viongozi wa vyama hivyo .
“ Kwa mujibu wa waraka huu Ibara ya 3.0, kifungu cha 3.3 imeeleza kwamba  majadiliano ya maridhiano yafanyike katika ngazi ya jimbo /Wilaya kwa viongozi wa vyama washirika kupeleka wajumbe watatu watakaojadili ili kufikia mufaka , lakini hili halikufanyika ”alieleza .
Amefahamisha kwamba Muungano huo wa  vyama vinne haauko wazi kwani unavinufaisha vyama viwili ndani ya Umoja huo na ambavyo vimepewa nafasi nyingi za wagombea CUF kwa upande wa Zanzibar na CHADEMA kwa upande wa Bara .
Akizungumzia uwamuzi wake wa kugombea nafasi hiyo  Hassan amesema kuwa alitakiwa achukue fomu na Uongozi wa Chama hicho , na baada ya kuhoji kuhusiana na uwepo na mgombea mwengine wa CUF aliambiwa kwamba suala la uteuzi sio kazi yake .
“Mimi nilipotakiwa njaze fomu nilihoji uwepo na mgombea mwengine wa CUF, niliambia kwamba uteuzi sio kazi yangu , lakini baada ya kuipeleka fomu yangu Jimboni CUF waliikataa sikujua ni kwa nini ”alifahamisha .

Tofauti ni chaguzi zilizopita NCCR Mageuzi hakina wagombea wa Ubunge na Uwakilishi Kisiwani Pemba lakini  kimewasimamia wagombea wawili tu wa Udiwani katika Wadi wa Msuka na Mchangamdogo .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.