Habari za Punde

Mgombea Urais wa Zanzibar Dk Shein,Akiwahutubia Wananchi wa Nungwi Zanzibar.

Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia mkutano mkubwa wa aina yake wa kampeni katika mji mdogo wa Nungwi katika mkoa wa Kaskazini Unguja na kuwataka wananchi kukichagua chama hicho kwa kuwa ndicho kinachothamini na kinachotekeleza malengo ya Mapinduzi ya mwaka 1964.

Aliwaambia maelfu ya wananchi waliohudhuria mkutano huo kuwa wanapaswa kuichagua CCM kwani ndicho chama chenye uwezo na kimeonesha mfano wa utekelezaji wa malengo ya Mapinduzi na ahadi za Rais wa kwanza wa Zanzibar hayati Mzee Abeid Amani Karume.

“Mapinduzi ndiyo yaliyoweka msingi wa usawa na kuondosha ubaguzi ambao uliwanyima haki na kuwakandamiza wananchi walio wengi wa Zanzibar” Dk. Shein alieleza.

Katika mnasaba huo alisema kuwa Mapinduzi yalileta usawa na kujenga mazingira ya kuijenga nchi yetu kwa ushirikiano na kwa umoja wetu na kwa maslahi yetu wote.

Mgombea huyo wa CCM alisema Zanzibar ni maarufu ulimwenguni kote tokea karme nyingi zilizopita lakini umaarufu huo hautakuwa na manufaa kwetu endapo hatutaweza kulinda na kuienzi amani na utulivu uliopo.

Katika kipindi kijacho aliahidi kuimarisha huduma za jamii ikiwemo elimu, afya, umeme na maji pamoja na miundombinu ya barabara ili kukidhi mahitaji makubwa ya huduma hizo kutokana na mji huo kupanuka sana kutokana na shughuli za biashara ya utalii.

“Tutaimarisha huduma za umeme kwa kuweka transfoma kubwa yenye KVA 200 katika mji mpya ulioko Ras Nungwi itakayoweza kuhudumia wateja wengi na kwa uhakika zaidi” Dk. Shein alisema na kuongeza kuwa mji huo mdogo utawekewa taa za barabarani hadi Kivunge.

Dk.Shein aliwaeleza wananchi hao kuwa biashara ya utalii ndio inayoipatia Zanzibar fedha nyingi za kigeni hivyo lengo la Serikali katika miaka mitano ijayo ni kuongeza idadi ya watalii wanoitembelea Zanzibar ifikie 500,000 ifikapo 2020 kutoka 300,000 hivi sasa huku jitihada zikielekezwa katika kuimarisha uwezo wa wananchi kitaaluma wa kuweza kuhudumia sekta hiyo. 

Aliwaeleza wananchi hao kuwa kupanua haraka kwa mji Nungwi ni uthibitisho kuwa Nungwi inaendelea kusonga mbele kwa kujenga majengo mengi na hoteli nyingi za kitalii.

Dk. Shein aliahidi atakapochaguliwa tena Serikali yake itawajengea uwezo wavuvi nchini kwa kuwapatia boti zenye ukubwa wa kati na kubwa ili waweze kuvua kwa uhakika na kupata mapato makubwa zaidi.

Kwa upande wa kilimo cha mwani, dk. Shein alisema ataiamarisha masoko la mwani kwa kutafuta masoko mapya ya zao hilo ili wakulima waweze kupata bei nzuri na kufaidi jasho lao. 



  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.