Habari za Punde

Dk Shein aongoza mazishi ya muasisi wa mapinduzi, Mzee Hamid Ameir

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                    06 Machi, 2016

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Maelfu ya wananchi wakiongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyeikiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo wameshiriki mazishi ya mmoja ya waasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar Mzee Hamid Ameir.

Mzee Hamid Ameir ambaye alifariki jana katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja mjini Zanzibar ambako alilazwa kwa matibabu amezikwa kijiji kwao Donge wilaya Kasakazi ‘A’ Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Kwa mujibu wa maelezo ya serikali yaliyosomwa na 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Mohamed Aboud Mohamed kwa waombolezaji,marehemu Hamid Ameir alishiriki kikamilifu katika Mapinduzi yaliyowakomboa wananchi wa Zanzibar kutoka kwa wakoloni mwaka 1964.

Marehemu ambaye alizaliwa 01 Januari, 1928 alijiunga na Chama cha Afro Shirazi mwaka 1957 na kushiriki kuunda Umoja wa Vijana wa chama hicho (ASPYL).

Marehemu Hamid Ameir alishika nyadhifa mbalimbali katika serikali na Chama cha Afro Shirazi na baadae Chama cha Mapinduzi.
Aliwahi kuwa kamanda wa Jeshi la Ukombozi na pia kushika nafasi ya naibu Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Viongozi wengine wa kitaifa walioshiriki mazishi ya mwasisi huyo wa Mapinduzi ni pamoja na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilal pamoja na mawaziri, makatibu wakuu na viongozi wa dini.  

Kutokana na kushiriki kwake katika Mapinduzi na kwa mchango wake katika kulinda na kuendeleza Mapinduzi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alimtunuku mzee Hamid Ameir Nishani ya Kumbukumbu ya Miaka 50 ya Mapinduzi katika sherehe zilizofanyika tarehe 11 Janauri, 2014 katika Viwanja vya Ikulu, Zanzibar.

Mwaka huo huo, tarehe 25 April, 2014 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete alimtunuku mzee Hamid Ameir, Nishani ya Kumbukumbu ya Miaka 50 ya Muungano.

Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 

1 comment:

  1. muandishi mtu mkubwa kama huyu, basi hata picha? au ccm ilimtupa mana kwa jina hatumjui

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.