STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 7.4.2016
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.
Ali Mohamed Shein leo amewaongoza viongozi na wananchi mbali mbali katika kisomo
maalum cha kumuombea dua Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi marehemu Sheikh Abeid Amani Karume ikiwa pia, ni maadhimisho ya
kumbukumbu ya miaka 44 ya kifo chake.
Marehemu
Mzee Karume ambaye pia, alikuwa Kiongozi wa Chama cha Afro-Shirazi (ASP) na
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliuawa siku ya
Ijumaa tarehe 07 April, 1972 saa 12:05 jioni katika Makao Makuu ya ASP ambayo
sasa ni Ofisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) iliyopo Kisiwandui mjini Unguja.
Katika
maadhimisho hayo yaliyofanyika Ofisi Kuu ya CCM ambako ndipo alipozikwa
marehemu, Dk. Shein na viongozi mbalimbali pamoja na wananchi walishiriki
kisomo maalum cha kumuombea dua kiongozi huyo ambaye kifo chake kiliushitua
ulimwengu mzima.
Baada
ya kisomo hicho viongozi hao walizuru kaburi la marehemu wakiambatana na
viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini ambao walipewa fursa za kumuombea dua marehemu
wakiwa kaburini hapo.
Kisomo hicho
cha kumuombea dua Marehemu Mzee Karume kilihudhuriwa na viongozi mbali mbali
akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu
Hassan kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe
Magufuli, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd na Rais
mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Sita, Mhe. Amani Abeid
Karume.
Viongozi
wengine walihudhuria katika hitma hiyo ni
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mzee Ali Hassan Mwinyi, Spika
wa Baraza la Wawakilishi Mhe. Zubeir Ali Maulid, Mufti Mkuu wa Tanzania Bara
Sheikh Abubakar Zubeir, Kadhi Mkuu wa
Zanzibar Sheikh Khamis Haji, Sheikh wa Mkoa wa Dar-es- Salam Sheikh Mussa Salum.
Aidha, Mama
Mwanamwema Shein alihudhuria katika tukio hilo akiungana na akina mama wengine
akiwemo, Mama Fatma Karume na Mama Asha Balozi na viongozi wengine wanawake wa
Kitaifa pamoja na viongozi wa serikali zote mbili na wakiwemo viongozi
wastaafu, viongozi wa vyama vya siasa, Masheikh kutoka Zanzibar na Tanzania
Bara, Wabunge, Wawakilishi, Mabalozi wadogo wanaofanya kazi zao hapa Zanzibar
na wananchi kutoka sehemu mbali mbali.
Kisomo hicho
cha kumuombea dua marehemu Mzee Abeid Amani Karume pia, ni miongoni mwa
maadhimisho ya Siku ya Mashujaa, kilitanguliwa na Qur-an tukufu iliyosomwa na
Ustadh Sharif Muhidin na kuongozwa na Sheikh Jafar Abdallah kutoka Masjid Noor
Mohammad,iliopo Kwa Mchina Mwanzo.
Mara baada ya
hitma hiyo, Sheikh Hamid Masoud Jongo kutoka Tanzania Bara, alitoa mawaidha yalioendana
na maudhui ya kumbukumbu hiyo na kumuelezea marehemu mzee Abeid Amani Karume
kuwa ni kiongozi bora kutokana na kuwafaa watu waliowengi hapa nchini na
kumuombea MwenyeziMungu ampe makaazi mema Peponi.
Sheikh Jongo
alisema kuwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano zimefaidika na Muungano
huo ulioasisiwa na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume pamoja na Marehemu Julius
Kambarage Nyerere huku Sheikh Jongo akishangazwa na wale wanaoupinga Muungano
huo.
Katika
mawaidha yake hayo alisisitiza umuhimu wa kumuombea dua kiongozi huyo kutokana
na msisitizo na msimamo wa kiongozi wa Waislamu, Mtume Muhammad (S.A.W) wa kupita
makaburi kwa kila mwaka kwa ajili ya kuwaombea dua wale wote waliouhami Uislamu
na kutoa mchango wao mkubwa katika dini hiyo.
Sambamba na
hayo, Sheikh Jongo alieleza kuwa kutokana na juhudi zake Mzee Karume ndio
zilizopelekea kupatikana uhuru sambamba na kuendelea kuwepo kwa amani na
utulivu hapa nchini.
Mara baada ya
tukio hilo, tukio lililofuata lilikuwa ni kuweka mashada ya maua katika kaburi
la marehemu Mzee Karume kitendo kilichofanywa na viongozi wakuu pamoja na
muwakilishi wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Meja Jenerali Issa Nassor,
wawakilishi wa familia, muwakilishi wa wazee waasisi Mzee Suleiman Omar pamoja
na muwakilishi wa Mabalozi wadogo
wanaofanya kazi zao hapa Zanzibar.
Marehemu
Mzee Karume aliongoza harakati za kupigania uhuru wa Zanzibar hadi kuongoza
Mapinduzi yaliyoung’oa utawala wa Kisultani uliokuwa ukihamiwa na Serikali ya
Kingereza baada ya watawala hao kufanya kila njama za kuwanyima uhuru wananchi
wa Zanzibar.
Mzee
Karume anakumbukwa sana na wananchi wa Zanzibar kwa namna alivyoweza katika
kipindi kifupi cha utawala wake kuleta mageuzi makubwa katika jamii ya Wazanzibari
ambapo alisimamia haki na usawa katika umiliki wa njia za uchumi kama ardhi na
kuondoa kabisa ubaguzi katika elimu, afya, ajira na kuwapatia wananchi makazi
bora sambamba na mambo mengine muhimu ya kimaendeleo na kimaisha.
Mwenyezi
Mungu alilaze roho ya marehemu mahala pema peponi-amin
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment