Viongozi waandamizi wa Wizara ya Afya wakisikiliza kwa makini mazungumzo kati ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein na Mwakilishi wa Shirika la Afya Ulimwenguni WHO hapaTanzania Dr.Chatora Rufaro akiongoza Ujumbe wa mashirika ya Umoja wa Mataifa UN
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na Mwakilishi wa Shirika la Afya Ulimwenguni WHO hapaTanzania Dr.Chatora Rufaro akiongoza Ujumbe wa mashirika ya Umoja wa Mataifa UN walipofika Ikulu Mjini Zanzibar [Picha na Ikulu.]
STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 19.4.2016
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein
ameeleza kuwa juhudi za makusudi sambamba na mashirikiano ya pamoja zinahitajika
katika kupambana na maradhi ya kipindupindu ambayo yameonesha kushika kasi hivi
sasa hapa nchini.
Dk. Shein aliyasema hayo katika mazungumzo
kati yake na uongozi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) hapa Tanzania, ukiongozwa
na Mwakilishi wa Shirika hilo Dk. Chatora Rufaro pamoja na viongozi wengine wa
Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) wanaofanya kazi zao hapa nchini.
Katika mazungumzo hayo Dk. Shein aliyapongeza
mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) yanayofanya kazi zake hapa nchini likiwemo Shirika
la Afya Duniani (WHO), pamoja na UNICEF katika juhudi zao za kuendelea kuiunga
mkono Zanzibar hasa katika mapambano ya maradhi ya kipindupindu yalioibuka hivi
sasa.
Dk. Shein alisema kuwa ujio wa Mwakilishi
huyo wa (WHO) hapa nchini katika kipindi hichi ni muhimu sana na utasaidia kwa
kiasi kikubwa katika kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia
Wizara ya Afya katika kusaidia mapambano ya maradhi hayo.
Alisema kuwa iwapo juhudi za makusudi
zitachukuliwa na kila mmoja akafanya wajibu wake ipasavyo sambamba na kuwa na mwamko
katika kuchukua tahadhari kuhusu kujikinga na maradhi ya kipindupindu hatua
hiyo itasaidia katika kupambana na maradhi hayo ambayo hatimae yatapungua ama
kuondoka kabisa.
Dk. Shein alisema kuwa maradhi hayo yana
historia hapa Zanzibar na yaliwahi kuibuka katika miaka ya nyuma lakini baada
ya juhudi kubwa za kuyatokomeza kuchukuliwa na Serikali kwa mashirikiano na
wananchi pamoja na washirika wa maendeleo yalichukua muda kuibuka tena kutokana
na juhudi za pamoja zilizochukuliwa wakati huo.
Aidha, Dk. Shein alieleza haja ya
kudumisha usafi hasa katika maeneo yote ya visiwa vya Zanzibar yakiwemo maeneo
ya Manispaa ya mji wa Zanzibar ambayo hali ya usafi wa mji huo haiko vizuri
hali ambayo inachangia kuibuka kwa maradhi hayo.
Akieleza umuhimu wa kutumia dawa za kutia
kwenye maji yaani vidonge vya “water guard” Dk. Shein alisema kuwa mbali ya
hatua hiyo watendaji wa Wizara ya Afya nao wanajukumu kubwa katika kutekeleza
majukumu yao na kusisitiza ulazimu wa kutumia maadili yao ya kazi katika kuwasidia
wananchi.
Akigusia suala zima la elimu kwa jamii,
Dk. Shein aliitaka Wizara ya Afya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi mara kwa
mara kupitia vyombo vya habari juu ya athari, kinga na maambukizi ya maradhi
hayo.
Dk. Shein alisema kuwa mripuko wa maradhi
hayo katika kipindi hichi ni changamoto kubwa kwa Wizara ya Afya na kueleza
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na juhudi zake za kuzisaidia
sekta zote katika kupambana na maradhi hayo.
“Maradhi ya kipindupindu ni rahisi kupambana nayo iwapo
kila mmoja atatimiza wajibu wake na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya ikiwa
ni pamoja na kuacha kutumia maji yasiyo salama ambayo ni moja ya chanzo kikubwa
cha kupata maradhi haya….. kama tulivyofanikiwa kupambana na Malaria nalo hili
linawezekana”,alisema Dk. Shein.
Nae Mwakilishi wa (WHO) nchini Tanzania Dk. Rufaro Chatora alimueleza
Dk. Shein azma ya Shirika hilo katika kuisaidia Zanzibar kwenye vita ya
kupambana na maradhi hayo hapa nchini na kusisitiza umuhimu wa kuwepo
mashirikiano na uratibu wa pamoja kati ya taasisi za Serikali, taasisi za
kiraia na watu binafsi katika kutekeleza wajibu wao juu ya kukabiliana na kipindupindu.
Mwakilishi huyo alieleza kuwa tokea mwezi wa Septemba mwaka jana
yalipoibuka maradhi hayo hapa Zanzibar wamekuwa wakifanya kazi kwa pamoja na
Wizara ya Afya na kuahidi ushirikiano zaidi katika kupambana na tatizo hilo
huku akisisitiza haja kwa vyombo vya habari kusaidia juhudi hizo.
Aidha, Mwakilishi huyo wa (WHO) amesema kuwa Shirika hilo kwa
kushirikiana na mashirika mengine ya Kimataifa litaendelea kuunga mkono juhudi
za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kukabiliana na maradhi hayo ili
kuhakikisha yanamalizika.
Sambamba na hayo, kiongozi huyo alieleza kuwa chanzo kikubwa cha maradhi
hayo ni maji hivyo kuna kila sababu ya kutoa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa
kutumia maji yalio safi na salama ikiwa ni pamoja na kutumia ‘water guard’
pamoja na kuimarisha usafi katika maeneo yote.
Akizitaja tahadhari juu ya maradhi hayo, Dk. Chatora alisema ni pamoja
na kuweka mazingira safi, kufuata masharti ya afya, kuchemsha maji ya kunywa
ama kutumia maji yaliyotiwa dawa ya kuulia bektiria wanaosababisha maradhi ya
kipindupindu.
Pia, Mwakilishi huyo alieleza haja kwa wananchi
kuwapeleka mapema katika vituo vya afya watu wanaobainika na dalili za maradhi
ya kipindupindu kwa vile imeonekana wagonjwa wengi wanapopelekwa vituoni afya
zao zinakuwa mbaya na hatimae matibabu yanakuwa magumu.
Mapema aliekuwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dk.
Mohammed Saleh Jidawi alieleza mashirikiano na uhusiano mwema uliopo kati ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mashirika ya Umoja wa Mataifa likiwemo (WHO)
jinsi linavyotoa ushirikiano wake katika vita ya kupambana na maradi hayo.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment