Na Mwashungi Tahir, MAELEZO-ZANZIBAR
WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha usafi wa mazingira katika maeneo ya skuli ili kudhibiti maradhi ya mripuko ikiwemo kipindupindu.
Amesema hayo alipokuwa kwenye ziara ya kutembelea skuli mbalimbali kufuatia mripuko wa maradhi ya kipindupindu unaoendelea Zanzibar na athari ya mvua za masika zinazoendelea kunyesha.
Waziri huyo amesema iko haja kwa walimu kuchukua tahadhari zaidi ya kuhifadhi mazingira kutokana na ongezeko la kipindupindu ili kuwakinga wanafunzi na dhidi ya maradhi hayo.
Mwalimu Mkuu wa skuli ya Faraja iliyoko Kilimahewa mjini Unguja Ameir Khamis Bakari, alimueleza waziri huyo kwamba skuli yao inakabiliwa na changamoto kadhaa zinazohitaji nguvu ya serikali kuzimaliza.
Aidha alisema kero nyengine ni mtindo wa wananchi wanaoishi karibu na skuli hiyo kutupa taka katika maeneo ya skuli.
Alieleza kuwa tayari uongozi wa skuli umetoa taarifa kwa viongozi wa shehia lakini hata hivyo hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa hadi sasa.
Akizungumzia changamoto hizo, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amalio Riziki Juma Pembe, alisema vitendo hivyo haviwezi kuvumiliwa hata kidogo.
Aliahidi kuwa uongozi wa wizara utakaa pamoja na viongozi wa shehia kuyatafutia ufumbuzi matatizo hayo ili kuwanusuru wanafunzi wa skuli hiyo na maradhi, na kuwawezesha kusoma katika mazingira mazuri.
Katika mfululizo wa ziara hiyo, waziri huyo alifika katika skuli ya sekondari Vikokotoni, na kumtaka mmiliki wa duka lililopo mkabala na skuli hiyo, kurekebisha mabomba ya maji machafu yanayoingiza maji ndani ya skuli hiyo na kuwapa usumbufu wanafunzi na walimu.
Kwa upande wake, Naibu Waziri Wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mmanga Mjengo Mjawiri, amewahimiza walimu wakuu kuweka vipindi vya masomo ya mazingira ili kuwajengea wanafunzi tabia ya kudumisha usafi.
Halikadhalika, ametoa wito kwa walimu wakuu kusimamia usafi katika maeneo ya skuli zao, ili kuimarisha usalama wa wanafunzi ambao ndio viongozi wa baadae.
Skuli nyengine zilizotembelewa na viongozi wa wizara hiyo, ni Mwanakwerekwe C, Kwamtipura na Haile Sellassie.
No comments:
Post a Comment