Habari za Punde

Jamii zaaswa kubadilika kukabiliana na kipindupindu

 Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar Dkt. Moh’d Dahoma akifungua mafunzo ya siku moja kwa wandishi wa Habari kuhusu maradhi ya kipindupindu katika Ukumbi wa Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar.
Baadhi ya waandishi wa habari walioshiriki mafunzo ya siku moja juu ya maradhi ya kipindupindu wakifuatilia mafunzo hayo katika ukumbi wa Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.
Mkuu wa Kitengo cha Elimu ya Afya Zanzibar Nd. Kheri Makame Kheri akitoa ufafanuzi kuhusiana na maradhi hayo na kuwataka waandishi kujikita zaidi kuelimsha jamii.
Ofisa Afya kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Ofisi ya Dar es salaam Dkt. Neema Kileo akisisitiza jambo kwa  waandishi wa habari (hawapo pichani) waliohudhuria mafunzo ya siku moja juu ya mripuko wa maradhi hatari ya kipindupindu Zanzibar.
 Mwandishi wa habari kutoka Zenj F M Radio Mustafa akichangia mada zilizowasilishwa katika mafunzo ya siku moaja ya waandishi wa habari iliyofanyika Wizara ya Afya Zanzibar Mnazimmoja.
Mtaalamu wa mabadiliko ya tabia katika afya na mawasiliano kutoka Wizara ya Afya Salum Aboubakar akitoa tathmini ya maradhi ya kipindupindu tokea yalipoanza mwezi Septemba mwaka jana mpaka hivi sasa.

Na Ramadhani Ali/MAELEZO ZANZIBAR          

Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar Dkt. Muh’d Dahoma amesema ili ugonjwa wa Kipindupindu umalizike inategemea zaidi  maamuzi ya familia na jamii kwa jumla  kukubali kubadilika.

Amesema desturi potofu na tabia za wananchi zinachangia kwa kiasi kikubwa  kuongezeka kwa maambukizi ya kipindupindu nchini.

Akifungua mafunzo ya siku moja kwa waandishi wa habari kuhusu ugonjwa wa kipindupindu yaliyofanyika Wizara ya Afya Mnazimmoja, Dkt. Dahoma amewataka waandishi wa habari kutoa elimu zaidi kwa  jamii  ili wajue sababu zinazopelekea kuongezeka ugonjwa huo na njia za kujikinga.


Amesema bado wananchi wanakuwa wagumu  kubadili mfumo wao wa maisha  licha ya juhudi zinazochukuliwa na Jumuiya za kimataifa, taasisi za Serikali na binafsi pamoja na vyombo vya habari.

‘’Bado watu wanaishi katika mazingira machafu, wengine hawana vyoo  na wapo hawataki kuyatibu maji ya kunywa, mambo yanayochangia mambukizi ya kipindupindu,’’ alisisitiza Dkt. Dahoma.

Ameishauri jamii kuwa tayari kubadilika baada ya kupata elimu ya maradhi ya kipindupindu ili kupunguza vifo vinavyotokana na maradhi hayo.

Akitoa takwimu ya maradhi ya kipindupindu tokea yalipoanza mwezi Septemba mwaka jana, amesema  wananchi 3,700  wameugua maradhi hayo na  46 kati yao wamefariki na  Wilaya ya Magharibi  inaongoza kwa kutoa wagonjwa wengi zaidi.

Mtaalamu wa mabadiliko ya tabia katika afya na mawasiliano kutoka Wizara ya Afya Zanzibar Nd. Salum Aboubakar amewashauri wahariri wa habari kuvipa  kipaumbele vipindi na habari zinazohusu Kipindupindu katika vyombo vyao ili wananchi waweze kuzinduka.

Nae Ofisa Afya kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Ofisi ya Dar es salaam Dkt. Neema Kileo ameshauri vipindi vinavyozungumzia kipindupindu vipangwe katika muda ambao wananchi wengi wanaweza kuvisikiliza.

Washiriki wa mafunzo hayo wamekubali kutoa muda zaidi katika vyombo vyao vya habari kwa  maafisa wa Kinga na Elimu ya Afya ili kutoa elimu zaidi katika kukabiliana na maradhi hayo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.