Habari za Punde

Taarifa kwa Umma: Ufafanuzi Juu ya Uvumi Kuhusu Hali ya Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF)

Hivi karibuni kumekuwa na taarifa mbalimbali zisizo rasmi kuhusu hali na mwenendo wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF). Baadhi ya taarifa hizo zimekuwa zikieleza kwamba mali za Mfuko huo zimetumiwa vibaya na hivyo kuathiri mafao kwa wanachama. Taarifa hizi zimesababisha hofu na taharuki miongoni mwa wanachama wa NSSF na wadau wa Sekta ya Hifadhi ya jamii kwa ujumla kwa kuhofia usalama wa fedha na mafao yao. 

Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) inapenda kuwaondoa hofu wanachama wote wa Mfuko wa NSSF na Wananchi kwa ujumla na kuwahakikishi kwamba Mfuko wa NSSF upo katika hali nzuri kifedha na unaendelea kulipa mafao ya wanachama kama kawaida. Kama mnavyofahamu, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko alikwishateuliwa na anaendelea na majukumu ya kusimamia shughuli zote za Mfuko. Vilevile, taratibu za kupata Bodi mpya ya Wadhamini ya Mfuko huo zipo katika hatua za mwisho. 

Aidha, SSRA kwa kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania kwa mamlaka waliyopewa chini ya Kifungu cha 6(2) (c) cha Sheria Na.8 ya mwaka 2008 ikisomwa pamoja na kifungu cha 40 na cha 48 wanaendelea kufanya kaguzi za Mifuko yote ukiwemo Mfuko wa NSSF kwa lengo la kuhakikisha kwamba muda wote Mifuko yote inakuwa katika hali nzuri kwa maslahi ya wanachama na taifa kwa ujumla. 

Mwisho, Mamlaka inapenda kuwaondoa wasiwasi wanachama walioathirika na taarifa hizi pamoja na wanachama wote wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na kuwahakikishia kwamba fedha na mafao yao yapo salama na Mamlaka inazifanyia kazi kero zao kwa bidii kubwa. Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii S.L.P 31846 Tovuti: www.ssra.go.tz Dar es Salaam.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii S.L.P 31846 Tovuti: www.ssra.go.tz Dar es Salaam

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.