Habari za Punde

UN Yawapiga Msasa Wanafunzi wa UDOM Kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs)

Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akiendesha semina fupi kuhusu Malengo 17 mapya ya Maendeleo Endelevu (SDGs) kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) (hawapo pichani) inayoendelea mjini Dodoma chuoni hapa.

Katika kuhakikisha kila Mtanzania anapata elimu kuhusu Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu (SDGs) ambayo yanatakiwa kumfikia mtu mmoja mmoja, ofisi ya Umoja wa Mataifa nchini (UN) imetoa mafunzo kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), mafunzo ambayo yataweza kuwajengea uwezo kuhusu mpango huo na jinsi unavyoweza kubadili maisha yao.

Akizungumza na MO blog kuhusu mafunzo hayo, Mtaalamu wa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini, Bi. Hoyce Temu alisema kuwa mafunzo hayo kwa wanafunzi wa UDOM ni sehemu wa mafunzo ambayo yanatolewa na ofisi ya UN nchini ili kuwawezesha Watanzania kuufahamu mpango huo ambao una malengo ya kubadili maisha ya kila mwananchi, mpango ambao utamalizika mwaka 2030.

Alisema katika mafunzo hayo wametoa elimu kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) kwa wanafunzi zaidi ya 200 na hayo siyo mafunzo ya kwanza kwani wameshatoa mafunzo kama hayo kwa wabunge wa Tanzania lakini pia wameshafanya mafunzo kama hayo jijini Arusha ambapo yalihudhuriwa na vijana zaidi ya 200.

“Tunataka kila Mtanzania ajue kuhusu Malengo ya Maendeleo Eendelevu (SDGs) tumeshatoa elimu sehemu nyingine hii siyo ya kwanza na tutaendelea kwenda maeneo mengine kutoa elimu zaidi na katika hilo ofisi ya Umoja wa Mataifa nchini ipo imejipanga kufanya hivyo,” alisema Bi. Temu.
Nae Mkuu wa Kitovu cha Mitaala katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Prof. Willy Komba alisema mafunzo hayo yamewajenga na kupata elimu ambayo walikuwa hawajaipata awali inayohusu Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) na pia kueleza kutokana na umuhimu wake watakaa kuangalia ni jinsi gani wataweka katika mtaala wa masomo ili wanafunzi wajifunze kuhusu SDGs.

“Sababu na mimi ndiyo Mkuu wa kitengo cha mitaala nitakaa na wenzangu tuone jinsi gani tunaweza kuweka katika mitaala yetu ili hata wanafunzi wajifunze kama masomo, tunawashukuru kwa mafunzo yenu mmetupa changamoto mpya ambayo hatukuwa nayo,” alisema Komba.

Sehemu ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wakisiliza kwa makini wakati semina fupi kuhusu Malengo 17 mapya ya Maendeleo Endelevu (SDGs) iliyoendeshwa na Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (hayupo pichani).

Mtaalamu wa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini, ambaye pia ni mmoja wa wakufunzi wa masuala ya SDGs, Hoyce Temu akifafanua jambo wakati wa semina fupi ilihusisha wanafunzi wa UDOM inayoendelea mjini Dodoma.
Mwanafunzi wa mwaka wa tatu UDOM wa Didgrii ya kwanza ya Mifumo ya habari na Mawasiliano, Lobezi Kulilo akihoji kuhusiana elimu ya SDGs kuwafikia watu walio vijijini.
Mwanafunzi wa Digrii ya kwanza ya Sayansi ya Kompyuta UDOM, Traygod Lyimo akiuliza swali kwa wakufunzi kuhusiana na SDGs.
Pichani juu na chini ni Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wakipitia vipeperushi mbalimbali vyenye taarifa za kina kuhusu Malengo 17 mapya ya Maendeleo Endelevu (SDGs) wakati wa semina fupi iliyoandaliwa na Ofisi ya Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini.

Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez, akijibu baadhi ya maswali yaliyoulizwa na wanafunzi wa UDOM wakati wa semina fupi kuhusu Malengo ya dunia iliyoandaliwa na Umoja huo mjini Dodoma jana.
Mkuu wa Kitovu cha Mitaala katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Prof. Willy Komba akitoa neno la shukrani kwa Umoja wa Mataifa kwa kuwapatia mafunzo ya SDGs mara baada ya kumalizika semina fupi kwa wanafunzi wa UDOM.
Kutoka kushoto ni Waziri wa Habari wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), James Msofe, Mtaalamu wa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini, ambaye pia ni mmoja wa wakufunzi wa masuala ya SDGs, Hoyce Temu na Mwanafunzi wa mwaka wa tatu UDOM wa Didgrii ya kwanza ya Mifumo ya Upashanaji Habari, Lobezi Kulilo katika picha kumbukumbu wakilishilia mabango ya SDGs.
Baadhi ya wanafunzi wa UDOM walioshiriki semina fupi kuhusu SDGs iliyoandaliwa na ofisi ya Umoja wa Mataifa chuoni hapo katika picha ya pamoja na vibao vyenye Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanafunzi wa UDOM mara baada ya kumalizika kwa semina kuhusu Malengo ya Dunia iliyoandaliwa na Ofisi ya Umoja Mataifa mjini Dodoma jana.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.