1.0.UTANGULIZI
MIONGOZO ya Dunia katika
kupigania haki na Ujenzi wa Demokrasia ya kweli kupitia taratibu na mifumo
mbali mbali ikiwemo ya Uchaguzi inazingatia na kuhimiza sana usawa na uwiano wa
kijinsia.
Mifumo hii inataka kuwepo nguvu
zinazolingana ama kuwiana katika vyombo vya maamuzi kati ya wanawake na wanaume
wanaomba na kupewa madaraka ya uongozi wa kiasiasa na hata katika ngazi za
uteuzi.
Lakini licha ya kuwepo mazingatio
hayo kwa mitazamo na maudhui ya kimataifa ni dhahiri kwamba bado wanawake wanakumbana
na changamoto za vipingamizi kadhaa wa kadhaa katika kufikia matarajio ya
kushika madaraka na uongozi wa kisisasa.
Hali hiyo imekuwa ikichangiwa na
sababu tofauti likiwemo mifumo
inayotokana na tamaduni kandamizi kwa baadhi ya jamii zinazowapunguzia
uwezo na kuwapa ukomo wa madaraka wanawake na hivyo kuonekana kwamba bado
wanawake hawajaweza kuwa na nguvu sawa
na wanaume katika kushika madara na dhamana za uongozi katika sura ya
kitaifa hata kimataifa.
Mawazo hayo kwa sasa yanakinzana sana na
fikrana na mawazo mbadala waliyonayo wanaharakati na taasisi na Jumuiya
tofauti Duniani zinazosimamia masuala ya usawa wa jinsia kwa kuhimiza michakato
ya kutafuta na kupewa wananchi dhamana na madaraka ya kisasa kwamba ni lazima
izingatie tangu hatua ya kisera, kitaratibu na kisheria kuwepo uwiano katika ya
mwanamke na mwaname.
Kufanikiwa kwa Kampeni za namna
hii kitaifa na kimataifa kunategemea sana upeo wa uelewa na fikra za
kimabadiliko kwa wanajamii, lakini
inabidi tuelewe kwamba kwa kiasi
kikubwa mchango wa vyombo vya habari makini unahitajika kufanikisha hilo.
Vyombo hivi hubeba jukumu la
ziada katika kuisaidia jamii kuchambua na kuelewa kwamba ili kuchagua kiongozi
anayefaa ni kwa kuzingatia uwezo wa kumudu
majukumu na kuchapuza kasi ya maendeleo yao na kamwe kusijali kuwa
mwanamke ama mwanamme lakini zaidi
kuzingatia uwezo, ari , kipaji , maadili na moyo wa uzalendo katika
harakati za ujenzi wa nchi.Ni kwa msingi huo, vyombo vya habari hivi sasa
vinabeba dhana pana zaidi duniani ya kuwa na , sio tu wa kuelimisha na
kuburudisha, lakini vinabeba dhamana ya kuwa muhimili wa nne wa dola licha
kwamba mihimili mingine ya dola inauona kama sio na kulibakisha Bunge, Serikali na mahakama
kuwa ndio mihimili rasmi pekee ya Dola.
2.0.WAJIBU NA JUKUMU LA VYOMBO VYA HABARI
KATIKA KUSAIDIA WANAWAKE KUFIKIA
MALENGO YA UONGOZI WA KISIASA
Ø Uandishi wa Habari ni taaluma muhimu iliyobeba jukumu
zito la kuihudumia jamii, kwa kuongeza upeo wao wa uelewa, upeo wa kufikiri,
utembuzi na pia uwezo kutambua na
kuchambua masuala tofauti yanayohusu jamii yenyewe yakiwemo , maendeleo yao ,
changamoto zao na hata matatizo
waliyonayo. Na kwamba taarifa zao lazima zilenge kuibua mijadala ya wazi
inayowashirikisha makundi yote, lakini mijadala hiyo ni vyema ilenge kuleta
suluhisho kwa changamoto na matatizo yaliyopo ndani ya jamii hiyo.
Ø Matatizo hayo yanaweza yakawa ya kiuchumi, kisiasa ama
kijamii na kiutamaduni ambapo katika kikwazo kimoja wapo cha wanawake kutofikia
malengo ya uongozi wa kisiasa hutokana na hayo.
Ø Hivyo basi, taaluma hii inahitaji waandishi mahiri sana
wanaofahamu vyema mila na desturi za
jamii zao na mambo yanayoleta vikwazo kwa jamii hiyo, lakini pia lazima
waandishi watambue vyema wajibu wao wa kuwajibika kuisaidia jamii na pia
kutambua vilivyo misingi na mipaka ya majukumu yao ya kuitendaji na kitaaluma.
Ø Kwa ujumla, vyombo vya habari vina wajibu wa kuwapasha
habari na kuelimisha jamii juu ya masuala mbali mbali yanayotokea ndani na nje
ya nchi katika mtazamo wa kuelimisha, kukosoa na kushajiisha utendaji bora,
lakini lazima waelekeze juhudi zao katika kuamsha ari na kuibua mijadala yenye
tija kwa jamii katika kufikia malengo yakiwemo yale ya wanawake katika kushika
madaraka na uongozi wa kisiasa .
Ø Pia vijawajibika kuikosoa jamii na viongozi moja kwa
moja na pia kuelekeza jamii pale haja ya kufanya hivyo inapotokea ili
jamii na viongozi wenyewe waweze kuwa na
mabadiliko sahihi yanayohitajika, ambayo sio tu yanajikita katika mitazamo ya
ndani, lakini lazima mabadiliko hayo yakidhi haja ya kitaifa na kimataifa
kwenye maeneo yote ya siasa , uchumi na utamaduni.
Ø Aidha katika kufikia malengo ya wanawake ya kushika
uongozi wakisiasa na hata nafasi nyengine, waandishi wa habari wanahitajika kubeba dhamana ya
uwajibikaji bora uliotukuka kwa kutenda haki na kuwa wawazi sana katika
shughuli zao za kila siku za kuipasha habari jamii kwenye mambo yanayohusu
vikwanzo vinavyowakwaza wanawake katika jitihada zao za kusaka uongozi wa kisiasa na kutimiza kiu
na malengo yanayofanana na hayo.
Ø Kwa ujumla, katika harakati za wanawake kutafuta na
kufanikiwa kushika madaraka ya uongozi wa kisiasa, vinapaswas kuwa na kazi
zifuatazo za kuwasaidia wanawake:.
Ø Kuandika habari zinazohusu masuala
ya wanawake katika harakati na
mbio za kusaka madaraka ya uongozi wa kisiasa kwa uwazi na zilizotafitiwa kwa
kina zitakazoshajiisha kuwajengea ujasiri, ari na uwezo wa kufikia malengo.
Ø Waandishi lazima kujitahidi kuandika habari za ukweli na
zenye uhalisia na zinazoakisi matukio yenye kupiga vita vipingamizi dhidi ya wanawake katika kila hatua ya
michakato ya chaguzi ikiwa ni pamoja na kushajiisha vyema kwa kuchambua sifa na
uwezo halisi ili wakubalike, sio tu kwenye jamii ya wanawake, lakini pia kwa
jamii kwa jumla.
Ø Kuhakikisha kwamba wanafuatilia taarifa zinazokwaza
jitihada za maendeleo ya wanawake
zinazotolewa mara kwa mara hasa
wakati wa harakati za uchaguzi na hatimaye kuwapa nafasi wanawake kuzungunza
mbele ya jamii kujenga jina na taswira
zao kisiasa.
Ø Ni vyema kwa waandishi wa habari kuaandika sifa halisi za
wanawake wanaoweza kupata nafasi za uongozi, sio tu ule wa kisiasa, lakini hata
kwa wale wanaoteulewa na mamlaka za uteuzi.
Ø
Ni kazi pia ya
waandishi wa habari kufanya kazi kwa
moyo wa kujitolea sana kwa kuwa na agenda makhususi inayolenga maslahi
ya wanawake kushika madaraka ya uongzi
wa umma katika ngazi mbali mbali.
Ø
Waandishi ni
vyema kutumia vyanzo vya uhakika vya
habari na kutoegemea upande wowote na zaidi waepuke masuala yote yanayoweza
kuwa vyanzo vya ukandamizaji wa wanawake
na kuwakosesha haki zao na matumaini ya kushika uongozi.
Ø Wanahabari wanawajibika pia kuzifahamu kwa kina sheria na
taratibu zote zinazoweza kuwa
vipingamizi kwa wanawake sio tu wakati wa uchaguzi ama michakazo ya
kusaka madaraka na uongozi wa kisiasa lakini pia vinavyokandamiza jitihada za kuwajengea uwezo
na ujasiri wanawake.
3.0. KAZI ZA VYOMBO VYA HABARI KATIKA HARAKATI ZA KUWASAIDIA WANAWAKE KUSHIKA
UONGOZI WA KISIASA
Kabla kuzungumzia vyombo vya habari kama nguzo ama kiungo
muhimu cha kuhimiza na kuchapuza kasi ya harakati za wanawake katika kutafuta
na kufikia malengo ya uongozi wa kisiasa , ni vyema kugusia kidogo dhana
ya vyombo vya habari katika kuangalia
kazi za vyombo hivyo kwamba ni kuelimisha , kushajiisha na kuburudisha na
kukosoa kama majukumu ya msingi.
Lakini, katika kazi ya kukuza harakati za wanawake
kidemokrasia vyombo hivi vinapaswa kwenda mbali zaidi katika hatua za
kuhakikisha vinatimiza wajibu wa msingi wa
kuchangia kuimarisha, kulinda, kukuza na kuhifadhi pia kuitetea haki za
wanawake kidemokrasia wakati wote.
Kwa upande mwengne, kama tujuavyo vyombo vya habari ni
daraja ama kiungo muhimu kwa jamii kupata habari na taarifa mbali mbali kutoka
kwa watawala na jamii yenyewe. Hivi pia vinajukumu kubwa la kuisaidia jamii
katika kuleta mabadiko ya fikra na kufikia maamuzi sahihi yanayohitajika ndani
ya jamii kimaendeleo. Mabadiliko hayo huletwa kwa njia mbali mbali kama vile
kuelimisha, kushajiisha, kukosoa, kuelekeza na kujenga ushawishi wa kuibua
mijadala katika mambo mbali mbali ambayo kimsingi yanapotekelezwa jamii hufahamu
na kujirekebisha. Utaratibu huu ndio
unaotambulika kama uandishi wa kuwajibika kwa jamii (social responsible
journalism). Hii ni kutokana na ukweli
kwamba jamii bora haiwezi kujengeka bila
ya vyombo vya habari makini na pia inavyoviaminwai sana na jamii kiasi kwamba wakati mwengine hata viongozi na
wanasiasa hukosa imani hiyo ya wananchi.
Katika kusaidia na kuimarisha uwezo wa wanawake kutimiza kiu ya uongozi wa
demokrasia na pia kuwa watekelezaji wazuri wa majukumu ya serikali na uongozi,
harakati za wawanawake hapa Zanzibar na kwengineko duniani, vyombo vya
habari ni lazima vikubali kuwajibika
ipasavyo katika mambo yafuatayo:.
Ø Kushajiisha uwajibikaji bora kwa wanawake
viongozi
Wanawake viongozi na pia raia ambao huwa wafuasi wao na wanapaswa kuwajibika
vyema tena kwa pamoja ambapo hali hiyo husaidia sana taifa kupiga hatua kwa
vile wote kwa pamoja wagubikwa na hisia za uzalendo wa nchi yao kuchapuza maendeleo bila kujali anayewaongoza ni
mwanamke .
Hapa inasisitizwa uwajibikaji bora utaongeza
ufanisi, kuzuia rushwa, ubaguzi na aina
zote za udhalilishaji wa kijinsia na
hivyo kukuza ufanisi na maendeleo huku ikizingatiwa sana kutobezwa haki za watu
kwa namna yeyote sambamba na viongozi kutekeleza majukumu yao kwa mujibu
wa sheria za nchi. Hivi leo mataifa yote ambayo vyombo vya habari vinafanya
kazi ya namna hiyo wameweza kupigiwa mfano kutokana na ufanisi unaoweza
kupatikana tena kwa kasi kubwa kuliko inavyokisiwa.
Ø Kupima na kuchambua utekelezaji wa sera za
wanawake kiuchumi na Kisiasa
Kwa
kuzingatia ukuaji wa haki za kijinsia katika kusaidia harakati za wanawake
viongozi, Vyombo vya Habari vina wajibu wa kuzifahamu sera zote zinazosimamia
maendeleo sio tu ya wananwake, lakini pia
kiuchumi na kisiasa . Pia lazima wawe na kipaji cha kuzichambua iwapo
sera hizo zina tija, kwanza kwa wanawake na umma kwa jumla. Kufanya hivyo ndio
kusaidia upatikanaji wa maslahi bora kwa
watu ili kazi ya kustawisha na kukuza
uwajibikaji na utekelezaji wake kupitia viongozi wanawake uwe na dhamira ya
kukuza ufanisi na demokrasia.
Ingawa
ni vyema kufahamu kuwa wakati
mwengine sera za mataifa maskini ikiwemo Tanzania, sera za kisiasa na kiuchumi
hugubikwa na msukumo wa mitazamo ya mataifa ya nje na taasisi nyenginezo huku
uwezo wa kuzitafsiri sera hizo kiuhalisia na kwa mitazamo ya ndani
ukashindikana kwa kuwa hukosekana dira madhubuti ya utekelezaji sera hizo
iliyobuniwa na wazalendo wenyewe. Iwapo
vyombo vya habari vitatimiza ipasavyo wajibu huo hapana shaka vitachangia sana
kukuza uwezo wa harakati za wanawake sio tu katika Nyanja za uongozi wa
kisiasa, lakini pia katika maeneo mengine ya nchi kimaendeleo.
Ø Waandishi
kuisaidia kuinganisha nguvu za wanawake na jamii
Ujenzi wa uwezo
wa wanawake bila shaka mtakubaliana name kwamba sio jambo jepesi na ni gharama
na mara nyengine inaweza hata kuchangia kuzalisha mifarakano na misuguano isiyo
ya lazima miongoni mwa wanawake wenyewe kwa wenyewe, wanasiasa , viongozi wa serikali
na hata wananchi hata jamii.
Aidha vyombo
vya habari, lazima vifanye kazi
ya kuhakikisha kwamba wanawasaidia wanawake kwa kuwajenga imani wananchi
kutambua mchango wa wanawake na hivyo kuendelea kuwa kitu kimoja kwa moyo safi
wakiamini kwamba wanawake wanaweza kulisaidia taifa.
Ø Vyombo kuwa kiungo madhubuti kati ya viongozi,
wanawake na wananchi
Vyombo kufanya kazi hii ni jambo muhimu sana
ambapo vyombo vya habari vikiwajibika
kwa umakini juu ya suala hilo ni dhahiri
kwamba nguvu za pamoja katika utekelezaji wa mambo mbali mbali yataweza
kufanikiwa. Haitarajiwi vyombo hivi
vikasadia kujenga fitna na uchonganishi
miongoni mwa wanawake na watawala
na watawaliwa na badala yake ni kuhakikisha kwamba vinawajibika kwa kujenga
taswira njema miongoni mwa jamii , viongozi
na wanawake wanaotafuta nafasi za uongozi wa kisiasa.
Ø Kujenga
ari kwa jamii kuleta mijadala ya maana kwa
wanawake
Kila mmoja
anakiri kwamba mijadala ya wazi inayofanywa na vyombo vya habari kuwahusisha
wananchi wa ngazi mbali mbali ni moja ya msingi muhimu wa kukua na kuanuka
demokrasia katika kuwajengea ari
wanawake ambapo wananchi hupata nafasi ya kupaza sauti zao na kutoa mawazo ,
michango na maelekezo yao ambapo huwa
aina moja ya ushiriki na ushirikishwaji na kwamba serikali sikivu inahitaji sana wananchi kujadili kwa
uwazi masuala mbali yanayowahusu
wanawake binafsi, viongozi wao
waliowachagua na hata wale walioteuliwa ili kuona kwamba ni kweli wanawajibika
ipasavyo kwa kuzingatia matakwa ya kimahitaji sasa naya baadaye katika harakati
za ujenzi wa nchi.
Ø Kujengea
taswira wananchi kuamini na kukubali mabadiliko yanaweza pia kuletwa na
wanawake
Vyombo hivi lazima vifanye kazi ya ziada
kuwaelimisha na kuwapa ujuzi na mawazo mbadala wananchi kwamba ujenzi wa
demokrsia inayozingatia usawa wa jinsia ni matokeo ya mchango wa vyombo vya
habari kutimiza wajibu wake ipasavyo, kwani katika hatua za ujenzi wowote
demokrasia ni kuamini kwamba hata mwanamke anaweza kuwa na mchango mkubwa na
kuwa kiongozi imara wa kushajiisha mabadiliko yanayohitajika.
4.0 VIKWAZO VINAVYOWAKABILI
WANAWAKE KUFIKIA MALENGO YA UONGOZI WA KISIASA
Ø
Ubaguzi wa jinsia na kutozingatia Jinsia
Suala la ubaguzi
wa kijinsia na kutozingatia jinsia kwa vyovyote vile linabakia kama changamoto
kubwa katika jamii kwani wapo watu hadi leo wamekuwa wakiwakosesha nafasi
wanawawake kwa sababu tu ya uwanawake wao na kutofahamu umuhimu wa wanawake .
Hili ni jambo baya ambalo linahitaji kupigwa vita na wanahabari kwani
litakapoachwa litaendelea ni kikwazo kikubwa cha kuwazuia wanawake wenye nia na
moyo ama ndoto za kushika uongozi kufifia.
Ø
Kuhakikisha
kwamba wajitahidi kupiga vita Rushwa
Suala la Rushwa linachukua nafasi pana katika kuwanyima
haki wanaostahiki. Na jambo hili limekuwa likijitokeza sana katika michakato
mbali mbali ya harakati za uchaguzi wa hata ule unaoitwa wa kidemokrsaia .
Kutokana na kushamiri kwake limekuwa likiwaathiri sana
wanawake kukosa kutimiza ndoto zao kwani ikumbukwe kwamba rushwa ni maovu kama
yalivyo mengine ya uvunjivu wa haki za binaadamu , kutowajibika kwa viongozi
ama ubadhirifu wa mali za umma. Waandishi wanapaswa kuwa mstari wa mbele
kufichua na kuyapiga vita maovu ya namna hiyo ili kulifanya taifa kuwa na
demokrsia ya kweli na wanawake wenyesifa waweze kupata nafasi .
Kwa bahati mbaya hata baadhi ya waandishi wamekua na mifano kadhaa hapa
Tanzania kwamba wapo wamejengea utamaduni wa aina hiyo wa kudai wao rushwa na
kuwa wabadhirifu badala ya wao kupiga vita mambo ya namna hii.
Ø
Uwezo duni wa kielemu na kujieleza
kwa baadhi ya wanawake
Hili ni tatizo kubwa kwa baadhi
ya wanawake wenye hamu na nia ya kushika dhamana na madaraka ya kisiasa .
Inahitajika kwa jumuiya na taifa kwa
jumla kujitolea sana kuwasomesha wanawake ili kuwa na elimu ya kutosha
itakayowawezesha kuwa na vigezo vya kiushindani na kuonekana kwamba kiwango
chao cha elimu kinafaa na ni cha kinatosha sana kupewa dhamana mbali mbali za
uongozi. Vyenginevyo, udhaifu huu unaweza kutumika sana kuwadhalilisha na
kuwabagua wanawake wenye nia na hivyo kusababisha
kunyimwa nafasi na fursa wazitakazo kwa wepesi sana.
Ø
Umasikini na kipato duni kwa wanawake waliowengi
Umasikini nao unachukua nafasi
nyengine, kwani badala ya mwanamke kufikiria mbinu bora ya ushindani akili yake
inakuwa mbali kuangalia mahitaji yake muhimu ya kukidhi maisha ya kila siku.
Mwanamke mwenye uwezo mkuwa wa kiuchumi anayo nafasi kubwa kwanza kukubalika
ndani ya jamii miongoni mwa wanawake na hata wanaume lakini pia anayofursa
muhimu ya kuchangia moja kwa mja kutatua kero za wanajamii na hivyo kuonekana
kwamba anafaa sana kuwa kiongozi. Mifumo ya umiliki wa rasilimali inayotoa
ridhaa kwa wanaume kumiliki zaidi nayo
inachangia kuwepo kwa hali ya umasikini kwa wanawake waliowengi.
Ø
Ukandamizaji wa baadhi ya mifumo ya utamaduni, mila na silka
Ukandamizaji nao unachukua nafasi
pana kwani jamii ya wazanzibari na watanzania kwa jumla bado wanaendelea
kuamini na kutumikia mifumo kandamizazaji ambayo haitoi nafasi kwa wanawake
kutimiza ndoto za masuala yao likiwemo hili la uongozi.
Hadi leo bado zipo jamii kutokana
na imani za kiutamaduni, mila na desturi zao zinaamini kwamba kiongozi bora
lazima awe mwanamme jambo ambalo sio sahihi kwani tafiti za kitaalamu
zinaonesha kwamba hata mashirika na taasisi zinazoongozwa na viongozi wanawake
zimepata maendeleo makubwa na ya haraka kuliko zile zinazoongozwa na wanaume.
Ø
Kuwepo misimamo mikali dhidi ya wanawake
Bado ipo misimamo mikali ya
dharau dhidi ya wanawake katika jamii. Wapo watu ambao kwa maumbile tu ya
wawanawake wao wameonekana kutowajali wanawake na hivyo kuwadharau, kuwakebehi
na kuwavunja moyo wanawake wanaopigania mabadiliko ya kimapinduzi ya kukataa
mifumo kandamizi ambayo imekuwa ikiwanyima sana haki na fursa wanazozihitaji za
kushika madaraka na uongozi wa ngazi mbali mbali mbali.
Misimamo ya aina hii bila shaka
ni adui mkubwa wa jitihada za wanawake na inahitaji kupigwa vita ili jamii
iondokane na hali hiyo , ingawa suala hili halipo kwa waliowengi kuwa na
misimamo mikali dhidi ya wanawake lakini dharau zinazotokana na misimamo hiyo
zimekuwa zikileta athari kubwa kwa wanawake.
Ø
Kujiingiza katika makundi
Wapo wanawake ambao hujaribu sana
kutengeneza na kujiingiza kwenye makundi , jambo hili limekuwa likiwaacha nyuma
wanawake wengi ambalo kwa kiasi kikubwa linashabihiana na ubaguzi kuwaona
wengine iwapo hawamo katika kundi fulani basi hawafai. Mathalani imani za
makundi ya siasa nayo imekuwa sumu kubwa katika kuwabeza wanawake na hata
kubezana wao kwa wao ijapokuwa wengine wanauwezo mkubwa, lakini baada ya
kutafautina katika itikadi na imani basi thamani ya mwengine miongoni mwao hushuka
na kuonekana kwamba si wamaana licha kwamba inawezekana kwamba akawa na uwezo
mkubwa kifikra, utendaji na uwajibikaji.
Ø
Baadhi ya wanawake kukosa ujasiri
Baadhi yao wanakosa ujasiri na kujiamini.
Jambo hili limekuwa likiwaathiri sana kwani ujasiri na kujamini ni nyenzo
muhimu katika kufikia malengo ya kushika madaraka ya kisiasa sio tu kwa
wanawake, lakini hata kwa jinsi nyengine. Wanawake wanapaswa kujitambua na kuwa
na ujasiri na moyo wa kujaribu na kujitoa kama walivyo wanaume wakiamini kwamba
kushindana kuna kushinda na kushindwa wala kushindwa isiwe ni sababu ya
kujipima kwamba ni dhaifu sana na kufaulu ikawa ndio sababu ya uwezo
uliotukuka.
Ø
Kutofahamu sera na miongozi mbali mbali inayotetea wanawake
Kikwazo changine ni hichi cha
baadhi ya wanawake kutokufahamu vyema sera na miongozo mbali inayotolewa kwa
ajili ya kusaidia wanawake kufikia malengo ya kushika uongozi wa kisiasa.
Miongozo na sera ni miongoni mwa mambo ya msingi ambayo inaweza kuchangia sana
uhamasishaji, ushajiishaji na kuongeza uelewa katika kupigania haki, umoja na
usawa wa kijinsia. Kutokufahamika ipasavyo inaweza kuwa kikwazo kikubwa ya
mwanamke kutotimiza malengo ya namna hiyo na hivyo kuikosa fursa ambayo
engepaswa kuipata.
5.0. CHANGAMOTO
KWA WANAHABARI KUWASAIDIA WANAWAKE
Katika kutimiza wajibu wao wa kuwasaidia
wanawake kujikwamua na vipingamizi mbali
mbali nchini Wanahabari nao wanakabiliwa na changamoto kadhaa katika kutimiza
wajibu na majukumu yao.
Ø
Uhaba
mkubwa nyenzo za kutendea kazi
Ili kufanikisha kazi za uimarishaji wa haki
na usawa wa kijinsia kwa waandishi kunahitajika kuwepo nyenzo za kutosha
zinazoweza kusaidia utekelezaji wa majukumu yao Ipasavyo . Vyombo vingi na
wanahabari wenyewe hawana uwezo kinyezo kutokana na umasikini unaochangia
kuwepo bajeti na maslahi duni wayapatayo. Wengi wao hawawezi kuwafikia vyema
wanawake hasa wa vijijini katika kuwasaidia pale wanapokuwa na masuala ya
msingi ambayo ni muhimu kufahamika na wengi. Maeneo mengi ya vijiji yana
matatizo kadhaa wa kadhaa ya kijamiii na kiuchumi ambyo kutatuliwa kwake na
serikali ni sehemu ya uimarishaji haki.
Ø
Uwezo
mdogo wa utambuzi na uchambuzi wa sera
Ili kutimiza haja ya uwanaharakati wa
kuwasaidia wanawake, mwanahabari anapaswa kujiamini katika utekelezaji wa kazi
zake kwa kuwa na upeo. Wanapaswa kuwa na uwezo mkubwa wa kutambua na kuchambua
mambo mbali mbali zikwemo sera na sheria au taratibu ili kuwa na uhakika na
kazi zao.
Kuwa na uwezo huo bila shaka ni kuchangia
kukua kwa demokrasia, lakini kwa bahati mbaya waandishi tuliowengi hatuna upeo
mkubwa wa mambo ya namna hiyo. Matokeo yake wengi wetu tumekuwa tukifanya kazi
za uwakala, wa kuripoti yaliyotendwa kwa kuwatumikia baadhi ya watu kwa maslahi
binafisi .
Ø Rushwa na kukosekana moyo wa uzalendo
Katika kazi ya kujenga uzalendo na usawa wa kijinsia
mwanahabari lazima achukue nafasi kubwa
katika kukabili majukumu yake na ni wazi atakumbana na majaribu tofauti ya
kudhoofisha juhudi na uzalendo wake ili alinde maslahi ya mtu ama kundi fulani.
Tunaelewa kwamba baadhi ya waandishi
tumejenga utamaduni wa aina hiyo. Ingawa tunaelewa kwamba rushwa ni dhambi kubwa
ya kimaadili na ni kosa la jinai lakini limekuwa likijitokeza sambamba na
kuwatumikia watu kuwakandamiza wengine.
6.0 HITIMISHO
Kuwepo kwa
mabadiliko ya kujali usawa wa kijinsia yanayopelekea mfumo mbali mbali iliyozoeleka kubadilika na wakati mwengine
kuingiza na kuasisi mipya ya uendeshaji shughuli za uongozi na kiserikali na dola pia ndiko kunakochangia kuwepo kwa matatizo ya kimazoea na utaalamu juu ya utambuzi wake na mbinu sahihi za
kuyakabili . Ikumbukwe kwamba hali kama ya ujenzi na uimarishaji wa haki na
uswa wa jinisia, kimsingi kunahitajika jitihada za pamoja katika kuyapatia ufumbuzi vikwazo , changamoto na matatizo mbali mbali
na kuweza kufikia lengo. Lakini ni lazima wanahabari kuwa bega kwa bega na
wanawake katika kutimiza wajibu na jukumu lao la msingi la kuisaidia jamii katika
kuleta mabadiliko wayatakayo. Haja ya kuwaelimisha
wananchi juu ya umuhimu wa Mfumo mpya na
kuachana na ile ya mazoea kitaifa naKimataifa ni muhimu sio tu hapa Zanzibar na Tanzania kwa jumla lakini ni kila kona ya
dunia .
Vyombo vya habari
vinabaki na nafasi yake muhimu ya kuelimisha, kutoa taarifa, kuhamasisha na
kukosoa , kuelekeza na kuchambua mambo yenye maana na tija kwa jamii hasa
inayohusu maendeleo ya mfumo mbali mbali ya uendeshaji
nchi na haki za wananchi zinavyochungwa, kutunzwa na kulindwa kupitia mifumo
hiyo ya uendeshaji wa dola.
Wanahabari bado wanapaswa wabakie kama ni mkombozi pekee
, sahihi na imara kwa wanawake kwa kuwa na agenda muhimu inayolenga kusaidia
mabadiliko ndani ya jamii .
Jamii inahitaji
waandishi wenye ujuzi na maarifa ya kisera, kisiasa na kimazingira pamoja na
kufahamu vyema utamaduni, mila na silka za jamii ili kuleta mabadiliko sahahi
yanayohitajika.
Aidha, kuna haja
kubwa kwa wanasiasa na viongozi kuweka misimamo mizuri ya utetezi, sio tu kwa
nadharia, lakini katika utekelezaji wa utetezi
wa kweli unaozingatia maslahi kamili ya nchi na wananchi na kuzingatia
sana Usawa na haki za kijinsia kwa kujali Sheria, haki na kuwajibika ipasavyo kwa kila mmoja.
Masuala muhimu yaliyojadiliwa katika uwasilishaji huu yanapaswa kufanyiwa kazi kwa nguvu zote sio tu kwa waandishi wa habari, lakini pia taasisi, wanasiasa na jamii kwa jumla
Ahsanteni
Sana.
MAREJEO
·
Alexander A.J (2003), Taking Sides
Clashing Views on Controversial issues in Mass Media. Dushikin Publishing
Group, USA.
·
Media Council of Tanzania
(2013),Training Manual on Gender and Media.
·
Ayubu Rioba& Fiili Karashani
(2002), Write or not to write Ethical concern in Journalism.
·
John. C. (1998), Studing Media,
Problem of theory and Method, Mc. Graw Hill, USA.
·
Baraza la Habari
Tanzania, (2009), Kupasha habari za Uchaguzi, Ecoprint Ltd. Dar es Salaam, Tanzania.
·
Katiba ya Zanzibar (1984), Toleo la
2010.
·
UNICEF (2003),Haki za Binaadamu,
Nyaraka za msingi.Runjiv Kapur
No comments:
Post a Comment