Habari za Punde

Dk Shein asifu ushirikiano mzuri uliopo kati ya Zanzibar na Jamhuri ya watu wa China



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                 14.06.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa uhusiano na ushirikiano mzuri ndani ya miaka 52 kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China umeweza kuleta mafanikio makubwa katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo hapa Zanzibar.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mazungumzo kati yake na Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China aliyeko Zanzibar Xie Yunliang,  aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kuaga kufuatia kumaliza muda wake wa kazi hapa nchini.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alieleza kuwa China na Zanzibar zinauhusiano wa muda mrefu ambao unaendelea kuimarika siku hadi siku kutokana na nchi hiyo kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta zake za maendeleo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta hizo za maendeleo zikiwemo elimu, kilimo, afya, viwanda, miundombinu na nyenginezo huku akiipongeza nchi hiyo kwa  kuimarisha uchumi wake.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimpongeza Rais wa nchi hiyo Xi Jinping kwa kuanza kutekeleza miongoni mwa miradi waliyokubaliana katika mazungumzo kati yake na kiongozi huyo wakati alipofanya ziara hapa Tanzania pamoja na Dk. Shein alipofanya ziara nchini humo kufuatia mwaliko wa kiongozi huyo.


Aidha, Dk. Shein alitoa pongezi na shukurani za pekee kwa China kwa kuiunga mkono Zanzibar katika ujenzi wa Hospitali ya Abdalla Mazee huko kiswani Pemba ambapo ujenzi wake huo  unatarajiwa kukamilika kati ya mwezi Ogasti  na Septemba mwaka huu.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa ufadhili pamoja na nafasi za masomo zinazotolewa na nchi hiyo kwa Zanzibar nazo zimeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini.

Pia, Dk. Shein aliipongeza nchi hiyo kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya kwa kuendeleza utamaduni wa kuwaleta Madaktari bingwa kutoka nchini humo wakiwemo kutoka Jimbo la Jiangsu.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa kuwepo kwa ziara za viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na viongozi wa siasa kati ya nchi hiyo na Zanzibar zitazidisha kupanua wigo wa maendeleo kati ya viongozi wa pande mbili hizo.

Dk. Shein alisema kuwa kumalizika kwa ujenzi wa jengo jipya la abiria katika kiwanja cha ndege cha Abeid Amani Karume kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza idadi ya wageni wanaokuja kuitembelea Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa idadi ya Mashirika ya ndege kufanya safari zao hapa nchini.

Nae Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China aliyeko Zanzibar Xie Yunliang ambaye anamaliza muda wake wa kazi hapa Zanzibar alimuhakikishia Dk. Shein kuwa nchi yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar kwa lengo la kuzidisha uhusiano uliopo.

Balozi Xie aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa mafanikio makubwa yaliopatikana katika kuimarisha na kuendeleza sekta za maendeleo na sambamba na kukuza uchumi Zanzibar.

Balozi huyo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa chini ya uongozi wa Rais Xi Jinping China itaendelea kuiunga mkono Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa mazungumzo yote yaliyofanyika kati ya kiongozi huyo na Dk. Shein yanafanyiwa kazi ya utekelezaji.

Pamoja na hayo, Balozi Xie alisema kuwa nchi yake itahakikisha inaendeleza ujenzi wa miradi yote iliyoanzishwa hapa Zanzibar pamoja na kuendeleeza mengine mipya huku akisisitiza kuwa  ujenzi wa kiwanja cha Mao Tse Tung unaotarajiwa kuanza hivi karibuni ni fahari kwa nchi hiyo kwani inalitukuza jina la kiongozi mkuu wa nchi yao.

Aidha, Balozi huyo alimueleza Dk. Shein kuwa ujenzi wa Hopsitali ya Abdalla Mzee iliyopo kisiwani Pemba unatarajiwa kumaliza kati ya Ogasti na Septemba mwaka huu huku akimueleza kuwa ujenzi wa Bandari mpya ya Mpigaduri tayari mchakato wake umeanza pamoja na ujenzi wa jengo jipya la abiria katika kiwanja cha ndege cha Abeid Amani Karume nao umo ukingoni kumalizika.

Balozi huyo mdogo alisema kuwa China itaendelea kutoa nafasi za masomo na ufadhili kwa Zanzibar pamoja na kueleza azma ya nchi hiyo kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha uvuvi wa bahari kuu.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.