HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA MAWASILIANO NA UJENZI
KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI
YA WIZARA YA ARDHI, MAJI, NISHATI NA MAZINGIRA KWA MWAKA WA FEDHA 2016/2017
Mheshimiwa Spika,
Awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi
Mungu mtukufu, Mwingi wa Rehema na Mwenye Kurehemu aliyeumba Mbingu na Ardhi,
ambaye ametujaalia uzima na afya njema na kutuwezesha kukutana hapa leo tukiwa
ndani ya Baraza lako tukufu, tukitekeleza majukumu yetu mbali mbali ya
kuwatumikia wananchi wetu ambapo leo tunajadili Bajeti ya Wizara ya Ardhi,
Maji, Nishati na Mazingira kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Spika,
Kwa dhati kabisa, napenda
pia kukushukuru wewe binafsi Mheshimiwa Spika kwa kunipa nafasi hii ya
kuwasilisha Maoni ya Kamati ya Mawasiliano na Ujenzi kuhusu Makadirio ya Mapato
na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kwa mwaka wa fedha
2016/2017.
Mheshimiwa Spika,
Nichukuwe nafasi hii pia kumpongeza Waziri na Naibu Waziri wa Wizara ya
Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Mheshimiwa Salama Aboud Talib, Mheshimiwa
Juma Makungu Juma pamoja na Katibu Mkuu alhaj Alkhalil Mirza na watendaji
wengine wote wa Wizara hii kwa
mashirikiano yao ya dhati kwa Kamati
wakati wote tulipokuwa tukipitia na kujadili Bajeti ya Wizara hii. Tunawashukuru
sana.
MheshimiwaSpika,
Aidha, napenda kuipongeza tena Wizara ya Ardhi, Maji,
Nishati na Mazingira kwa kuweza kuwasilisha mbele ya Baraza lako tukufu Bajeti ya Wizara hiyo kwa
mwaka wa fedha 2016/2017 kwa umahiri na ufanisi mkubwa katika mfumo wa bajeti
unaozingatia programu “Program Based Budget”(PBB).
Mheshimiwa Spika,
Sitakuwa nimetenda haki iwapo nitaendelea na hotuba hii bila ya kutoa
shukurani za pekee kwa Waheshimiwa Wajumbe na Makatibu wa Kamati yangu, ambao
tumeshirikiana kwa umoja wetu kuyapitia na kuyachambua makadirio haya ya Bajeti
ya Wizara hii na hatimae kuyakubali bila ya marekebisho yoyote.
Mheshimiwa Spika,
Kwa kuheshimu, kuthamini na kutambuwa mchango wao mkubwa kwenye Kamati hii
hadi kufanikisha kazi hii iliyokusudiwa, naomba niwataje kwa majina Waheshimiwa
Wajumbe na Makatibu wa Kamati hii ya Mawasiliano na Ujenzi ya Baraza la
Wawakilishi kama ifuatavyo:-
1. Mhe. Hamza Hassan
Juma Mwenyekiti
2. Mhe. Suleiman
Sarhan Said M/Mwenyekiti
3. Mhe. Abdalla Ali
Kombo Mjumbe
4. Mhe. Nassor Salim
Ali Mjumbe
5. Mhe. Said Omar
Said Mjumbe
6. Mhe. Mohamedraza Hassanali Mjumbe
7. Mhe. Bahati Khamis
Kombo Mjumbe
8. Mhe. Kadija Omar Kibano Mjumbe
9. Mhe. Mwanaidi Kassim
Mussa Mjumbe
10. Ndg. Fatma Omar Ali Katibu
11. Ndg. Himid Haji
Choko Katibu
MheshimiwaSpika,
Kwa mwaka wa fedha
2015/2016, Baraza la Wawakilishi ililiidhinishia Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati
na Mazingira Matumizi yenye jumla ya Tshs. 7.198, 900,000 bilioni kwa ajili ya
Fungu N01 kwa matumizi ya kazi za kawaida. Aidha, Baraza pia ililiidhinishia
Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kutumia jumla ya Tshs.
28.750,560,000 bilioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za maendeleo. Vile vile,
kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara iliidhinishiwa kukusanya jumla ya Tshs.
4,799,625,000 bilioni kama ni mapato yatokanayo na vianzio mbali mbali katika
Taasisi zake, ambapo hadi kufikia Machi, 2016 Wizara ilikuwa imeshakusanya
jumla ya Tshs. 3,596,948,678 ambazo sawa na asilimia 75% ya makadirio kwa mwaka
MheshimiwaSpika,
Imeelezwa katika
hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kwa mwaka huu
wa fedha 2016/2017 Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira imepangiwa jumla
ya Tshs.9,555,400,000 bilioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida na Tshs.
47,900,786 bilioni kwa ajili ya kazi za maendeleo. Aidha, Wizara
inakadiriwa kukusanya jumla ya Tshs.
6.100,000,000 bilioni kutoka katika vianzio mbali mbali vilivyomo katika
Taasisi zake.Aidha, katika utaratibu mpya wa Bajeti inayozingatia Programu
(PBB), Wizara hii imepangiwa kutekeleza Programu Kuu Nne (4) na Programu Ndogo
Nane (8). Kama zilivyofafanuliwa wakati hotuba hiyo ya Bajeti ya Wizara ya
Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu kama Kamati nyingine imefanyakazi ya
kuipitia na kuichambua bajeti katika mzingira magumu kwani imekubali kupitisha
mipango na bajeti zake bila ya hata kwenda kukagua na kuona hizo shughuli
zilizopangwa kutekelezwa hasa kutokana na kuchelewa kuanza shughuli zetu
Barazani katika kipindi hiki lakini nnaamini kua kwa Bajeti ijayo tutaweza
kumsaidia sana Mhe.Waziri kwa kumpa ushauri mzuri katika kufanikisha majukumu
yake.
Kamati yangu pia inasisitiza Wizara kuwa makini sana na matumizi ya fedha
zitakazoingizwa katika Programu hizo kwani licha ya uhaba wa fedha, matokeo ya
fedha zitakazoingizwa yatahitaji kuonekana na kupimwa kwa umakini na ufanisi mkubwa hususan katika
utekelezaji wa Programu hizo Muhimu.
PROGRAMU YA USIMAMIZI WA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI
Mheshimiwa Spika,
Kama ilivyoelezwa Programu hii kuwa ina jukumu kubwa la
kuhakikisha kunakuwepo upatikanaji wa Huduma bora za Nishati, Umeme na Maji katika Visiwa vyetu hivi viwili kwa upande wa
Unguja na Pemba pamoja na visiwa vidogo vidogo vinavyoishi watu hapa Zanzibar,
kuzingatia na mahitaji ya wananchi wetu. Aidha, kupitia Programu hiiutekelezaji
wake ni Usimamizi wa usambazaji wa mafuta nchini, Usambazaji wa huduma za umeme,
Uhifadhi wa maeneo ya vianzio vya maji, Upatikanaji wa huduma ya maji safi na
salama kwa watumiaji wa mijini na vijijini.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu kupitia Programu hii inapenda kuchua fursa
hii tena kuwapongeza Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kupitia
Mamlaka yaMaji (ZAWA), kwa jitihada zao kubwa za kuhakikisha kuwa hadi wananchi
wanaoishi vijijini kuwa wanapata huduma ya maji safi na salama. Kama tunavyojua
kwa upande wa usambazaji maji vijijini kwa hivi sasa Zanzibar inaongoza kwa
Nchi za Bara la Afrika kwa kuwafikishia huduma ya maji huko vijini, pamoja
kwamba bado kuna baadhi ya vijiji bado havijafanikiwa kupata huduma hii lakini
kupitia mradi wa uchimbaji visima wa Raas-El- Khaima tunategemea kwa kipindi
kifupi tu cha hapo baadae basi wananchi wengi zaidi wataweza kupata huduma ya
maji safi na salama katika vijiji vyao. Aidha,changamoto kubwa tunayoiona kwa
kuvikamilisha visima hivyo kwasababu mkataba wake ni kuchimba visima tu lakini
huduma nyingine za ununuzi wa Pump na usambazaji wa mabomba ni jukumu la SMZjambo
ambalo bado kutokana na gharama kubwa linaweza kuchukua muda mkubwa kuweza
kukamilisha visima hivyo ili kuwezakufanikiwa kutoa huduma hiyo, kwa kua hivi
sasa visima vingi tayari vimeshachimbwa kupitia mradi huo na uwezo wa Serikali
kupitia Mamlaka kwa hivi sasa ni mdogo kuweza kukamilisha, basi tunamuomba Mhe. Waziri kufanya safari maalum
kwenda Raas-El-Khaima ili kufanya mazungumzo zaidi ili Serikali ya
Raas-El-Khaima waongeze mkataba mpya wa kusaidia kusambaza maji kupitia visima
hivyo, kwani lengo la mradi huo ni kuwaondolea wananchi tatizo la upatikanaji
wa maji kwani maji yameshapatikana lakini hayajawafikia wananchi kama
ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Spika,
Pamoja na jitihada hizo za Serikali kuwasogezea huduma ya
maji safi na salama wananchi wake, lakini bado kuna wananchi ambao wanajenga
karibu na vianzio vya maji na kupelekea uhaba wa upatikanaji wa maji lakini pia
kuchafua maji kutokana na uchafu wa majumbani.
Mheshimiwa Spika,
Kama tulivyoeleza upatikanaji wa maji vijijini umepiga hatua
kubwa lakini bado kwa Mkoa wa Mjini na Magharibi hususani Wilaya ya Mjini
Unguja bado tatizo la upatikanaji wa maji limekua ni tatizo kubwa kwani kuna
baadhi ya maeneo upatikanaji wake ni mdogo sana jambo ambalo linawafanya
wananchi wengi kununua maji ambayo hawana uhakika wa ubora na usafi na bila ya
kujua yanatoka wapi. Kamati yangu inataka kujua vipi ule mradi wa Japan kupitia
Mkoa Mjini naMagharibiambao ulitegemewa kuliondoa tatizo hilo sijui umefikia
wapi? Pamoja na changamoto mbali mbali zinazoikabili Mamlaka ya Maji kwa kua
kamati yangu haikupata muda wa kuweza kukagua na kujua matatizo ya Mamlaka hii
naomba kamati yangu ipewe muda tunaamini kwa mwaka ujao baada ya ukaguzi
tutaweza kuishauri vizuri Serikali kupitia Mamlaka ya Maji ili kuhakikisha
wananchi wote ambao mtandao wa maji umepita basi wanapata huduma ya maji kama
inavyotakiwa.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inaitaka Mamlaka ya maji kwa kushirikiana na
masheha kuandaa utaratibu wa mawasiliano ya karibu ili kutoa taarifa ya mabomba
yanayovuja maji kwani kuna maeneo mengi hapa mjini mabomba ya maji huwa
yanavuja maji kwa muda mrefu bila kufanyiwa ukarabati kwa wakati na hii pia
hupelekea maji mengi kupotea na kuwakosesha wengine kupata huduma hii muhimu
kwa binaadamu.
Mheshimiwa Spika,
Vilevile, Kamati yangu inaitaka Mamlaka kuweza kuwaajiri
vijana ambao wapo Wizarani kwa muda mrefu na wengine wanadhamana muhimu lakini
bado wapo kama wafanyakazi wa muda bila ya kuajiriwa,hii inaweza kupelekea
kutokua waaminifu na kuweza kufanya udokozi kwani hawana uhakika wa ajira yao,
Hivyo, Kamati yangu inaitaka tena Mamlaka kuweza kuwapatia posho la usafiri
linalostahiki kwa watumishi wao ambao hupangiwa kufanya kazi mashamba kwani
mshara wao sehemu kubwa huutumia kwa usafiri jambo ambalo huwarudisha nyuma
katika mipango yao ya kimaisha.
Mheshimiwa Spika,
Pia, Kamati yangu kupitia Programu hii inaiomba Wizara
husika kuwaongezea uwezo na ujuzi watendaji wa Mamlaka ya Maji (ZAWA) katika
utendaji wao wa kazi za kila siku. Ili kuweza kuondoka na kadhia ya utendaji wa
kazi kimazoea hali ambayo kupelekea kuikosesha Serikali mapato kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika,
Kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana katika maeneo
yetu ya mjini na vijijini kwa Unguja na Pemba. Kamati inaishauri Mamlaka ya
Maji (ZAWA) kuanzisha utaratibu
maalum wa ulipaji wa ada yamaji kwa njia ya simu za mkononi ili kuongeza wigo
wa ukusanyaji wa mapato ya huduma ya maji, kwani wakati mwingine mtu huwa
anaona taabu ya kufuata maeneo ya kulipia maji lakini kupitia huduma ya simu ya
mkononi ni wakati wowote anaweza kulipa bila ya usumbufu wa aina yetote, pia
kamati yangu inaitaka mamlaka kuboresha huduma zao za ulipaji bili za maji
kwani inaonekana hauko salama sana na unashawishi mkusanyaji kuweza kuchota
kwani pesa ina bilisi mbaya, pia tunaishauri Mamlaka ya Maji kutengeneza
Database ya wateja wake wote ambao wanaopata huduma ya maji ili kuweza kua na
uhakika wa makusanyo wanayoyarajia kuyapata kwa kila mwezi, katika utaratibu
huo wanaweza kuweka utaratibu wa kulipa kwa mwaka au kila miezi mitatu au sita jambo
ambali litaweza kuongeza mapato na ya uhakika zaidi, pia katika kuboresha
mapato na kudhibiti matumizi ovyo ya maji basi Kamati yangu inashauri Mamlaka
inunue mita za kusoma maji yanayotumika na kutoa bili sahihi kwa mtumiaji.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inaishauri Mamlaka ya Maji kwa kuweka mabomba yalioimara ili kuweza kuwarahisishia
wananchi kupata huduma hizo kwa urahisi. Pia kubadilisha yale mabomba ya zamani
yaliyochakaa ambayo baadhi yao yamekua yakivujisha maji, na mengine hata spea
zao zimekua taabu kupatikana kwenye soko kwa hivi sasa.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu haijaridhika hata kidogo kutokana na kiwango
kidogo cha makusanyo ya ada ya maji ambapo kama alivyoelezea Mhe. Waziri kuwa
kati ya malengo waliyojiwekea kukusanya Tshs. 5.1 Bil hadi March wameweza
kukusanya 1,9 Bil kiasi cha asilimia 37% tu, kiasi hiki ni kidogo sana kwa hiyo
tunaitaka Mamlaka kuhakikisha kwa mwaka ujao wanaweza kukusanya pesa zote
walizokadiria na kama nilivyoelezea hapo mwanzo Kamati yangu inaahidi kutoa
msaada wa mawazo na fikra mpya ili kuhakikisha kwa mwaka ujao lengo hili
linafanikiiwa kwa 100%.
SHIRIKA LA UMEME
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inalipongeza sana Shirika la Umeme Zanzibar
kwa kuweza kuwapatia huduma ya umeme wananchi wote wa Zanzibar mijini na
vijini, kama ilivyo huduma ya maji Serikali yetu kupitia Shirika la Umeme
imeweza kuwasambazia huduma hii wazanzibari karibu asilimia 80 ni mfano wa
kuigwa katika nchi za Afrika ya Mashariki na kati pamoja na Nchi nyingine za
Dunia ya tatu, kutokana na huduma hii hasa vijijini wananchi wengi wamekua
wakijiongezea mapato kupitia biashara mbali mbali ikiwemo sekta ya uvuvi. Pia
Kamati yangu inalipongeza Shirika la Umeme kwa kuweza kuwapatia wananchi huduma
wa uungaji wa Umeme kwa njia ya mkopo kwani hali za wananchi wetu kiuchumi ni
duni lakini kupitia huduma hii imeweza kuwaungia kwa malipo kupitia bili zao,
hii pia imeweza sana kuwapunguzia umaskini.
Vilevile,Kamati inaishauri Wizara kukaa pamoja na Shirika
la Umeme, ili kuweza kutafuta mbinu mbadala ya kulitatua tatizo la foleni
katika vituo vinavyotoa huduma za uuzaji umeme hususan kwa Wilaya ya Mjini
(Unguja).Aidha,Kamati inaishauri Wizara kupitia Shirika la Umeme, Zanzibar
kuongeza vituo vya uuzaji umeme huo katika maeneo mbali mbali ya mjini ili
wananchi waweze kuondokana na usumbufu unaojitokeza katika vituo hivyo.
Mheshimiwa Spika,
Kutokana na hali hiyo, Kamati yangu haikusita kuishauri
Shirika la Umeme, Zanzibar kuanzisha kituo kimoja cha kuuzia umeme kisiwani
Pemba katika mji wa ChakeChake. Ili kuweza kuwasaidia wananchi kupata huduma
hii kwa wakati na wepesi zaidi.
Mheshimiwa Spika,
Kamati pia inasikitishwa na taarifa za ucheleweshwaji wa
mapato kutoka katika taasisi za Serikali ya Zanzibar na baadhi ya Jamhuri ya
Muungano ambayo yangeliweza kulisaidia
Shirika la Umeme katika kutimiza majukumu yake suala ambalo linachangia
kwa kiasi kikubwa kudhoofisha kazi za ZECCO ikiwemo kutoa huduma kwa wateja
wapya na kulipia madeni makubwa yanayoikabili kutoka Tanesco. Kwakuwa Kamati
yangu inaamini taasisi zote zinaingiziwa fedha katika vifungu vyao ambazo wanatakiwa
kulipa bili ya Umeme. Kamati yangu kwa bajeti inayokuja haitokubali kuipitisha
Bajeti ya Wizara yoyote ambayo inadaiwa na Shirika la Umeme kwani wanalipa
mzigo mkubwa wa madeni Shirika ambalo bado linatoa huduma ya Umeme kwa hasara
kutokana na bei wanayouziwa na Tanesco, kwa hiyo Kamati inatoa angalizo hili
kwa Mawaziri kwani shughuli zao bila ya Umeme basi hawawezi kutoa huduma katika
taasisi zao, ili kuweza kuondoa kadhia hiyo bado Kamati yangu inaitaka Shirika
la Umeme kuwawekea Mitre za Tukuza Wizara zote ili kuliwezesha Shirika kufanya
kazi zake kwa ufanisi na kuondokana na mzigo wa madeni wa kila siku kutoka
Tanesco, na kwakua katika Bajeti ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano Waziri wa
Fedha wa SMT alieleza kua suala la madeni ya Bili ya umeme kwa taasisi za SMT
hivi Serikali kupitia Wizara ya Fedha ya SMT zitalipwa moja kwa moja kutoka
kwenye mafungu ya Wizara Kamati yangu imefarijika na mpango huo ,kwa hiyo
tunamuomba Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme kumuandikia Katibu Mkuu Wizara ya
Fedha SMT na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi SMT kuhusu deni lao pamoja bili
mpya ili kuwajuulisha kua malipo mengine yalipwe moja kwa moja kwa Shirika la
Umeme Zanzibar,kwa hiyo hili naomba Waziri alifanyie kazi kupitia ZECO. Kamati
yangu hadi tunaandika ripoti hii Shirika linazidai taasisi hizo za Serikali
karibu Tshs.30,046,626,237.98 kwa
kweli hili deni kubwa sana nawaomba waheshimiwa tulisaidie Shirika letu kuweza
kupwa pesa zao ili liweze kutuhudumia ipasavyo.
Mheshimiwa Spika,
Kwa upande wa Pemba Kamati yangu inaishauri Serikali
kuwavutia wawekezaji katika kisiwa cha Pemba ili kuweza kusaidia kununua huduma
ya Umeme kwani Shirika linapata hasara kubwa kwa kulipa gharama kubwa kwa
Tanesco kwa Umeme katika kisiwa cha Pemba kulingana na mapato yanayopatikana
katika kisiwa cha Pemba.
Pamoja na hayo Kamati yangu inalitaka Shirika kujiandaa
na upatikanaji wa Gesi asilia hapa Zanzibar ili kuweza kuzalisha Umeme kwa bei
ndogo kupitia umeme wa Gesi kama ilivyo kwa upande wa wenzetu kule Tanzania
Bara, kwani bado wananchi wetu wanapata huduma ya umeme kwa gharama kubwa.
Mheshimiwa Spika,
Pamoja na yote, Kamati
yangu inalipongeza Shirika kwa utoaji wao wa huduma kwa haraka hasa pale
inapotokea hitlafu kwenye maeneo tofauti bila ya kujali wakati ikiwa usiku au
mchana. Kamati yangu pia inalipongeza Shirika kwa kuhakikisha wateja wote hivi
sasa wanapatiwa huduma ya Umeme wa Tukuza jambo ambalo litasaidia kuongeza
mapato kwa Shirika.
IDARA YA NISHATI NA MADINI
Mheshimiwa Spika,
Naipongeza Idara hii yahuduma zaNishati kwa kazi nzuri
inazozifanya na tafitinyingi wanazozifanya hasa kwa upatikanaji wa Umeme
mbadalaikiwemo upepo na Solar kwa kushirikiana na Mashirika mbali mbali ya Kimataifa,
pamoja na pongezi hizo lakini tunaitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati ya Maji
na Mafuta (ZURA) katika kudhibiti
mwenendo wa biashara ya uagizaji na uingizaji wa mafuta wawe makini sana kwani
hivi sasa kuna malalamiko mengi kwa baadhi ya watumiaji wa mafuta kwenye
vipando ikiwemo magari wakati mwingine huuziwa mafuta machafu ambapo hupelekea
kuwatia hasara kubwa kwa uharibifu katika mashine zao za magari kutokana na
mfuta machafu yasiyokua na viwango. Kutokana na hali hiyo, Kamati yangu
inaitaka Wizara kuhakikisha inatafuta Kampuni ya kuyapima na kuyakagua viwango
vya mafuta kama wanavyofanya wenzetu T’bara kwa upande wa Mamlaka ya Kudhibiti
Mafuta ( EWURA).
Mheshimiwa Spika,
Katika suala hili tunamtaka Mhe.Waziri akija kufanya
majumuisho atuelezee wananpango gani wa kuwa na taasisi kama hiyo hapa Zanzibar
ili kupunguza hasara kwa wenye vyombo vya moto kwani hata wakipata matatizo hakuna
fidia yoyote wanayolipwa aidha na Mamlaka au wamiliki wa vituo vya mafuta.
PROGRAMU YA USIMAMIZI WA MAZINGIRA NA MABADILIKO YA TABIANCHI
Mheshimiwa Spika,
Lengo kuu la Programu hii ni kuhakikisha usimamizi
thabiti wa masuala yote yanayohusiana na mazingira na kudhibiti athari za
kimazingira na mabadiliko ya tabianchi. Aidha, hapo awali utekelezaji wa
Programu hii ulikuwa ukitekelezwa na Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais na baada
ya mabadiliko ya Wizara utekelezaji wa Programu hii utasimamiwa na Wizara ya
Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira.
Mheshimiwa Spika,
Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Programu hii iliombewa
kuidhinishiwa kutumia jumla Tshs. 624,076,000 kwa ajili ya utekelezaji wa
Programu hii ya Usimamizi wa Mazingira
na Mabadiliko ya Tabianchi. Aidha, kati ya fedha hizo zilizoidhinishwa
ilikuwa Tshs. 174,076,000 kutoka Serikalini na Tshs. 450,000,000 kutoka kwa
Washirika wa Maendeleo.
Mheshimiwa Spika,
Kutokana na Umuhimu wa kudhibiti matumizi mabaya ya
kimazingira yanayoendelea katika baadhi ya sehemu kwa upande wa Unguja na
Pemba. Kamati inaiomba Wizara kupitia Mradi wa Usimamizi wa Mazingira na
Mabadiliko ya Tabianchi utakaosimamiwa na wafadhili wa UNDP, DFID na AFDB
pamoja na Serikali yetu, kuweza kutoa
elimu kwa wananchi kupitia vyombo vya habari mbali mbali juu ya umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na
kuzisaidia jamii katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.Aidha,
Kamati pia inaishauri Kamati zote za
masheha kuunda Kamati za mazingira katika Shehia zao ili kuweza kusaidia na
kulinda maeneo yetu yasiharibiwe na yalindwe kwa mujibu wa Sheria za Mazingira.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu imegundua hivi sasa kuna maeneo mengi hapa
Zanzibar hasa yaliyoko kwenye fukwe mbali mbali hivi sasa yamekua yakivamiwa na
maji ya Bahari na hata kwenye maeneo ambayo yalikua wanachi wakiyatumia kwa
ajili ya Kilimo hivi yamejaa maji chumvi ya Bahari hasa kwa upande wa kisiwa
cha Pemba, watu wengi wameingia kwenye umasikini baada ya maeneo yao ya kilimo
kuingia maji ya chumvi, kwa upande wa ukanda wa Maisara kwa Unguja hata yale
maeneo ambayo tumekua tukiyatumia kwa ajili ya kufanya mazoezi kwenye fukwe
hivi yameanza kujaa maji na inakua shida kuyatumia wakati wa maji kujaa wakati
hapo mwanzo tukiyatumia muda wote.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inaomba ufafanuzi kuhusu Zanzibar
inavyofaidika na misaada ya kimataifa kupitia programu za Kimataifa za kusaidia
hifadhi ya mazingira Duniani kama ipo basi tungelipenda kuona ni miradi gani
tunayosaidiwa, kwani tunasikia katika mikutano mbali mbali ya Kimataifa kuwa
mataifa ya Dunia ya tatu yamekua yakidai fidia ya uharibifu wa Mazingira
unaofanywa na Mataifa makubwa Duniani kupitia moshi wa viwanda vyao ambo
unaathiri sana uharibifu wa “OZONE LAYER”ambapo inasababisha joto kali lakini
pia husababisha mvua kubwa sana za” Alninyo” na mfano mzuri mvua za hivi
karibuni zilizonyesha hapa Zanzibar zimesababisha maafa makubwa sana lakini
hatukusikia mfuko wa mazingira kuweza kuwasaidia wananchi walioathirika, kwani
kuna maeneo tangu tuzaliwe yalikua hayajai maji lakini hivi sasa miji yote
wakati wa mvua basi wananchi tunasubiri kuzama jambo ambalo wazanzibari
tumeanza kuingia kwenye taharuki kubwa hadi mvua zipite kwa hiyo suala hili ni
lazima tupate maelezo ya kina sababu zinazosababisha mvua siku hizi kuwa kubwa
sana na joto kwa nini limekua kali sana. Lakini pamoja na yote hayo Idara hii
inafanya kazi nzuri na tunaomba waendelee na jitihada hizo za kutupatia elimu
ya mazingira.
MheshimiwaSpika,
Kama nilivyoeleza hapo mwanzo kwa kua Kamati yangu
haikuwahi kufanya ziara kwenye Wizara na kuona utendaji wao nitamuomba Waziri
akija hapa aje atueleze kuhusu baadhi ya miradi mikubwa inayojitokeza hapa
Zanzibar hususan Mradi wa Ujenzi mkubwa unaoendelea hapo Mtoni Unguja mradi
ambao unafukia eneo la Bahari kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja cha michezo ya
baharini na michezo mingine ya watoto , kamati yangu inataka kujua tu je ni
athari gani inaweza kupatikana kupitia mradi ule? Je mradi ule hautoathiri
mkondo wa njia ya Meli kubwa zinazopita kuingia kwenye Bandari ya malindi na
ujenzi mpya wa Bandari ya Mpiga Duri?.
Mheshimiwa Spika,
Kwakua mradi huu ni mpya kwa hapa kwetu basi ni vyema
tukapata taarifa sahihi kutoka Serikalini kwani katika nchi ya Dubai walipoanza
kufukia Bahari na kujenga kisiwa na baadae kujenga Hoteli kulijitokeza athari
nyingi ikiwemo maji ya Bahari kupanda kwenye maeneo mengine lakini kwa kuwa
wenzetu wanauwezo mkubwa kiuchumi waliweza kuidhibiti hali hiyo,
PROGRAMU YA USIMAMIZI NA UPANGAJI WA MATUMIZI YA ARDHI
Mheshimiwa Spika,
Miongoni mwa majukumu makuu ya Programu hii ni kuhakikisha kunakuwepo na usalama katika
matumizi ya ardhi kwa maendeleo ya nchi yetu kiujumla. Aidha, Kamati yangu
inaiomba Wizara husika kuwa makini katika utekelezaji wa Programu ndogo
zilizomo ndani ya Programu hii kuu.
Mheshimiwa Spika,
Kama inavyofahamika kuwa moja kati ya changamoto
inayowakumba wananchi wetu ni usalama wa umiliki wa ardhi zao, usajili wa ardhi
kiholela (kinyume na taratibu za kisheria) pamoja na utatuzi wa migogoro ya
ardhi inayoendelea kila muda ukisonga mbele katika Mahakama zetu za ardhi. Na
kamati yangu inaamini kadhia hii itamalizika tu pale ule mpango wa Wizara wa
kusajili ardhi yote na kuwamilikisha wahusika basi kadhia hii itaisha kwani
kuna maeneo mengi hasa kwetu vijini kuna mashamba ambayo tumerithishwa na wazee
wetu kutokana na uzoefu tu lakini hata wao baadhi yao hawana hata hizo hati
miliki lakini wameshajenga, wanalima na vijukuu vyao pia wanaendelea na maisha
hapo, kwa hiyo mpango huo utasaidia kuondoa tatizo hilo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu imegundua kutokana na matatizo mengi
yaliyojitokeza hasa kunyanganywa baadhi ya wawekezaji maeneo yao na mengine
kufutwa kinyume na taratibu na mengine pia kuundiwa Kamati Teule na Baraza hili
lakini hadi leo hutukuletewa taarifa ya utekelezaji wa maamuzi ya Baraza hadi
leo hatujui kilichoendelea kwa hiyo ni vyema basi Wizara ikaandaa taarifa
maalum ya utekelezaji wa maagizo yale ili kujiridhisha kua ile kazi kubwa
iliyofanywa na Baraza na kutumia pesa nyingi imeleta matunda gani kwa jamii,
lakini pamoja na hayo tunamuomba Waziri kuweza kuwarejeshea maeneo yao wale wawekezaji
ambao tayari wanataka kuekeza kwenye Miradi Mikubwa ambayo itaongeza ajira kwa
watu wetu lakini pia kuongeza wigo wa mapato yetu hasa ukizingatia kua Bajeti
hii inalenga kutegemea mapato ya ndani zaidi kuliko kutegemea misaada kutoka
nje ambapo kwa miaka ya hivi karibu imekua na masharti magumu kila kukicha.
Mheshimiwa Spika,
Kamati pia inaomba Kamisheni ya Ardhi kuandaa utaratibu
maalum wa kutoa elimu kwa wananchi juu ya matumizi mabaya ya Ardhi na athari
kwa pamoja, ili kuweza kuondokana na kadhia hii ya migogoro ya ardhi zinazouzwa
na kusajiliwa kinyume na taratibu zilizowekwa kisheria. Kutokufanya hivyo, ni
kuiongezea mzigo Serikali na kuikosesha mapato yatokanayo na wawekezaji.
Mheshimiwa Spika,
Katika eneo hili tunakuomba Mhe. Waziri uwe mkali hasa
kwa baadhi ya waekezaji ambao wameyachukua maeneo yao kwa ajili ya uwekezaji
pamoja ya kuwa Ardhi ni mali ya Serikali lakini mwananchi anapokubali kupisha
muekezaji basi alipwe fidia kwa mujibu wa makubaliano na sio kutumia nguvu na ubabe
katika kuwadhulumu wanyonge haki zao. Aidha, katika jambo hili Kamati yangu haitokuwa
tayari kuwaona wananchi wetu wakipokonywa haki zao za matumizi ya Ardhi zao na
matajiri kwa kutumia uwezo wa kifedha waliokuwa nao, kwani na wao ni raia wa
Nchi hii na ni wajibu wao kufaidi matunda ya Mapinduzi Matukufu ikiwemo
kumiliki Ardhi zao. Na katika suala hili Kamati yangu inaahidi kuwasaidia
wananchi wake kwa kila njia.
MAHKAMA YA ARDHI
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inaipongeza Wizara kupitia Mahkama ya Ardhi
kwa kazi nzuri ambayo hivi sasa wanaifanya kwani kwa mwaka uliopita kati ya
kesi 168 zilizoripotiwa karibu kesi 138 zimeshatolewa maamuzi ambapo kwa Unguja
kati ya kesi 118 zilizoripotiwa tayari 98 zimeshapatiwa hukumu na kwa Pemba
kati ya kesi 50 tayari kesi 40 zimeshapatiwa hukumu ,hapa kwa heshima kubwa Kamati
yangu inaipongeza Mahkama ya Ardhi kwa kufanya kazi zao vizuri na kile kilio
chetu Waheshimiwa Wajumbe wako wa Baraza hili tukufu kuwa kesi za Ardhi
zinachukua muda mrefu kupatiwa ufumbuzi na kuiomba Serikali kuunda Mahkama
maalum ya Ardhi ili kushughulikia kesi hizo sasa dawa imepatikana kutokana kasi
kubwa ya uendeshwaji wa kesi hizo, lakini tunawaomba pia Mahakimu wa Mahkama ya
Ardhi waendelee kufanya vizuri na kuwa waadilifu kama walivyoanza hivi sasa
isijekua ile kesi ya Mgema ukamsifu “TEMBO
“ kulitia maji. Aidha, pamoja na pongezi hizo tunawaomba Mahakimu wa
Mahkama za Ardhi kujitahidi kuwa waadilifu katika kuendesha na kutoa hukumu
hizo kwani mara nyingi kesi hizo hutawaliwa sana sana na vishawishi vya
matajiri kutaka kuweadhulumu haki zao wanyonge kupitia Mahkama hizo kwani
wanyonge hawatokuwa na uwezo wa kuhonga ili kujiokoa na kunyang’anywa ardhi zao
na mapapa ambayo yako vinywa wazi kwa gharama zozote ilimradi waweze
kuwanyang’anya haki za watu kwa kuwatumia Majaji wa Mahkama hizo. Kwa hiyo,
Mahakimu wajue kuwa wamebeba dhima kubwa kwa Mwenyeenzi Mungu kwani ardhi sio
jambo la mchezo hata kidogo ,kwani ukisikia Mataifa makubwa Duniani wanapigana
vita basi sababu kubwa ni kutaka kunyang’anya Ardhi za Nchi nyingine.
PROGRAMU NDOGO YA UPANGAJI WA MIJI NA MATUMIZI YA ARDHI.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu pia inaipongeza Idara hii ya Mipango Miji na
Vijiji kwa kuandaa upangaji upya wa Miji na Viji pamoja na matumizi bora ya
Ardhi, ili kuwawezesha wananchi wetu kuweza kufaidika na matumizi bora ya ardhi
kiuchumi na kijamii kwa maeneo yote ya Zanzibar. Pamoja na pongezi hizo Mhe.
Waziri ameeleza kwenye kitabu chake kuwa Idara ya mipango miji tayari
imeshapanga maeneo matatu ya wazi katika Eneo la Kibandamaiti, Eneo la Daraja
Bovu na Eneo la Kiembe Samaki kupitia mfuko wa (Urbarn Development Fund) tunamuomba akija kufanya majumuisho
atuelezee kuwa ni uboreshaji gani ambao unaokusudiwa kufanywa katika maeneo
hayo niliyoyataja kwani wananchi wengi hawaijui mipango hiyo ili na wao
kujitayarisha kukabiliana na changamoto zozote zitakazojitokeza wakati wa
utekelezaji wa mipango hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Pia, Mhe. Waziri katika kitabu chake ametuelezea kwamba
katika mradi mpya wa mpango mkuu wa matumizi ya Ardhi, (Zanzibar Town Master Plan)kuwa kwa hivi sasa kitovu kikuu cha Mji Mkuu
wa Zanzibar kinahama kutoka Mji Mkongwe na kuhamia maeneo ya ng’ambo bila shaka
shughuli nyingi za za kijamii, maofisi kiuchumi na kibiashara na sehemu za
mapumziko zitaongezwa na kuimarishwa katika maeneo ya ng’ambo ambapo kaulimbiu
yake ni “Ng’ambo Tuitakayo”mpango
huu kwa kweli ukifanikiwa utaiongezea haiba mji wetu wa Zanzibar kwani hivi
sasa mji upo kienyeji sana na hata majengo yake hayailetei haiba nzuri mji
wetu. Hivyo, tunaiomba Idara kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waweze
kujua mipango yenu ili na wao waweze kutoa maoni yao na pia kutoa ushirikiano
wakati wa utekalezaji wa mpango huo. PIa, Kamati yangu inaishauri Idara kuweza
kuchora ramani ya mji wetu utakavyokuwa na kuweka mabango (BILL BOARD) makubwa sehemu zenye mikusanyiko mikubwa kwenye
maeneo hayo ili wananchi kuona nikitu gani kilicholengwa kufanywa katika maeneo
hayo.
PROGRAMU NDOGO NA USIMAMIZI WA SHUGHULI ZA UJENZI NA
NYUMBA
Mheshimiwa Spika,
Programu hii kama alivyoelezea Mhe. Waziri kuwa
inatekelezwa na Idara ya Ujenzi na Shirika la Nyumba,Kamati yangu inaipongeza
Idara kwa kazi walizozifanya katika kipindi hiki ikiwemo usafishaji wa makaro
na uzibuaji wa mabomba ya maji machafu katika nyumba zetu za maendeleopamoja na
uandaaji wa michoro mbali mbali ya ujenzi usajiliwa wakandarazi mbali mbalikazi
hizi zote zinahitaji utaalamu mkubwakwa hiyo iko hajaya kuwalinda na kuwapa
maslahi bora watumishi wake ili waweze kufanya kazi zao vizuri zaidi.
PROGRAMU NDOGO YA UHIFADHI NA UENDELEZAJI WA MAMLAKA YA
MJI MKONGWE
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu pia inaipongeza Mamlaka ya Uhifadhi Mji Mkongwe
kwa kuendelea kuulea na kuuweka Mji Mkongwe kuendelea kuwa na hadhi yake kuwa
ni mji kati ya Miji Mikongwe Duniani ambayo ni urithi wa kimataifa, sisi
wazanzibari tunapaswa tuulinde na tuuhifadhi kwa pamoja mji huu kwani ni sehemu
ya kivutio kikubwa Duniani ambapo unaitangaza Zanzibar na kuweza kuwavutia
watalii wengi pamoja na wanafunzi wakiwemo watafiti mbali mbali ambao hufika
Zanzibar ili kuja kufanya shughuli zao za kitalii na kimasomo. Kwa maana hiyo,
tunawaomba sana wale wote wanaoishi na kufanya shughuli zao za kimaisha za kila
siku kuhakikisha kuwa wanatunza mazingira lakini pia kuhakikisha urithi huu
haupotezi hadhi yake, kwa hiyo tunamuomba sana Mkurugenzi aendelee kusimamia na
kuulinda mji wetu ili usije kupoteza hadhi yake kimataifa.
Mheshimiwa Spika,
Kamati inaipongeza tena Idara kwa kutafuta mradi wa
ujenzi wa ukuta wa uzio wa Bahari hapo Mizingani ambapo Kamati yangu inatarajia
kuwa baada ya kumaliza ujenzi huo basi utaweza kubadilisha haiba ya Mji wetu
ili kuongeza kuvutiaMji wetu na pia kuongeza shughuli za kibiashara na kiuchumi
ambapo tunategemea pia kutaongeza shughuli za ajira katka eneo hilo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inapongeza pia jitihada za Mamlaka ya
Uhifadhi Mji Mkongwe, kwa kufanikisha upatikanaji wa ufadhili wa ukarabati
mkubwa wa jengo la Beit-el-Ajabkupitia Serikali ya Oman. Aidha, Kamati yangu
inamuomba Mkurugenzi asichoke ili kufuatilia ukarabati huo unaanza kwa muda
uliopangwa kwani tangu nyumba hiyo ilipoporomoka jengo hilo limeikosesha
Serikali mapato mengi ambayo yalikua hupatikana kupitia ada ya jengo hilo. Pamoja
na hayo, Kamati yangu inaitaka Serikali baada ya kukamilika ukarabati huo basi
kuwe na mfuko maalum ambao utakusanya mapato ya jengo hilo ili ziweze kusaidia
kurekebisha pale patakapo leta khitlaf yoyote kwani makosa tuliyoyafanya kwa
mapato yanayokusanywa huingia katika mfuko mwengine ambapo zikihitajika
inachukua muda mwingi kupatikana kwa ajili ya kazi ilikusudiwa kufanyika.
UKARABATI WA JENGO LA CHAWA DARAJANI
Mheshimiwa Spika,
Kamati yanguinaipongeza Mamlaka kwausimamizi mzuriwa
karibu waukarabati wa jengo hilo kupitia mfuko wa Hifadhi ya jamii ZSSFkutokana na umuhimuwa shughuli za
uchumikwa wananchiwetu katika jumba hilo. Aidha, tunaziomba taasisizinazohusika
na ujenzi huo kuhakikisha ukarabati huo unaenda kwa haraka ili wale wananchi
waliokuwa wakifanya shughuli zao hapo waweze kurejea tena ili waweze kuendelea
na shughuli zao za biashara kila siku, kwani katika kipindi cha ukarabati huo
kutaleta usumbufu mkubwa kwa wao na familia zao lakini kama tunavyojua
shughuli maendeleo pia huleta changamoto
lakini inabidi tuwe wastahamilivu, pamoja na hayo tunaiomba tene Idara husika
kuhakikisha wale wadau ambao walikuwepo
mwanzo wenye maduka na wapangaji waliokuwepo mwanzo warejeshwe ili kuendelea na
biashara zao na shughuli nyengine za kijamii kama hapo mwanzo.
Vile vile, Kamati yangu inapongeza Mamlaka kwa kuanzisha utaratibu
wa kuratibu na kuyasimamia maeneo ya wazi na kuyasajili kwani katika miaka ya
hivi karibuni kumekua na utaratibu wa uvamizi wa maeneo ya wazi aidha kwa
kujengwa au kufanya shughuli neingine za kijamii na kibiashara na inapofika mtu
kuondolewa basi anakua mkali hataki kuondoka na jambo hili mwisho hupelekea
kuharibu ile haiba ya Mji mkongwe. Kamati yangu inaendelea kuiomba Mamlaka
kuhakikisha hizo sehemu za wazi zilizobakia zinaendelea kuhifadhiwa ili kuwapa
wananchi wengi kuweza kuzitumia. Pamoja na yote Mamlaka hii inafanya kazi zake vizuri na
tunampongeza sana Mkurugeni kwa Usimamizi wake imara.
Mheshimiwa Spika,
Kamati ya Mawasiliano na Ujenzi imejadili na
kuyakubali mapendekezo ya Makadirio ya
Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kwa mwaka wa
fedha 2016/2017, na inawaomba Waheshimiwa Wajumbe wako wote waijadili,
watoe mapendekezo yao na hatimae
kuipitisha Bajeti hii.
Mheshimiwa Spika,
Mwisho napenda kuwashukuru na kuwapongeza tena viongozi
na watendaji wa Wizara hii kwa juhudi wanazochukua katika kutekeleza kazi zao
pamoja na ushirikiano wao kwa Kamati hii. Aidha, nawashukuru Waheshimiwa
Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kwa kunisikiliza kwa makini na utulivu wa hali ya
juu wakati wote nilipokuwa nikiwasilisha hotuba hii.
Mheshimiwa Spika,
Naomba kuunga mkono hoja na naombakuwasilisha.
Ahsante,
……………………..,
Hamza Hassan Juma,
Mwenyekiti
Kamatiya Mawasiliano naUjenzi,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment