Habari za Punde

Hotuba ya Waziri wa Ardhi,Maji,Nishati na Mazingira BLW

HOTUBA YA WAZIRI WA ARDHI, MAJI, NISHATI NA MAZINGIRA MHESHIMIWA SALAMA ABOUD TALIB (MBM) KUHUSU
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2016/2017 KATIKA BARAZA LA WAWAKILISHI

UTANGULIZI

  1. Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako, naomba kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu sasa likae kama Kamati, ili liweze kupokea, kujadili na hatimae kuidhinisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

  1. Mheshimiwa Spika, aidha, naomba nichukuwe fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kutujaalia uzima na afya njema na kwa kuniwezesha kwa niaba ya wafanyakazi wenzangu kuwasilisha muhutasari wa hotuba ya Wizara Ardhi, maji, Nishati na Mazingira mbele ya Baraza lako.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa furaha kubwa naomba nichukue fursa hii kumpongeza kwa dhati Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dk. Ali Mohammed Shein kwa kuchaguliwa tena na Wananchi kuendelea Kuiongoza Zanzibar kwa ushindi mkubwa katika uchaguzi wa marudio uliofanyika Machi 20, 2016. Kuchaguliwa kwake kumedhihirisha kukubalika kwake kwa Wananchi kutokana na uongozi wake imara wenye busara na hekima nyingi katika kuwaletea maendeleo Wananchi wa nchi hii.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba pia nichukue nafasi hii kumpongeza Balozi Seif Ali Iddi kwa kuteuliwa tena na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar. Kuteuliwa kwako ni ushahidi wa uwajibikaji katika kutekeleza majukumu ya Serikali na kutoa mchango wako katika kuwaletea wananchi maendeleo yao katika shughuli zao za kila siku.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kukupongeza kwa dhati wewe binafsi kwa kuchaguliwa kuwa Spika wa Baraza la tisa la Wawakilishi, tunamuomba Mwenyezi Mungu akujaalie uwezo, hekima, busara na uwadilifu katika kuliongoza vyema Baraza letu hili. Vilevile, naomba kuwapongeza Wajumbe wa Baraza lako Tukufu waliochaguliwa na wananchi na walioteuliwa na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar kupitia viti maalum ili kuweza kushirikiana na Serikali katika kutatua changamoto mbali mbali zinazowakabili wananchi.

  1. Mheshimiwa Spika, Naomba pia niungane na Wafanyakazi wenzangu kutoa mkono wa pole kwa Wananchi wote walioathirika kutokana na maafa yaliotokana na mvua kubwa zilizonyesha katika visiwa vyetu. Sote tunaamini kwamba mvua ni neema lakini haya yote yametokea kutokana na kudra ya Mwenyezi Mungu Muumba Mbingu na Ardhi. Hivyo tunamuomba Mwenyezi Mungu awape subira wale wote ambao kwa namna moja au nyengine wamefikwa na maafa haya.

  1. Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu kuelezea utekelezaji wa shughuli za Wizara kwa mwaka wa fedha 2015/2016 na muelekeo kwa mwaka wa fedha 2016/2017 kama ifuatavyo:-

Mapato na Matumizi:

  1. Mheshimiwa Spika, suala la ukusanyaji wa mapato ni kiashiria muhimu sana katika kupima mafanikio ya utekelezaji. Wizara yangu katika Mwaka wa Fedha 2015/2016 ilipangiwa kukusanya jumla ya Tsh 4,799,625,000/= kutokana na vyanzo mbali mbali vya Taasisi zake. Hadi kufikia tarehe 31 Machi 2016 jumla ya Tsh 3,596,948,678/= zimekusanywa. Kiwango hichi ni sawa na asilimia 75% ya makadirio.

Kwa ufafanuzi zaidi naomba angalia kiambatanisho “A”.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi ya Mwaka wa Fedha 2015/16, Wizara yangu imepangiwa kutumia jumla ya Tsh 35,949,460,587 /=. Kati ya Fedha hizo, kazi za kawaida ni Tsh 7,198,900,000 /= na kazi za maendeleo ni Tsh 28,750,560,587 /=. Hadi kufikia tarehe 31 Machi 2016 Wizara yangu ilikwishapatiwa Tsh 3,838,441,267/= kwa kazi za Maendeleo sawa na asilimia 13.4% na Tsh 5,319,579,160/= kwa kazi za kawaida sawa na asilimia 74 %ya makadirio, hivyo kufanya jumla ya fedha zote tulizozipata kuwa ni Tsh 9,152,556,878/= sawa na asilimia 25.5% ya makisio yote.

Kwa ufafanuzi zaidi angalia kiambatanisho “B1 na B2 ”

  1. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa utekelezaji wa shughuli za Wizara, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara yangu ilifanikiwa kutekeleza majukumu yake kupitia programu kuu tano zifuatazo:

Programu 1: Mipango, Sera na Utawala wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati.
Programu 2: Usimamizi na Upangaji wa Matumizi ya Ardhi
Programu 3: Uhifadhi wa Mji Mkongwe, Uratibu na Usimamizi wa Shughuli za Ujenzi na Nyumba za Serikali
Programu 5: Usimamizi wa Huduma za Uzalishaji na Usambazaji wa Nishati na Maji.
Programu 6: Usimamizi wa Mazingira na Mabadiliko ya Tabia nchi.

PROGRAMU KUU: MIPANGO, SERA NA UTAWALA WA ARDHI, MAKAAZI, MAJI NA NISHATI

  1. Mheshimiwa Spika, Programu hii ilikuwa na jukumu la uratibu katika utekelezaji wa kazi za Wizara. Programu hii inatekelezwa na Idara Mipango, Sera na Utafiti, Idara ya Utumishi na Uendeshaji, na Afisi Kuu Pemba kupitia programu ndogo tatu ambazo ni Mipango na Sera za Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, Utawala na Maendeleo ya Rasilimali watu pamoja na programu ndogo ya Uratibu wa Shughuli za Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Pemba.

PROGRAMU NDOGO YA MIPANGO NA SERA ZA ARDHI, MAKAAZI, MAJI NA NISHATI.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 utekelezaji wa Programu hii ndogo ulilenga kutekeleza shughuli za Kuratibu/ kuandaa Mipango na Miongozo ya Kisera ya utekelezaji wa kazi za Wizara, Kuratibu, kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa programu na miradi na shughuli za Wizara pamoja na kuendeleza tafiti kwa ajili ya kuleta ufanisi katika utoaji wa huduma katika sekta za Wizara.

  1. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi wa Machi 2016 Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imefanikiwa kutekeleza mambo yafuatayo kwenye programu hii ndogo.

Kuratibu shughuli zote za Wizara ikiwemo Programu na Miradi ya Maendeleo.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Miradi ya Maendeleo, Idara imesimamia Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo kwa kufanya kazi za Uratibu, Ufuatiliaji na Tathmini ya Utekelezaji ( monitoring and Evaluation) kwa lengo la kuhakikisha kwamba miradi hiyo inatekelezwa kwa ufanisi kama ilivyopangwa. Miradi iliyosimamiwa na Idara hii ni hii ifuatayo :-

  1. Usambazaji Umeme Vijijini.
  2. Uimarishaji wa miundombinu ya Umeme na Kulijengea Uwezo Shirika.
  3. Usambazaji Maji Vijijini.
  4. Uimarishaji wa Shughuli za Maji Mijini.
  5. Kuijengea Uwezo Mamlaka ya Maji Awamu ya Pili.
  6. Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira.
  7. Utekelezaji wa Sera ya Nishati
  8. Utafiti wa Nishati Mbadala.

  1. Mheshimiwa Spika, katika uandaaji wa miongozo ya Kisera na Kisheria, Wizara imekamilisha utayarishaji wa Rasimu ya Sera na Sheria ya Mafuta na Gesi Asilia na hivi sasa ipo katika hatua za mwisho za ukamilishwaji wake. Hatua hii itaihakikishia Zanzibar kupata fursa ya uendelezaji wa shughuli za mafuta na Gesi Asilia.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Mipango na Sera za Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, jumla ya Tsh 161,884,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 101,654,949/= sawa na asilimia 63% ya Makadirio.

PROGRAMU NDOGO YA UTAWALA NA MAENDELEO YA RASILIMALI WATU

  1. Mheshimiwa Spika, Program hii ndogo inatekelezwa na Idara ya Utumishi na Uendeshaji na inajukumu la usimamizi na utawala wa rasilimali za Wizara ambapo kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 iliweza kutekeleza yafuatayo:-

  1. Kuajiri wafanyakazi 12 katika fani mbalimbali ambazo zilihitajiwa kujazwa kwa sababu tofauti ili kuongeza ufanisi wa kazi kwa kutoa huduma zenye tija kwa wananchi.

  1. Jumla ya wafanyakazi 546 wamepatiwa fursa ya kushiriki mafunzo mafupi, wafanyakazi 162 wanaendelea na mafunzo ya muda mrefu, na jumla ya wafanyakazi 41 wamemaliza mafunzo ya muda mrefu.

  1. Iliratibu shughuli za kustaafisha Wafanyakazi na kuwatayarishia mafao yao ambapo jumla ya wafanyakazi 45 walistaafu na kuratibiwa mafao yao.

Kwa ufafanuzi zaidi wa uendelezaji wa mafunzo Viambatanisho C na D vinahusika.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Utawala na Maendeleo ya Rasilimali watu jumla ya Tsh 804,252,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 570,016,314/= sawa na asilimia 71% ya makadirio

PROGRAMU NDOGO YA URATIBU WA SHUGHULI ZA ARDHI, MAKAAZI, MAJI NA NISHATI PEMBA.

  1. Mheshimiwa Spika, Program hii ndogo inatekelezwa na Afisi Kuu Pemba na ina jukumu la uratibu na usimamizi thabiti wa kazi za Wizara ikiwemo Programu na Miradi ya Maendeleo kwa Pemba ambapo kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 iliweza kutekeleza yafuatayo:-

  1. Kufanya utambuzi wa maeneo (parcels) 4,939 katika maeneyo ya Kiungoni, Limbani, Selemu na Kipangani kwa Wilaya ya Wete. Wara, Msingini na Mkoroshoni kwa Wilaya ya Chake Chake. Chokocho, Uweleni na Ng’ombeni kwa Wilaya ya Mkoani pamoja na Kusajili jumla ya maeneo (parsels) 544 yaliyofanyiwa utambuzi. Vile vile taratibu za kuwapatia kadi za usajili wa ardhi wananchi 236 ambao wameomba kupatiwa kadi hizo tayari zimeanza.

  1. Jumla ya Hati Miliki za matumizi ya ardhi 58 zimetayarishwa kati ya hizo hati za muda (provisional) ni 34 na hati za kudumu ni 24.


  1. Kukamilishwa kwa kazi ya uthamini wa Nyumba zilizoathirika katika ujenzi wa barabara ya Ole/ Kengeja na uthamini wa mimea katika barabara ya Bahanasa /Mtambwe. Vile vile kazi za uthamini wa maombi 138 ya uhaulishaji wa ardhi zimefanywa.

  1. Jumla ya viwanja 324 vimepimwa kwa ajili ya shughuli mbali mbali kama vile makaazi, biashara, taasisi, vitega uchumi mashamba na mengineo.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya uratibu wa Shughuli za Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Pemba jumla ya Tsh 1,018,229,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 624,347,150/= sawa na asilimia 61% ya makadirio.

PROGRAMU KUU: USIMAMIZI NA UPANGAJI WA MATUMIZI YA ARDHI


  1. Mheshimiwa Spika, Kufuatia kuundwa kwa Kamisheni ya Ardhi, jukumu la programu hii limeanza kutekelezwa chini ya chombo hili kipya chini ya usimamizi wa Katibu Mtendaji. Chombo hiki ndio chenye dhamana ya Utawala na Usimamizi wa Ardhi hapa nchini. Jukumu la program hii ni kuhakikisha kunakuwepo na usalama wa matumizi ya Ardhi kwa maendeleo ya nchi (Security of tenure) pamoja na kujenga matarajio ya kuwa na matumizi ya Ardhi yaliobora na fanisi lilipangiwa kutekelezwa na Idara ya Ardhi, Afisi ya Usajili wa Ardhi, Idara ya Upimaji na Ramani na Idara ya Mipango Miji na Vijiji, ambazo zote hizo zimo ndani ya Sheria ya Muundo wa Kamisheni.

Mbali na taasisi hizo Mahakama ya Ardhi nayo inahusika katika utekelezaji wa programu hii. Utekelezaji wa programu hii umegawanyika katika programu ndogo mbili ambazo ni Utawala wa Ardhi na Upangaji Miji na Matumizi ya Ardhi.

PROGRAMU NDOGO YA UTAWALA WA ARDHI


  1. Mheshimiwa Spika, Program hii ndogo inatekelezwa na Idara ya Ardhi na Usajili, Idara ya Upimaji na Ramani pamoja na Afisi ya Msajili wa Ardhi ambapo kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 programu hii ndogo iliweza kutekeleza Huduma za Ugawaji na Usimamiaji wa Ardhi, Uthamini wa Ardhi, Usajili wa Ardhi pamoja na utatuzi wa migogoro ya Ardhi kwa kutekeleza shughuli za msingi zinazohusiana nazo.

  1. Mheshimiwa Spika, Kuhusu utayarishaji wa Hati Miliki jumla ya Hati 362 zilitayarishwa kati ya Hati 650 zilizolengwa kutayarishwa. Hii ni sawa na asilimia 55.69 ya lengo lilowekwa. Kati ya hizo Hati 131 ni za Muda na Hati 231 ni za kudumu. Kuhusu Utayarishaji wa Mikataba ya Ukodishaji Ardhi, jumla ya Mikataba 58 ya Ukodishwaji Ardhi ilitatayarishwa kati ya mikataba 60 iliyopangwa. Hii ni sawa na asilimia 96 ya lengo lilowekwa.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa shughuli za Uthamini wa Ardhi jumla ya kazi za utiaji thamani 200 kwa mali zisizohamishika zilipangwa kutekelezwa ambapo hadi kufikia Machi Mwaka 2016 kazi 121 zilitekelezwa ikiwa ni asilimia 60.5% ya lengo la mwaka. Kazi hizo ni pamoja na kazi 116 za uthamini kwa ajili ya mirathi, 1 kwa ajili ya uthamini wa fidia, na 4 kwa ajili ya uthamini wa kujua soko la sasa (yaani market determination).

  1. Mheshimiwa Spika, Shughuli ya Utambuzi wa Kumjua Mwenye Haki ya Matumizi Ardhi ni utangulizi wa zoezi la usajili wa ardhi na haikuainishwa katika malengo ya Wizara ya mwaka 2015/16 lakini ilitekelezwa kwa mashirikiano ya bajeti ya washirika wa maendeleo Finland chini ya mradi wa SMOLE na pia Mradi wa Urasimishaji Mali na Biashara (MKURABITA) unaotekelezwa kwa pamoja baina ya SMZ na SMT. Jumla ya maeneo 1,207 vilifanyiwa utambuzi kati ya hayo maeneo 300 ni katika Shehia ya Chwaka na maeneo 907 yalifanyiwa katika Shehia ya Jang’ombe.

  1. Mheshimiwa Spika, Idara ya Upimaji na Ramani kwa mwaka wa fedha 2015/2016 hadi Machi, 2016, katika kutekeleza programu ndogo ya Utawala wa Ardhi imetekeleza yafuatayo:
Usimamiaji wa Shughuli za Upimaji.

  1. Mheshimiwa Spika, Idara ya Upimaji na Ramani, Katika mwaka wa fedha 2015/16 imeweza kupima jumla ya viwanja 506, kwa matumizi mbalimbali, kama inavyoonekana katika jaduweli iliyopo chini.

Jaduweli Namba 1 : Maeneo Yaliyopimwa
Nam
Matumizi
Idadi ya Viwanja
1
Makaazi
202
2
Hudma mbalimbali
41
3
Vitega Uchumi
46
4
Taasisi
15
5
Mashamaba ya Kilimo (Watu binafsi)
202
JUMLA
506
Chanzo: Idara ya Upimaji na Ramani

Idara pia imeweza kuweka Mipaka ya Wilaya ya Unguja na Pemba, kwa kusirikiana Uongozi wa Mikoa na Wilaya husika. Kazi iliyofanywa inakadiriwa kufikia Asilimia 32% ya mipaka yote.

Aidha Idara imeanza zoezi la kuzingiza kumbukumbu za Alama za Upimaji (Control Points) katika database maalumu ili ziweze kupatikana na kutumika kwa urahisi katika kazi mbalimbali za Upimaji na Ukushanyaji taarifa za Kijografia. Kazi hii nayo imeweza kufanikishwa kwa asilimia 20%.

Utayarishaji na utowaji wa Ramani Msingi.

  1. Mheshimiwa Spika, Idara Katika utayarishaji na utowaji wa Ramani Msingi. Idara imeweza kuchapisha ramani msingi (Topographical Base Map)100 za Zanzibar za kipimo cha (1:10,000) na ramani picha (Othorphotographs) 31. Aidha katika kufuatilia taarifa za kupwa na kujaa kwa maji ya bahari, kutoka chombo kilichopo Malindi (Tide Gaudge) Idara imeweza kukushanya taarifa za utabiri wa mwaka mzima.

Ukushanyaji na uwekaji wa taarifa za Ardhi

  1. Mheshimiwa Spika, Idara ya Upimaji na Ramani kwa kushirikiana na Idara za sekta ya Ardhi zilizopo, ambazo sasa ziko chini ya Kamisheni ya Ardhi, imeimarisha Mfumo wa ukusanyaji wa taarifa za ardhi (Zanzibar Land Information System (ZALIS) kwa kiwango cha asilimia 25%. Kwa ushirikishaji wa wadau wengine. Aidha jitihada za awali zimeanza kuchukuliwa kwa kuwaeleimsha wadau husika wa matumizi ya mfumo huo wa ZALIS.

AFISI YA MRAJIS WA ARDHI

  1. Mheshimiwa Spika, Afisi ya Mrajis wa Ardhi ni Taasisi yenye jukumu la kusajili ardhi yote ya Zanzibar kwa kuweka taarifa za wamiliki wa haki ya matumizi ya ardhi. Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Afisi ya Mrajis imeweza kutekeleza program ndogo ya Utawala wa Ardhi kwa kutoa huduma ya kusajili ardhi na utowaji wa kadi za usajili, kama ifuatvyo:

Usajili wa Ardhi

  1. Mheshimiwa Spika, katika kazi za usajili jumla ya maeneo 300 yalisajiliwa kwa upande wa Unguja, baadhi ya Shehia za Wilaya za Mjini na Magharibi ndizo zilizokwisha sajiliwa, na jumla ya maeneo 109 yamesajiliwa kwa shehia ya Mkoroshoni na Limbani za huko Pemba.
  1. .Mheshimiwa Spika, kwa upande wa huduma ya Utolewaji wa kadi za usajili wa ardhi, hadi Machi Jumla ya Kadi za usajili wa ardhi 410 zimetolewa kwa wananchi ambao ardhi zao zimeshasajiliwa kwa Unguja. Kwa Pemba wananchi 236 wanategemewa kutengenezewa kadi zao kwa kipindi cha miezi mitatu kijacho.

  1. Mheshimiwa Spika, Afisi ya Mrajisi katika kufanikisha huduma ya usajili pia imefanikiwa kuanzisha mfumo wa elektroniki katika usajili wa ardhi ambao utafanyakazi kwa karibu na sekta nzima ya Ardhi. Hatua za matayarisho ya kutumia mfumo wa elektroniki katika uhifadhi wa data za usajili wa ardhi zinaendelea. Kwa sasa viwanja 3000 taarifa zake tayari zimeshaingizwa katika mfumo wa electroniki.

  1. Mheshimiwa Spika, Katika utowaji wa huduma ya Usajili wa Ardhi Afisi ya Mrajisi inawajibu wa kufanyakazi kwa karibu na Afisi ya Usajili Wa Ardhi Za Mirathi. Katika mwaka 2015/16 hadi Machi,2016, Jumla ya nyumba za mirathi 934 kati ya 1415 kwa Wilaya za Mjini na Magharibi, 266 Nungwi, 62 kati ya 114 Chwaka tayari zimeshafunguliwa majalada ya mirathi Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana.

  1. Mheshimiwa Spika, Katika kufanikisha suala zima la Usajili wa Ardhi, Afisi inafahamu umuhimu wa kutoa eleimu kwa ngazi tofauti, katika mwaka tunaomaliza Afisi iliweza Kutoa elimu ya usajili kwa Wananchi kwa kufanya mikutano mitatu (3) ya kuelimisha wananchi kuhusiana na usajili wa ardhi. Mikutano hiyo imefanyika katika Shehia ya Jang’ombe, Mji Mkongwe na Shehia ya Chwaka. Aidha, mikutano hiyo pia ilitumika kutoa elimu ya mirathi kwa wananchi kwa kushirikiana na Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana.

MAHAKAMA YA ARDHI

  1. Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Ardhi inaendelea na kazi zake za kupokea, kusikiliza na kuamua kesi za migogoro ya ardhi zinazowasilishwa na wananchi pamoja na taasisi mbali mbali. Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Mahakama ya Ardhi imepokea kesi mpya 168 ambazo zimefunguliwa Unguja na Pemba pamoja na kesi za awali. Mahakama imeendesha vikao 12,283 vya kusikiliza kesi ambapo kesi 138 zimetolewa hukumu kwa mchanganuo ufuatao:-

Unguja: Kesi mpya 118 zimepokelewa na kesi 96 zimetolewa maamuzi.

Pemba: Kesi mpya 50 zimepokelewa na kesi 40 zimetolewa maamuzi.


  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Utawala wa Ardhi jumla ya Tsh 1,011,941,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 728,607,314/= sawa na asilimia 72% ya makadirio

PROGRAMU NDOGO YA UPANGAJI WA MIJI NA MATUMIZI YA ARDHI

  1. Mheshimiwa Spika, Program hii ndogo inatekelezwa na Idara ya Mipango Miji na Vijiji, ambapo katika kutekeleza programu hii ndogo kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 Idara hii ililenga kutowa huduma zifuatazo:

Kupanga Matumizi bora ya ardhi kwa miji yote ya Zanzibar
Kusimamia maendeleo ya ardhi mijini, mikoani na maeneo ya fukwe
Kuimarisha miji ili kukuza uchumi na kuleta maisha bora


  1. Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2015/2016, Idara kupitia programu hii ndogo imeweza kutekeleza malengo yake kama ifuatavyo:

Kupanga matumizi bora ya Ardhi kwa Miji yote ya Zanzibar


  1. Mheshimiwa Spika, Katika kutekelza lengo hili Idara imeweza kutekeleza yafuatayo:


  1. Kuelimisha jamii kuhusu malengo ya Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Ardhi Zanzibar (National Spatial Development Strategy - NSDS). Jumla ya semina tatu (3), zilizowashirikisha wadau mbali mbali zilifanywa. Serikali ilipitisha rasmi Mkakati wa Maendeleo ya Ardhi Zanzibar (NSDS), mnamo tarehe 4 Machi 2015.


  1. Kupanga matumizi ya ardhi ya miji midogo miwili, mmoja Pemba na mmoja Unguja ili kuongeza huduma katika mikoa yote ya Zanzibar na kuhakikisha kuwa wananchi wote wa Zanzibar wanakuwa karibu na miji midogo na wanapata huduma zao zote katika miji hiyo. Idara ya Mipango Miji na Vijiji tayari imeshapanga mipango midogo (Local Area Plan) ya miji mitatu hadi sasa. Miji hiyo ni Chwaka, Mkokotoni na Nungwi.
  1. .Idara ya Mipango Miji na vijiji tayari imeshayapanga maeneo matatu ya wazi. Eneo la Kibanda maiti, eneo la Daraja bovu na eneo la Kiembe samaki. Hivi sasa Idara inafanya jitihada kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Mji (Urban Development Fund) kuyajenga maeneo hayo. Lengo la Serikali ni kuhakiksha kuwa katika maeneo yote ya makaazi kuna maeneo ya wazi yenye hadhi kama ile ya bustani ya Forodhani.

Kusimamia Maendeleo ya Ardhi Mijini, Mikoani na maeneo ya Fukwe

  1. Mheshimiwa Spika, Katika kutekelza lengo hili Idara imeweza kutekeleza yafuatayo:

  1. Sambamba na utayarishaji wa Master Plan, Idara ilitayarisha rasimu ya sheria mpya ya mipango miji, (Planning and Developement Act), ili kuchukua nafasi ya sheria kongwe ya Mipango Miji na Vijiji (Town and Country Act, Cap 85) ya mwaka 1955.


  1. Kuelimisha jamii juu ya Sera, Sheria na kanuni mpya za Mipango Miji kwa kufanya mikutano mitatu juu ya Sera na kuweka kanuni mpya. Mnamo Agosti 2015 , kanuni mpya ya usimamizi na udhibiti ujenzi Zanzibar ilipitishwa rasmi (GN 38, 2015). Kanuni hii imeweka mfumo mpya wa utoaji vibali ambao unasimamiwa na taasisi saba, ikiwemo Manispaa, Halmashauri, Wilaya ya Magharibi B, Mamalaka ya Mji Mkongwe, Bodi ya wataalam wa ujenzi, na Jumuiya ya Wafanya Biashara Zanzibar.
Kuimarisha Miji ili kukuza uchumi na kuleta maisha bora

  1. Mheshimiwa Spika, Katika kutekelza lengo hili Idara imeweza kutekeleza yafuatayo:


  1. Mnamo tarehe 4 Machi 2015, Serikali ilipitisha Mpango Mkuu wa Matumizi ya Ardhi ya Jiji la Zanzibar (Zanzibar City Master Plan). Kwa mujibu wa mpango huu, kitovu cha Mji wa Zanzibar kinahama kutoka eneo la Mji Mkogwe na kuja eneo la Ng’ambo. Kwa maana nyengine maeneo mapya ya shughuli mbali mbali za kijamii, kibiashara na kiuchumia kama vile maofisi, maduka, sehemu za huduma na sehemu za mapumziko zitaongezwa na kuimarishwa katika eneo la Ng’ambo.

Idara kwa msaada wa Serikali ya Holand, kupitia Manispaa ya Mji wa Amsterdam, ilifanya mpango mdogo (Local Area Plan) wa eneo la Ngambo: ”Ng’ambo Tuitakayo”. Mpango huu umefanywa kwa mashirikiano na taasisi za Serikali, za kiraia na wananchi kwa ujuma. Aidha, idara imefanya mikutano na wakaazi na masheha wa Shehia zote 15 ambazo zimo katika eneo la kitovu cha mji, ambazo ni shehia ya Mchangani, Vikokotoni, Mwembetanga, Kikwajuni juu, Kikwajuni Bondeni, Rahaleo, Gulioni.

  1. Kuimarisha kitengo cha utafiti na maendeleo. Katika kipindi cha mwaka 2015/2016, Idara ilipokea jumla ya wanafunzi 40 kutoka nchi mbali mbali kama vile Sweden, Holand, Ufaransa, Finland na Uengereza. Wanafunzi hao walikuja Zanzibar kufanya tafiti mbali mbali zinazohusiana na Mipango Miji na Vijiji kwa kushirikiana na wafanyakazi wetu na hivyo kutoa fursa ya kubadilishana uzoefu na upeo. Aidha, Idara yenyewe imefanya tafiti tano (5) muhimu zinazohusu maendeleo ya Mji wa Zanzibar, ikiwemo utafiti juu ya maendeleo ya Kitovu kipya cha biashara na huduma Ng’ambo, utafiti juu ya Mipango ya miji midogo ya Chwaka, utafiti juu ya Utumiaji wa mitandao (GIS) na utafiti juu ya uanzishwaji wa kituo kipya cha mabasi Ng’ambo.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Upangaji wa Miji na Matumizi ya Ardhi jumla ya Tsh 270,055,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 226,514,649/= sawa na asilimia 84 % ya makadirio.

PROGRAMU KUU: UHIFADHI WA MJI MKONGWE, URATIBU NA USIMAMIZI WA UJENZI NA NYUMBA ZA SERIKALI

  1. Mheshimiwa Spika, Programu hii ilikuwa na jukumu la kusimamia shughuli za ujenzi wa Nyumba na Uhifadhi wa Mji Mkongwe. Programu hii inatekelezwa na Idara ya Ujenzi, Shirika la Nyumba na Mamlaka ya Uhifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe kupitia programu ndogo mbili, ambazo ni Uratibu na Usimamizi wa Shughuli za Ujenzi na Nyumba za Serikali na Uhifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe.


PROGRAMU NDOGO YA URATIBU NA USIMAMIZI WA SHUGHULI ZA UJENZI NA NYUMBA ZA SERIKALI.

  1. Mheshimiwa Spika, Program hii ndogo inatekelezwa na Idara ya Ujenzi na Shirika la Nyumba, ambapo kiutekelezaji programu hii ndogo kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 kupitia taasisi hizi mbili zilizotajwa imeweza kutekeleza shughuli zake kama ifuatavyo :

Kuzifanyia matengenezo nyumba za maendeleo Unguja na Pemba.
  1. Mheshimiwa Spika, Shirika la Nyumba Zanzibar limeweza kutapisha/kutoa maji machafu ikiwa ni pamoja na kujenga sock-pit Mombasa na kutapisha Septic tank Michenzani na pia kubadilisha mabomba yaliyoharibika. Aidha Shirika limefanikiwa kuondoa matope yaliokuwa yakisababisha kujaa kwa makaro na kusambaa kwa maji machafu katika Nyumba za Mchina Mombasa na baadhi ya Nyumba za Michenzani.

Uimarishaji wa Mapato


  1. Mheshimiwa Spika, Shirika la Nyumba la Zanzibar kwa mwaka wa fedha 2015/2016 ilipangiwa kukusanya jumla ya Tsh. 624,000,000/=. Hadi kufikia tarehe 31 Machi 2016 Shirika limefanikiwa kukusanya jumla ya Tsh. 471,650,550/= sawa na asilimia 76% ya makadirio.

  1. Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Idara ya Ujenzi, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 imeweza kutekeleza yafuatayo:-

  1. Kuandaa michoro na makadirio ya ujenzi kwa jengo la ZRB Pemba pamoja na jengo la ZECO- Unguja

  1. Kuandaa michoro na kusimamia matengenezo ya jengo la Tume ya Sayansi liliopo Maruhubi.

  1. Kusajili wakandarasi 29 na kufikisha jumla ya 181.

  1. Kusajili miradi 97 ambao imesimamiwa na wataalamu waliosajiwa

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Uratibu na Usimamizi wa Shughuli za Ujenzi na Nyumba za Serikali jumla ya Tsh 757,854,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 564,614,059/= sawa na asilimia 75 % ya makadirio.

PROGRAMU NDOGO YA UHIFADHI NA UENDELEZAJI WA MJI MKONGWE

  1. Mheshimiwa Spika, Program hii ndogo inatekelezwa na Mamlaka ya Uhifandhi na Uendelezaji Mji Mkongwe ambapo kiutekelezaji programu hii ndogo kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 kupitia taasisi hii imeweza kutekeleza malengo yaliyokusudiwa kama ifuatavyo :
Utekelezaji wa mpango wa matumizi ya barabara
  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka imetayarisha na kuwasilisha Serikalini mpango wa matumizi ya barabara zilizomo katika eneo la Mji Mkongwe (eneo la Urithi wa Kimataifa), kwa madhumuni ya kupunguza msongamano mkubwa ulioukabili mji huu unaoletea athari kubwa kwa majengo ya kihistoria pamoja na viliyomo, unaoushushia hadhi Mji huu kama ni Urithi wa Kimataifa.

Ujenzi wa Ukuta wa Ukingo wa Bahari ya Mizingani
  1. Mheshimiwa Spika, Kazi ya ujenzi wa ukuta mpya inaendelea vizuri, ambapo kutokea upande wa bustani ya Forodhani mita 30 za ujenzi wa ukuta umekamilika, na kwa kutokea upande wa mkahawa wa Mercury kazi ya ujenzi wa msingi (foundation) wa ukuta huo imekamilika. Kinachoendelea hivi sasa ni ujenzi wa ukuta ambapo wastani wa asilimia 22 ya kazi ya ujenzi wa ukuta mpya kwa pande zote imekamilika.

Ukarabati wa Jengo la Chawl liliopo Darajani
  1. Mheshimiwa Spika, Jengo la Chawl ni miongoni mwa majengo mashuhuri (Monuments) yenye daraja la kwanza ndani ya Mji Mkongwe. Mamlaka ilikamilisha utayarishaji wa ramani za awali (Existing drawings) na za mapendekezo (Proposed drawings) pamoja na makisio ya gharama kwa ajili ya ukarabati wa jengo hilo na baadae kuwasilishwa ( ZSSF) ambao ndio waliokabidhiwa rasmi jengo hili na Serikali kwa ukarabati na kulirejesha tena kwenye matumizi ambayo yatakuwa na tija zaidi tofauti na hali ya sasa. ZSSF wameanza kuchukua hatua za awali kwa kuwatumia washauri elekezi ambao wanahitajika kufuata maelekezo ya kiutalaamu wa kiuhifadhi kutoka Mamlaka ya Mji Mkongwe.

Ukarabati wa Jengo la Beit-el-Ajaib
  1. Mheshimiwa Spika, Jengo la Beit el Ajab ni miongoni mwa majengo mashuhuri yanayotambulikana kimataifa na lenye daraja la kwanza kiuhifadhi. Mamlaka ya Mji Mkongwe imekamilisha utayarishaji wa ramani za awali (existing drawings) na za mapendekezo (proposed drawings) pamoja na makisio ya gharama kwa ukarabati na ujenzi mpya wa eneo lililoanguka wa jengo la Beit el Ajaib na kuwasilisha nchini Oman. Kilichofata ni kuletwa kwa mtaalamu kutoka Oman kwa ajili ya uhakiki wa makisio hayo, utayarishaji wa nyaraka nchini Oman na zabuni (tender documents). Kwa kushirikiana na wataalamu wa Mamlaka ya Mji Mkongwe kazi hiyo imemalizika na kuwasilishwa nchini Oman. Mamlaka tayari imepokea barua kutoka Wizara ya Urithi na Utamaduni ya Oman ambayo ndiyo iliyokuwa ikishughulikia suala hili tangu hapo awali na kwamba shughuli za ujenzi wa Beit el Ajab zinatarajiwa kuanza rasmi mapema mwezi wa Juni 2016.

Kuweka kumbukumbu za matumizi ya maeneo ya wazi.
  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka inaendelea na kazi ya kuhakiki na kuweka kumbukumbu za matumizi ya maeneo yote ya wazi yaliyomo ndani ya Mji Mkongwe ambayo baadhi yake hayakuwa na mpangilio mzuri wa matumizi ambayo yanatambulika na Mamlaka. Mamlaka imeandaa mpango wa matumizi ya maeneo hayo ambao unahusisha utoaji wa mikataba kwa watu binafsi kwa matumizi yao mbali mbali ya kijamiii na kibiashara, bila kuathiri uhifadhi na kwamba bado maeneo hayo yatakuwa milki ya Serikali. Jumla ya mikataba 10 imefungwa baina ya Mamlaka na watumiaji binafsi wa maeneo ya wazi kwa kuchangia mapato na uimirashaji wa uhifadhi ndani ya Mji Mkongwe.

Mpango wa Uwekaji wa Posta na Mabango ya Matangazo
  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka imetayarisha mpango wa uwekaji wa mabango ya matangazo na ubandikaji “advertisements and publications” (postas) kama inavyokubalika kwa miji yenye hadhi Ulimwenguni. Madhumuni ni kuondoa tatizo la kuzagaa kwa mabango ya matangazo ya aina mbali mbali katika kuta za majengo, miti na mapambo ya ndani ya Mji Mkongwe ili kusaidia kuuweka mji wetu katika hali ya usafi ambao hivi sasa kuta nyingi zimechafuliwa kwa ubandikaji ovyo wa mabango ya matangazo hayo.

Takwimu za Idadi ya Mahoteli na Maduka ya Vinyago
  1. Mheshimiwa Spika, ukaguzi uliofanywa na Mamlaka umegundua kuwepo kwa mahoteli 68 ndani ya Mji Mkongwe na maduka 94 ya biashara za vinyago hususani katika eneo la Shangani. Lengo la takwimu hizi ni kuweka mpango utakaosaidia Mamlaka kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Uhifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe jumla ya Tsh 360,047,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 306,343,500/= sawa na asilimia 85% ya makadirio.

PROGRAMU KUU: USIMAMIZI WA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI

  1. Mheshimiwa Spika, Program hii inajumuisha Programu Ndogo moja tu ambayo ni Usimamizi, Uendelezaji na Usambazaji wa Huduma za Maji na Nishati na inatekelezwa na Taasisi nne ambazo ni Mamlaka ya Maji (ZAWA), Shirika la Umeme (ZECO), Mamlaka ya Kudhibiti na Kusimamia Ubora wa Viwango vya Huduma za Maji na Nishati Nchini (ZURA) na Idara ya Nishati na Madini na ina jukumu la kusimamia Uzalishaji na Usambazaji Endelevu wa Huduma za Maji na Nishati.

MAMLAKA YA MAJI

  1. Mheshimiwa Spika, Sekta ya maji inaendelea kutoa mchango mkubwa katika ustawi wa jamii zetu Mijini na Vijijini katika kuimarisha afya za wananchi kwa matumizi ya majumbani, maendeleo ya kiuchumi katika kuendeleza Kilimo, utalii, biashara, na kubwa zaidi ni umuhimu wa maji katika utunzaji wa mazingira kwa ajili ya ustawi wa maendeleo ya Taifa letu.

Ukusanyaji wa Mapato

  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Maji Zanzibar kwa bajeti ya mwaka a fedha 2015/2016 ilipangiwa kukusanya jumla ya TShs bilioni 5.1 kutokana na mauzo ya maji na shughuli nyenginezo. Hadi kufikia Machi 2016, jumla ya TShs bilioni 1.9 zimekusanywa sawa na asilimia 42% ya makadirio ya makusanyo yote.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Sekta ya Maji kupitia Mamlaka ya Maji ilifanikiwa kutekeleza Shughuli za Programu na Miradi ya Maji sita ambayo ni Programu ya Usambazaji wa Maji Vijijini, Programu ya Uhuishaji na Upanuzi wa Shughuli za Maji Mijini, Mradi wa Kuijengea Uwezo Mamlaka ya Maji Awamu ya Pili (JICA PHASE 2), Mradi wa Kuimarisha Miundombinu ya Maji na Kuijengea Uwezo Mamlaka kifedha (ADF 12), Mradi wa uchimbaji visima wa Ras al- khaimah pamoja na Kazi za Kawaida zikiwemo Kulinda na kuhifadhi vianzio vya Maji na Kufanyia Matengenezo Miundombinu ya Maji.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa kipindi hichi cha mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara yangu iliendelea kuwapatia Maji safi na salama wananchi waishio vijijini kupitia Programu ya Usambazaji Maji Vijijini kwa kujikita zaidi na ukarabati wa miundombinu ya maji kwa ulazaji wa mabomba, ujenzi wa vibanda vya kuendeshea mitambo, ununuzi na ufungaji mita za watumiaji maji, ujenzi wa vituo vya malipo ya maji na huduma kwa wateja pamoja na ujenzi wa matangi katika maeneo mbali mbali ya Vijijini Unguja na Pemba kama inavyoonesha katika jadweli lifuatalo:


Jaduweli namba 2. Utekelezaji wa Programu ya Usambazaji Maji Vijijini

SN
KAZI ZILIZO TEKELEZWA
MAELEZO YA UTEKELEZAJI
MAENEO HUSIKA
1
Ulazaji wa mabomba
Jumla ya kilomita 17.634 zimefanyiwa kazi ambapo kilomita 10.134 kwa Unguja na 7.5 kwa Pemba kazi hii ni endelevu
Mwanguo, Mvuleni, Makunduchi, Tumbatu na Kinduni kwa Unguja. Kidundo, Mtambwe, Mtuhaliwa, Wambaa, Rui na kilindi kwa Pemba.
2
Uwekaji wa Pampu na Mota mpya
Maeneo husika yamefanyiwa kazi kutokana na na pampu na mota za awali kuungua au kuzidiwa na mahitaji ya watumiaji. Aidha kazi hii ni endelevu
Kizimkazi, Kitogani, Ukongoroni, Kisongoni, Matemwe, Jambiani Kivulini, Bwejuu na Kibele kwa Unguja.
Na kwa Pemba ni Mgagadu, Mchanga Mdogo, Shengejuu Ng’ambwa, Konde ,Kironjo A, na Michenzani.
3
Ujenzi wa Vibanda vya kuendeshea pampu
Kazi hii inatarajiwa kuendelezwa katika mwaka wa fedha ujao.
Kinduni, Makunduchi Uwandani, Kibuteni kwa Unguja. Na kwa Pemba ni Shumbavyamboni na Mahuduthi.
4
Ujenzi wa matangi ya kuhifadhia Maji
Kazi imekamilika kiasi kwa hatua za awali kwa upande wa makunduchi na imekamilika kwa maeneo yaliyobakia.
Makunduchi, Mtende, Michamvi, Upenja na Tunguu Mjonga
5
Ujenzi wa ofisi ya afisa wa maji wilaya ya kusini na huduma kwa wateja
Kazi hii inaendelea na inatarajiwa kukamilishwa ndani ya mwaka wa fedha ujao ili kurahisisha upatikanaji wa Huduma kwa Wateja hususan huduma za malipo kwa wananchi wa ukanda wa Kusini ya Unguja

Paje.
6.
Ufungaji wa Mita za watumiaji maji.
jumla ya mita 48 zimefungwa kwa upande wa unguja na mita 118 zimefungwa kwa upande wa pemba kazi hii ni endelevu
Marumbi, Matemwe na Pwani Mchangani kwa Unguja. Mgagadu,Jadida, Kizimbani, Limbani, Kipangani na Kifumbikai kwa Pemba.
Chanzo: Mamlaka ya Maji, Zanzibar




Uhuishaji na Upanuzi wa Shughuli za Maji Mijini
  1. Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara yangu kupitia Mamlaka ya Maji ilifanikisha kazi za Programu ya Uhuishaji na Upanuzi wa Shughuli za Maji Mijini kwa kuhusisha shughuli tofauti katika maeneo mbali mbali ya Mjini Unguja na Pemba kama inavyojionesha katika jaduweli ifuatayo:

Jaduweli nambari 3 : Uhuishaji na Upanuzi wa Shughuli za Maji Mijini
S/N
KAZI ZILIZOFANYIKA
UTEKELEZAJI HALISI
MAENEO HUSIKA
1.
Ufungaji wa Mita za watumiaji maji

jumla ya mita 211 zimefungwa kwa upande wa unguja na mita 477 zimefungwa kwa upande wa pemba Kazi ya ufungaji mita ni endelevu
Melinne kwa Unguja. Wawi, Tibirizi, Madungu, Uwanja wa Ndege, Limbani, Jadida, Bopwe, Uweleni, Mkoroshoni Bahanasa na kwa Pemba.
2.
Uwekaji wa Pampu na Mota Mpya
Maeneo husika yamefanyiwa kazi kutokana na na pampu na mota za awali kuungua au kuzidiwa na mahitaji ya watumiaji. Aidha kazi hii ni endelevu
Kaburi Kikombe, Kinumoshi N4, Mbweni matrekta, chumbuni,Selemu No 1, Mombosa kwa Mchina kongwe, Masumbani, Magogoni, Welezo, K/Kikombe, Mombasa afisini, na Kwa binti Amrani No 2 kwa Unguja. Na kwa Pemba ni kwa Sharif Ali namba-1,2 na 3, Darajani, Jondeni, Jamvini na Kwa Bi Mtumwa.
3.
Ulazaji wa Mabomba
Jumla ya kilomita 3.103 zimefanyiwa kazi Kazi hii ni Endelevu
Kwerekwe C, Welezo na Masingini kwa Unguja.
4.
Ununuzi wa vidhibiti umeme
Jumla ya vidhibiti umeme 15 vimenunuliwa
Chunga, M/Mchomeke,Kianga na Welezo kwa Unguja. Kwa Pemba ni kironjo Kijuki na Sizini, Mtambwe kaskazini, Kwa sharifuali na Darajani Mkoani.
5.
Upelekaji wa Umeme Vituoni
Kazi imekamilika
Kwerekwe C Unguja
6.
Ujenzi wa Matangi ya Kuhifadhia Maji
Kazi imekamilika
Chumbuni, Dole na Kianga
Chanzo: Mamlaka ya Maji, Zanzibar.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 mbali na shughuli za Programu,Wizara yangu imefanikiwa kutekeleza Miradi ya Maji kama ifuatavyo.

Mradi wa Kuijengea Uwezo Mamlaka ya Maji (Awamu ya Pili)

  1. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unaofadhiliwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo (JICA), umeendelea na kazi zinazohusu kuijengea Uwezo Mamlaka ya Maji kwa kutekeleza shughuli za Mradi huu kama inavyoonekana katika jaduweli ifuatayo.

Jaduweli nambari 4: Utekelezaji wa Kazi za Kuijengea Uwezo Mamlaka ya Maji (Awamu ya Pili)
SN
Shughuli Mahsusi Zilizotekelezwa
Utekelezaji Halisi
1.
Ununuzi na Ufungaji wa mabomba na viungio vyake katika maeneo ya Gulion hadi Makadara
Jumla ya mabomba yenye ukubwa wa inchi 2½ hadi inchi 16 yamenunuliwa na tayari kilomita 2 zimeshalazwa.
2.
Ukusanyaji na Utunzaji wa taarifa za Mamlaka ya Maji.
Kukusanya taarifa zilizoweza kutambua mivujo ya maji kuanzia mwaka 2013-2015 kupitia (Survace leakage survey) ambapo jumla ya shehia 45 za Mjini na 23 za Magharibi zimeweza kuhifadhiwa katika mfumo wa GIS.
3.
Kupanga na Kutekeleza Shughuli za Kupunguza mivujo ya Maji
kukutana kwa wiki mara moja na kujadili jinsi ya kuandaa michoro (Technical Standards) juu ya uandaaji michoro, ulazaji na matengenezo ya mabomba,
kuendelea na ulazaji wa mabomba katika eneo la Gulioni-Makadara na kuanzisha mfumo wa manifold kwa nyumba ishirini zilizofungwa mita ili ziatakazorahisisha ufungaji wa mita na matengenezo.
4.
Kuongeza viwango vya elimu na taaluma kwa wafanyakazi wa Mamlaka ambapo
Jumla ya wafanyakazi 4 wamepatiwa mafunzo nchini Japan
5.
Kuendesha Utafiti na Ukaguzi kwa Wateja kwa baadhi ya maeneo ya Mjini Magharibi ambapo
zoezi hili tayari limekamilika kwa zoni ya Saateni na lipo katika hatua za kumalizia katika zoni ya Mpendae
Chanzo: Mamlaka ya Maji, Zanzibar

Mradi wa Kuimarisha Miundombinu ya Maji na Kuijengea Uwezo Mamlaka Kifedha (ADF 12)
  1. Mheshimiwa Spika, Mradi huu umekamilisha kazi ya utiaji saini mikataba ya ujenzi wa Mradi kwa wakandarasi kutoka kampuni ya NSPT ya Tanzania kwa kazi ya Ujenzi wa vianzio vya maji na Kampuni ya SPENCON kwa kazi ya ujenzi wa miundo mbinu ya Maji ambapo tayari wakandarasi wote hao wawili wameshakabidhiwa maeneo ya mradi kwa ajili ya kuanza kazi. Kwa upande wa ujenzi wa vyoo maskulini na usafi wa mazingira ambayo ni sehemu mojawapo ya Mradi huu tayari Mshauri elekezi wa Kampuni ya Howard Humphreys Tanzania Ltd. ameshakamilisha Ripoti ya Usanifu wa Mradi na kuiwasilisha kwa hatua zinazofuata.

Aidha, kwa upande wa Kazi ya Kuijengea Uwezo Mamlaka ya Maji, Mradi umeendesha warsha ya uchambuzi wa zabuni (Tender Evaluation Workshop) kwa lengo la kuijenga uwezo kamati ya uchambuzi wa zabuni na tayari taratibu za ununuzi wa mita 6,900 za watumiaji wa maji zinaendelea.
Mradi wa Uchimbaji Visima wa Ras al- Khaimah
  1. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Machi 2016, jumla ya visima 136 vimechimbwa kati ya 150 sambamba na ujenzi wa matangi 6 ya kuhifadhia maji, ulazaji wa mabomba, na ujenzi wa miundo mbinu mengine ya maji. Kazi inayoendelea kwa sasa ni ukamilishaji wa visima 14 vilivyobakia.

  1. Mheshimiwa Spika, kama zilivyo Mamlaka nyengine, Mamlaka ya Maji Zanzibar ina wajibu wa kutekeleza Kazi zake za Kawaida kupitia vyanzo vyake vya mapato ili kutimiza dhana ya kuwa Taasisi inayojitejemea na kujiendesha kibiashara, kwa lengo la kuondokana na utegemezi wa rasilimali, hususan fedha kutoka Serikali kuu.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Mamlaka imefanikiwa kutekeleza shughuli mbali mbali zinazohusiana na matengenezo ya miundombinu ya maji kama inavyoonekana katika jaduweli ifuatayo:

Jaduweli nambari 5: Matengenezo ya Miundombinu ya Maji
S/n
Kazi zilizotekelezwa
Maeneo yaliyohusika
1.
Matengenezo ya mabomba









Migombani, Kianga, Jang’ombe, Mchangani, Bambi, Kihinani, M/Makumbi, Kijangwani, M/Mchomeke, Shaurimoyo, Lumumba, Mpendae, Kijichi, M/Kwerekwe, Nungwi, Matemwe, Welezo, Kwamtipura, Magogoni, Chunga, Mbweni, Meya, Mikunguni, Sogea, Baraza la Wawakilishi, Kilimani, Michenzani, Kilimahewa, M/Ladu, Pangawe, Michungwa Miwili, Kinuni, Migombani Ikulu, Mwanyanya, Kibweni, Kwamchina, Kombawapya, na Daraja bovu, Matemwe, kilimani, Michenzani, Migombani, Meya, Welezo, Melitano, Mkunazini, Elimu Mbadala, Kwarara, Tunguu na Kianga kwa Unguja. Na kwa upande wa Pemba ni Jamvini, Mjini Chake, Mjini Mkoani, Mjini Wete, Kinyikani, Wesha,Vitongoji Kilindi,Kisiwapanza, Mtambile, Shumba Mjini Changaweni, Makangale, Konde, Makongwe, Gando, Junguni, Kojani, Pandani ,Ole.Wambaa na Ukunjwi.
3.
Marekebisho ya Umeme
Visima vya Kiashange, Kaburi Kikombe, Mwembe Mchomeke No 51,Kibuteni, Bumbwini, Kidanzini, Kiboje, Bweleo, Manzese, Mgambo, Muyuni, Chunga No 09, Chwaka, Chaani, Dunga S.S.Metha, Chumbuni,Kibele, Bweleo, Msikiti Mzuri No 10, Msikiti Mzuri 12, Kisongoni Nungwi Kae, Matrekta, Mfenesini, Kinumoshi No 3,4,5, Machui, Welezo No 2, Mombasa Ofisini, Umbuji, Kitogani, Kianga No 7 na Salem 1 kwa Unguja. Na Sizini,Kironjo,Kijichame,Makangale,Gawani,Bunguni, Kibomani, Penjewani,Ziwani,Ngambwa,Kwapweza, Kwa Sharifuali, Chanjaani, Changaweni, Mtambile, Ngombeni, Ngwachani, Mjimbini kwa upande wa Pemba.
4.
Matengenezo ya pampu na mota zilizoungua
Visima vya Bweleo, Machui, KaburiKikombe, Bumbwini Kidanzini, Mombasa Afisini, Kieshange No 4 Kitogani, Mwanyanya, Jendele, Maungani na usafishaji wa visima (Flushing) imefanyika katika maeneo ya MigombaniPangeni, K/Kikombe,Welezo na Saateni workshop kwa Unguja. Na Pemba ni Visima vya Mfikiwa, Ukutini, Makangale,Changaweni Chake Chake, Mjimbini, Sharifuali no-3 na Wingwi Mlindo. FlUshing Kwa Pemba imefanyika Visima vya Ng’ambwa, Mauleni, Ng’wachani, Bogoa, Kijichame,Mfikiwa, Ole skuli, Mazurui, Kwamkoba, na kinowe.
Chanzo: Mamlaka ya Maji, Zanzibar
IDARA YA NISHATI NA MADINI
  1. Mheshimiwa Spika, Idara ya Nishati na Madini ni taasisi inayohusika na Usimamizi na Usambazaji wa Huduma ya Nishati hapa nchini kwa lengo la Kuimarisha Upatikanaji na Usambazaji wa Nishati yenye ufanisi, kwa bei nafuu na inayozingatia Uendelevu wa Mazingira yaliyo salama na rafiki kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii ambapo kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Idara hii ilisimamia na kutekeleza mambo yafuatayo:-

Mradi wa Utekelezaji wa Sera ya Nishati

  1. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unatekelezwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Washirika wa Maendeleo na unahusika zaidi katika maeneo makubwa mawili ambayo ni Kuijenga uwezo Sekta ya Nishati - Awamu ya Pili (Zanzibar Energy Sector Support Consolidated Phase) kwa mashirikiano na Shirika la maendeleo la Sweden (SIDA) na eneo kuu la pili ni Kuimarisha Mazingira pamoja na Kupambana na Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi ambapo baada ya kukamilika kwa maeneo haya mawili, bila shaka sekta ya Nishati kwa Zanzibar itakuwa imeimarika na kuongeza ufanisi kiutekelezaji ambayo ni hatua muhimu sana kwa mustakbali wa uchumi wetu na sekta zote kwa ujumla.


  1. Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mradi wa Kuijenga uwezo Sekta ya Nishati - Awamu ya Pili, Idara kwa kushirikiana na Ubalozi wa Sweeden tayazi imetiliana saini na Kampuni ya Multy Consultant ASA ya nchini Norway ambayo ilishinda zabuni ya ushauri Elekezi kwa mradi huu unaotarajiwa kutekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka huu wa fedha.

Aidha, Idara kwa kushirikiana na iliyokuwa Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais chini ya mradi wa mabadiliko ya Tabia nchi kwa ufadhili wa UNDAP imetekeleza yafuatayo:-

  1. Jumla ya mifumo (38) ya umeme wa jua (Solar Units) imewekwa katika maeneo mbali mbali Unguja na Pemba.

  1. Ziara za ukaguzi katika maeneo yaliyofungwa mifumo hiyo kwa kutathmini ufanisi zimefanyika.

  1. Hati ya muongozo (guidelines document) imeandaliwa sambamba na kuendesha semina ya kushajihisha matumizi ya miongozo hiyo.
  2. Kuandaa Mpango Kazi wa utekelezaji wa Será ya Nishati

  1. Kuandaa Kanuni za kupiga marufuku matumizi ya taa zenye kutumia umeme mwingi (incandescent bulbs).
  2. Kufunga taa sanifu (energy saving bulbs) katika maeneo maalum ya majaribio (pilot areas) ambayo ni Fumba na Mwakaje.

Mradi wa Utafiti wa Nishati Mbadala
  1. Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na azma yake ya kukamilisha Mradi huu wa Nishati MbadalaUnaofadhiliwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Jumuiya ya Nchi za Ulaya (EU) wenye lengo la kufanya utafiti ili kubaini uwezekano wa Zanzibar kupata umeme kwa njia mbadala.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/206, Wizara imesimamia zoezi la usafishaji maeneo pamoja na ujenzi wa minara mitano yenye urefu wa mita sabiini na moja (71 m) pamoja na kufunga vifaa vya kurikodia (sensors) kwa lengo la kukusanya taarifa za mwenendo wa upepo na nguvu za jua. Ujenzi huo umetekelezwa chini ya Kampuni ya AGMIN kutoka Italy. Vile vile Wizara imekamilisha kupatikana kwa mkandarasi (Kampuni ya MWH ya Spain) ambae atashughulikia masuala ya kisheria pamoja na kuzijengea uwezo taasisi zinazoshughulikia miradi ya Nishati Mbadala. Aidha, Mshauri elekezi (Kampuni ya Intec Gopa ya Ujerumani) anaendelea na kazi na ukusanyaji wa tarifa hizo (data collection) na tayari ameshatoa ripoti yake awali ya miezi mitatu (Oktoba-Disemba 2015) inayoonesha mwelekeo mzuri wa mwenendo wa upepo na nguvu za jua.

  1. Mheshimiwa Spika, mbali na shughuli za Maendeleo kwa mwaka wa fedha 2015/2016 imefanikiwa kutekeleza Kazi za Kawaida kama ifuatavyo:-

Kushiriki katika Mikutano ya Masuala yote yanayohusu Nishati ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa pamoja na Kuendelea kusimamia Upatikanaji wa Mafuta Zanzibar.

  1. Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza hili, Idara imefanikiwa kusiriki mikutano kadhaa iliyofanyika ndani na nje ya nchi ikiwemo vikao vya Jumuiya ya Afrika Masharikikatika masuala ya nishati ya umeme ( Dar es Salaam- Tanzania na Kigali - Rwanda). Bilashaka fursa hii inaongeza uzoefu na utaalamu kwa wafanyakazi wa Idara hii.

Aidha, katika kuhakikisha nishati ya mafuta inapatikana kwa uhakika na, Idara inaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Kusimamia na Kudhibiti nishati nchini ili kutambua mwenendo wa biashara ya mafuta pamoja na kufanya ufuatiliaji na ukaguzi kwenye vituo vyote vya makampuni yanayoendesha biashara ya mafuta hapa nchini.


Kuendeleza Mashirikiano na Wadau wa Maendeleo katika Kuendesha Mafunzo yanayohusiana na suala la Mafuta na Gesi Asilia pamoja na Kujenga Uelewa kwa Wananchi juu ya Masuala ya Nishati.


  1. Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuendeleza Mashirikiano na wadau mbali mbali wa maendeleo wa ndani na nje, Idara imefanikiwa kuendesha semina tatu zinazohusiana na masuala ya mafuta na gesi asilia ambazo zimewashirikisha wafanyakazi wa Idara ya Nishati na Madini ikiwa ni sehemu ya kuwajengea uwezo Kitaaluma. Jumla ya semina mbili, vipindi vya redio na televisheni na mikuano kadhaa imefanyika kwa lengo la kujenga uelewa kwa wananchi .

SHIRIKA LA UMEME

  1. Mheshimia Spika, Shirika la Umeme ni taasisi inayohusika na Usimamizi na Usambazaji wa Huduma ya Nishati ya Umeme hapa nchini kwa lengo la Kuimarisha Upatikanaji na Usambazaji wa Nishati hiyo kwa ufanisi, yenye uhakika na kwa bei nafuu kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa programu ya usimamizi wa huduma za Maji na Nishati. Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Taasisi hii ilisimamia na kutekeleza kazi ya Usambazaji na Uimarishaji wa Miundo Mbinu ya Umeme Mjini na Vijijini.

Mapato na Matumizi

  1. Mheshimia Menyekiti,kimsingi Shirika hili kama ilivyo kwa mashirika mengine ya umma hapa nchini sio tu yana wajibu wa kuhakikisha upatikanaji wa huduma zenye ubora unaokubalika kitaifa na kimataifa na kwa gharama nafuu kwa lengo la kuimarisha ustawi wa jamii yetu kiuchumi, kijamii na kimazingira bali pia kuliwezesha Shirika kujiendesha kibiashara na hatimaye kuweza kuchangia katika mfuko mkuu wa Serikali.


  1. Mheshimia Menyekiti, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Shirika lilikadiria kukusanya Tsh. 107,063,020,514/= kutokana na Biashara ya kuuza umeme na huduma nyenginezo zinazotolewa kwa wananchi na wafanyabiashara ikiwemo wawekezaji mbali mbali hapa nchini. Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2016 Shirika limekusanya jumla ya Tsh. 63,277,985,396/= sawa na asilimia 59.1% ya makadirio.

Kwa upande wa Matumizi, Shirika lilikadiria kutumia jumla ya Tsh. 99,838,743,939/=. Hadi kufikia tarehe 31 Machi 2016, Shirika lilikwishatumia Tsh. 67,980,810,349/= sawa na asilimia 68.1% ya makadirio kama inavyoonekana katika jaduweli lifuatalo.
Jaduweli nambari 6: Matumizi ya Shirika la Umeme kwa mwaka wa fedha 2015/2016
MAELEZO
MAKADIRIO YA MWAKA 2015-2016
MATUMIZI HALISI Julai,2015 hadi Machi, 2016.
Ununuzi wa Umeme
TANESCO
58,456,165,441.00
46,281,896,474.96
Kazi ya kawaida
26,378,880,650.00
11,699,728,964.07
Kazi ya maendeleo
15,003,697,848.00
9,999,184,910.39
Jumla
99,838,743,939.00
67,980,810,349.42
Chanzo: Shirika la Umeme, Zanzibar

  1. Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi hichi cha mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara yangu kupitia Shirika la Umeme iliendelea kuwapatia huduma za umeme wananchi waishio mijini na vijijini kupitia Programu na Miradi ya Umeme nchini kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na Washirika mbali mbali wa Maendeleo waliopo ndani na nje ya nchi kwa kujikita zaidi na ukarabati wa miundombinu ya umeme na usambazaji wa umeme Vijijini Unguja na Pemba.

Usambazaji wa Umeme Vijijini
  1. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2015/2016 Shirika limejenga kilomita 33.1 ya umeme mkubwa na kilomita 83.9 za laini ndogo ya Umeme pamoja na uwekaji wa Transfoma 35 za kusambaza umeme katika Vijiji 36 kwa Unguja na Pemba kama inavyoonekana katika jaduweli ifuatayo-:

Jadueli nambari 7: Vijiji Vilivyopatiwa Umeme
UNGUJA
PEMBA
Binguni Mtakuja
Chupwe Micheweni
Bungi Usalama
Gongomawe
Cheju Kisomanga
Kisiwa cha Makoongwe
Donge Kiongwe Kidogo
Kisiwa cha Shamiani Muambe
Hanyegwa Mchana
Kisiwa Panza
Kandwi
Kiziwani Shungi
Kijini
Konde Mipurani
Matetema
Mazoweya Pujini
Maungani Kichakapunda
Mgeni nje Shumba vyamboni
Mbuyu Tende
Michungwani
Mgambo
Mitungujani
Ndijani Nyambiza
Mjananza Wingwi
Tunguu
Mjimbini Kangani
Ubago Wilayani.
Mtimbu Pujini
Upenja Kaskazini
Muambe kwasaanani
Uzi Pwani
Mwachawa
Pujini Kibaridini
Sebudawa Micheweni
Shengejuu Mtambwe
Wawi Magome
Chanzo: Shirika la Umeme, Zanzibar
Uimarishaji wa Miundombinu ya Umeme.

  1. Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha miezi 9, Shirika limebadilisha waya chakavu kilomita 37.9, nguzo mbovu 1,319 na kupima transfoma 577 kwenye maeneo ya Mijini na Vijijini pamoja na kuzifanyia marekebisho zile zilizokuwa na matatizo ili kuhakikisha kwamba hali ya upatikanaji wa huduma bora ya Umeme inapatikana kwa uhakika na kwa wakati wote.

Ufungaji wa Mita za TUKUZA:
  1. Mheshimiwa Spika, lengo la mradi huu ni kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya Shirika na kupunguza malimbikizo ya madeni. Hadi kufikia Machi, 2016, Shirika limenunua mita 13,000 za TUKUZA kwa gharama ya Tsh.1,423,500,000/=. Kati ya hizo, Mita 6,645 zimefungwa kwa Wateja wapya na Mita 6,355 zimebadilishwa kwa wateja wa zamani wenye mita za kawaida na mbovu.



MAMLAKA YA UDHIBITI YA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI

  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Udhibiti ya Huduma za Maji na Nishati ni Taasisi yenye jukumu la kusimamia Huduma za Maji safi na Maji taka, Nishati ya umeme pamoja na Mafuta na Gesi (down stream) na kwa hiyo inalenga kutekeleza lengo kuu la Programu ya Usimamizi wa Huduma za Maji na Nishati ambalo ni Kufikia Usimamizi Endelevu na Usambazaji Toshelezi wa Huduma za Maji na Nishati kwa mujibu wa Mahitaji ya Jamii.

  1. Mheshimiwa Spika, Kwa Mwaka wa Fedha wa 2015/2016 Mamlaka ya Udhibiti ya Huduma za Maji na Nishati imefanikiwa kutekeleza mambo yafuatayo:-

Kuandaa Kanuni za Usimamiaji wa Sekta ya Mafuta kuanzia Uagiziaji, Upakuaji, Uhifadhi, Usambazaji, Uuzaji na Ujenzi wa Vituo vya Mafuta.
  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka katika kusimamia vyema majukumu ya kusimamia biashara ya mafuta nchini, imeandaa Kanuni za Kusimamia Biashara ya Mafuta (Petroleum Supply Regulations,2015) na Kanuni za Kusimamia ujenzi wa vituo vya Mafuta ili kuweka mazingira ya vituo hivyo kuwa katika viwango vinavyokubalika.

Kuanza Shughuli za utoaji wa leseni.

  1. Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza hili, Mamlaka imeanza kufanya ukaguzi wa vituo vyote vya mafuta kwa upande wa Unguja ili kujiridhisha juu ya viwango na ubora wa vituo hivyo. Hadi Machi, 2016 Mamlaka imekagua vituo 30 kati ya vituo vyote 50 vilivyopo Zanzibar na kutoa maelekezo ya kufanya matengenezo na marekebisho kwa vituo ambavyo havikidhi viwango kabla ya kuwapa leseni.


Kuanza kupanga bei za mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa.

  1. Mheshimiwa Spika, Mamlaka ilikabidhiwa rasmi jukumu la kupanga bei elekezi na Bodi ya Mapato ya Zanzibar mapema mwezi Disemba 2015. Kuanzia mwezi Februari, 2016 Mamlaka imeanza kazi ya kupanga na kutoa bei elekezi kwa bidhaa zote za mafuta hapa nchini ambapo zoezi hili linafanyika kila mwezi.

Kujenga uelewa juu ya majukumu na kazi za Mamlaka kwa wadau na Jamii kwa jumla.

  1. Mheshimiwa Spika, Kwa vile Mamlaka hii ni mpya, ni wazi kuwa wananchi wanahitaji kuijua na kuielewa Mamlaka vizuri, hivyo Mamlaka imekuwa ikifanya mikutano na Makampuni yanayoleta mafuta Zanzibar (Oil Marketing Companies), wamiliki wa vituo vya mafuta na wataalamu kutoka katika taasisi mbali mbali za Serikali na zisizo za Serikali kwa lengo la kuwaelimisha kuhusu Majukumu na Kanuni zinazosimamiwa na ZURA. Jumla ya semina Nne (4) zimefanyika kwa Unguja na Pemba. Vile vile Mamlaka imeanza kutoa vipindi vya kuelimisha jamii kwa njia ya televisheni.

Ushirikiano na Taasisi za Kikanda zinazohusiana na udhibiti wa huduma za Maji na Nishati

  1. Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa suala hili, Mamlaka imekuwa ikishirikiana kwa karibu na Taasisi za Tanzania Bara kama vile Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Taasisi inayosimamia uhifadhi wa Mafuta (TIPER), Wakala wa uagizaji wa Mafuta ya jumla Tanzania (PBPA), Kampuni ianayoweka alama katika mafuta (GFI) nk. Vile vile Mamlaka imejenga uhusiano mzuri na Taasisi inayohifadhi mafuta ya Mombasa Kenya (Kipevu Oil Jet).

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza program ya Usimamizi wa Huduma za Nishati na Maji jumla ya Tsh 31,565,198,587/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 6,030,458,943 /= sawa na asilimia 19% ya makadirio.

PROGRAMU KUU: USIMAMIZI WA MAZINGIRA/MABADILIKO YA TABIANCHI

  1. Mheshimiwa Spika; Itakumbukwa kwamba kufuatia uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016 Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imefanya mabadiliko ya miundo ya Mawizara zake iliyopelekea kuundwa kwa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira, hivyo programu hii ya usimamizi wa Mazingira/mabadiliko ya tabianchi hapo awali ilikua chini ya usimamizi wa Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais na hivi sasa inasimamiwa na Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira.

  1. Mheshimiwa Spika, Kama tunavyofahamu kwamba suala la mazingira linachukua nafasi kubwa na ya pekee wakati wa kujadili suala la Mabadiliko ya Tabianchi. Kwa mantiki hiyo ni kweli kwamba suala la mazingira linapaswa kupewa kipaumbele wakati wa kujadili dhana nzima ya Mabadiliko ya Tabianchi huku tukilenga kuyafikia maendeleo endelevu ya kiuchumi.kiteknolojia na kijamii bila ya kuathiri mazingira yaliyotuzunguka katika maisha yetu ya kila siku.

  1. Mheshimiwa Spika, Idara ya Mazingira na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira (ZEMA) kwa mwaka wa fedha 2015/2016 kupitia programu ndogo mbili ambazo ni Usimamizi wa Mazingira na Usimamizi wa Mabadiliko ya tabianchi kwa pamoja zilipanga na kutekeleza majukumu kama ifuatavyo:

Programu ndogo ya Usimamizi wa Mazingira

  1. Mheshimiwa Spika, Programu hii ndogo inatekelezwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira na Idara ya Mazingira ambapo kwa mwaka wa fedha 2015/2016 imefanikiwa kutekeleza mambo yafuatayo:-

Kutayarisha Kanuni za Usimamizi wa Mazingira.

  1. Mheshimiwa Spika, rasimu za awali za mapitio ya Kanuni ya Tathmini ya Athari za Kimazingira ya mwaka 2002 na Kanuni ya Marufuku ya Mifuko ya Plastiki ya mwaka 2011 zimetayarishwa kwa kuondosha mapungufu yaliyokuwepo na kuingiza hoja muhimu za wadau.

Kuendesha Operesheni 84 za mifuko ya plastiki na pia 84 kwa maliasili zisizorejesheka.


  1. Mheshimiwa Spika, jumla ya operesheni 16 za mifuko ya plastiki zimefanyika kwa Unguja na Pemba ambapo zaidi ya kesi 17 zimefikishwa mahakama husika na kutolewa hukumu.

Kufanya ufuatiliaji wa kimazingira kwenye maeneo 84 yaliyoharibiwa kimazingira.

  1. Mheshimiwa Spika, jumla ya maeneo 35 yenye uharibifu na uchafuzi wa mazingira yametembelewa na kutolewa muongozo wa kimazingira na kisheria. Kati ya maeneo hayo 23 yapo Unguja na 12 yapo Pemba. Kwa ufafanuzi zaidi angalia Kiambatanisho E.

Kufanya shughuli za Ufuatiliaji, Tathmini na Ukaguzi wa kimazingira kwa miradi ya Uwekezaji iliopo hapa nchini.


  1. Mheshimiwa Spika, jumla ya miradi 45 imefanyiwa ufuatiliaji na kutolewa muongozo wa kimazingira na kisheria. Kati ya miradi hiyo 30 Unguja na 15 Pemba Miongozo hiyo ilikuwa inahusisha usimamizi wa taka na maji machafu hasa kutoka kwenye mabwawa ya kuogelea. Vilevile jumla ya miradi 25 imefanyiwa Tathmini za Kimazingira na kupewa vyeti vya kimazingira. Aidha jumla ya miradi 18 imefanyiwa ukaguzi wa kimazingira na kupewa vyeti vya ukaguzi huo. Kwa ufafanuzi zaidi angalia Viambatanisho F na G.

Kuelimisha jamii juu ya Sheria ya Mazingira kupitia vipindi vya Radio, TV na mikutano ya uhamasishaji.


  1. Mheshimiwa Spika, jumla ya vipindi 25 (18 Radio na 7 TV) vya kuelimisha jamii juu ya usimamizi wa mazingira vimetayarishwa na kurushwa kupitia ZBC Radio, ZBC TV, Coconut, Hits FM Chuchu FM. Aidha, ZEMA na Idara ya Mazingira zilitembelea Wizara zote pamoja na Ofisi za Mikoa kuonana na watendaji wakuu wa taasisi hizo pamoja na taasisi zilizo chini ya Wizara hizo kwa lengo la kuelimisha wadau juu ya Sheria ya Mazingira ya mwaka 2015.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu zake, Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira na Idara ya Mazingira ziliidhinishiwa kutumia Tsh 255,000,000/=. Hadi kufikia Machi, 2016 taasisi hizi zilikwisha ingiziwa Tsh 38,375,000/= sawa na asilimia 15%.

Programu ndogo ya Mabadiliko ya Tabianchi
  1. Mheshimiwa Spika, Programu hii ndogo inatekelezwa na Idara ya Mazingira, Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kupitia Idara ya Misitu na Maliasili zisizorejesheka, Wizara Fedha na Mipango kupitia Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kupitia Idara ya Nishati na Madini na Jumuiya ya Maendeleo ya Jamii na Uhifadhi wa Mazingira Zanzibar (Community Development and Environmental Conservation in Zanzibar - CODECOZ).
  1. Mheshimiwa Spika, Mpango kazi wa utekelezaji wa Mkakati wa Mabadiliko ya Tabianchi umetayarishwa kutokana na vipaumbele vilivyoainishwa kwenye Mkakati wa Mabadiliko ya Tabianchi wa Zanzibar wa mwaka 2014. Mpango kazi huo unategemewa kuzinduliwa rasmi mwezi wa Juni, 2016 kwa ajili ya utekelezaji.

  1. Mheshimiwa Spika, Mpango wa Kijamii wa Kuhimili Athari za Mabadiliko ya Tabianchi (Local Adaptation Plan of Action - LAPA) kwa Wilaya 3 (Micheweni, Kaskazini “A” na Kusini Unguja) umetayarishwa. Mpango huu unakusudiwa kutumika katika kuhamasisha nyezo za utekelezaji za Mpango huo na hatimae kutayarisha mipango ya Wilaya nyengine zilizobakia hatua kwa hatua kutegemea na upatikaaji wa fedha. Aidha, katika suala la kuendelezwa baadhi ya maeneo yaliyoathiriwa na mabadiliko ya tabianchi, jumla ya hekta 100 za mikoko/mikandaa imepandwa kwenye maeneo 17 ya Unguja (10) na Pemba (7) kwa ajili ya kuendeleza maeneo yaliyoharibiwa.

  1. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Katika kutekeleza programu ndogo ya Mabadiliko ya Tabianchi, jumla ya Tsh 450,000,000/= ziliidhinishwa kutumika. Hadi kufikia Machi, 2016, fedha zilizoingizwa ni Tsh 459,345,000/= sawa na asilimia 102%.

MUELEKEO KWA MWAKA WA FEDHA 2016/2017
  1. Mheshimiwa Spika, kwa heshima naomba kuwasilisha muelekeo wa Bajeti yenye kuzingatia programu ya Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira ina jumla ya Programu Kuu nne ambazo ni;
  1. Programu 1: Mipango, Sera na Utawala wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira
  2. Programu 2: Usimamizi na Upangaji wa Matumizi ya Ardhi
  3. Programu 5: Usimamizi wa Huduma za Maji na Nishati
  4. Programu 6: Usimamizi wa Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi.


  1. Mheshimiwa Spika, jumla ya Tsh Bilioni 57,456,186,000 zinatarajiwa kutumika katika utekelezaji wa Programu hizi nne.

  1. Mheshimiwa Spika, Naomba sasa uniruhusu kutoa maelezo kwa ufupi kuhusu Programu na Programu ndogo zinazohusiana na Wizara yangu kama ifuatavyo.

PROGRAMU YA MIPANGO, SERA NA UTAWALA WA ARDHI, MAJI, NISHATI NA MAZINGIRA

  1. Mheshimiwa Spika, programu hii inajukumu la kuimarisha uratibu katika utekelezaji wa Kazi za Wizara ambapo matokeo ya muda mrefu yanayotarajiwa ni Kukuza ufanisi katika utawala wa rasilimali ardhi pamoja na utoaji huduma za kijamii. Programu itasimamiwa na Idara ya Utumishi na Uendeshaji, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti na Afisi Kuu Pemba ambapo jumla ya Tsh. 2,342,446,000/= zinatarajiwa kutumika kwa utekelezaji wake. Programu hii imegawanyika katika Programu ndogondogo kama ifuatavyo:-

Mipango na Sera za Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira/Mabadiliko ya Tabianchi


  1. Mheshimiwa Spika, dhumuni la Programu ndogo hii ni Uratibu wa Shughuli na Kazi za Wizara kwa Ufanisi, ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa Programu hii ni Kuratibu/Kuandaa Mipango na Miongozo ya Kisera ya Utekelezaji wa Kazi za Wizara, Kuratibu, Kufuatilia na Kutathmini Utekelezaji wa Programu, Miradi na shughuli za Wizara na Kuandaa Tafiti kwa ajili ya Kuendeleza ufanisi katika utoaji wa huduma katika sekta za Wizara. Jumla ya Tsh 173,067,000/= zinatarajiwa kutumika.

Utawala na Maendeleo ya Rasilimali watu

  1. Mheshimiwa Spika, dhumuni la programu ndogo hii ni kuhakikisha usimamizi thabiti na utawala wa rasilimali za Wizara, ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa programu hii ni Kukuza Viwango vya Wafanyakazi na kuhifadhi kumbukumbu na Taarifa za Wafanyakazi wa Wizara. Jumla ya Tsh 808,112,000/= zinatarajiwa kutumika.

Uratibu wa Shughuli za Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Pemba


  1. Mheshimiwa Spika, dhumuni la programu ndogo hii ni Uratibu na Usimamizi Thabiti wa Kazi za Wizara kwa pemba, ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa programu hii ni Kuratibu Shughuli za Mipango na Utawala pamoja na Kuratibu na Kusimamia masuala ya Ardhi, Makaazi maji na Nishati Pemba. Jumla ya Tsh 1,361,267,000/= zinatarajiwa kutumika.

PROGRAMU YA USIMAMIZI NA UPANGAJI WA MATUMIZI YA ARDHI


  1. Mheshimiwa Spika, programu hii inajukumu la kuhakikisha kunakuwepo na usalama wa matumizi ya ardhi kwa maendeleo ya nchi (security of land tenure). Matokeo ya muda mrefu yanayotarijiwa ni kuwa na matumizi ya ardhi yaliyobora na fanisi. Programu hii inasimamiwa na Kamisheni ya Ardhi na Mahakama ya Ardhi ambapo jumla ya Tsh. 2,275,072,000/= zinatarajiwa kutumika.

  1. Mheshimiwa Spika, programu hii imegawanyika katika Programu ndogo ndogo kama ifuatavyo:

Utawala wa Ardhi

  1. Mheshimiwa Spika, Dhumuni la Programu ndogo hii ni kuhakikisha Usalama wa Umiliki wa Ardhi kwa Wananchi ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa Programu hii ni ugawaji na usimamiaji wa ardhi kwa matumizi mbali mbali, Uthamini wa ardhi na Usimamiaji wa shughuli za Upimaji na Ramani, Usajili wa ardhi. Jumla ya Tsh 1,065,460,000/= zinatarajiwa kutumika.


Upangaji wa Miji na Matumizi ya Ardhi

  1. Mheshimiwa Spika, dhumuni la programu ndogo hii ni Kuhakiksha Kunakuwepo Uwiano wa matumizi ya Ardhi kati ya Matumizi ya Uchumi na Kijamii, ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa programu hii ni kuwepo kwa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi kwa Miji yote ya Zanzibar, Kusimamia Maendeleo ya Ardhi Mijini, Mikoani na maeneo ya Fukwe, Kuimarika kwa Miji ili Kukuza Uchumi na Kuleta Maisha Bora. Jumla ya Tsh 1,021,398,000/= zinatarajiwa kutumika.

Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi

  1. Mheshimiwa Spika, Dhumuni la Programu ndogo hii ni kuhakikisha kwamba kunakuwepo na utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa haraka zaidi kadri ya inavyojitokeza, ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji programu hii ndogo ni pamoja na kupungua kwa migogoro ya Ardhi. Jumla ya Tsh 188,214,000/= zinatarajiwa kutumika.


PROGRAMU YA USIMAMIZI WA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI

  1. Mheshimiwa Spika, jukumu la programu hii ni kuhakikisha kunakuwepo upatikanaji wa Huduma za Nishati na Maji inayotosheleza mahitaji ya Watu. Matokeo ya muda mrefu yanayotarajiwa ni upatikanaji wa huduma bora za Nishati, Umeme na Maji kwa wananchi.

  1. Mheshimiwa Spika, Programu hii itasimamiwa na Idara ya Nishati na Madini, Mamlaka ya Kudhibiti Huduma za Maji na Nishati, Shirika la Umeme na Mamlaka ya Maji ambapo jumla ya Tsh. 48,978,195,000/= zinatarajiwa kutumika katika utekelezaji wake.

  1. Mheshimiwa Spika, matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa programu hii ni usimamizi wa usambazaji wa mafuta nchini, usambazaji wa huduma za Umeme, uhifadhi wa maeneo ya vianzio vya maji, upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa watumiaji mijini na vijijini.

PROGRAMU YA USIMAMIZI WA MAZINGIRA NA MABADILIKO YA TABIANCHI

  1. Mheshimiwa Spika, proramu hii itatekelezwa kupitia programu ndogo ya Usimamizi wa Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi na utekelezaji wake utaimarisha usimamizi wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi. Programu hii inasimamiwa na Idara ya Mazingira na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira.

  1. Mheshimiwa Spika, dhumuni la programu hii ni kuhakikisha usimamizi thabiti wa masuala ya kimazingira , ambapo matokeo ya muda mfupi (output) yanayotarajiwa katika utekelezaji wa programu hii ni Kudhibiti athari za kimazingira kwa kuyaendeleza maeneo yaliyoathirika na mabadiliko ya tabianchi, kuendeleza tathmini za kimazingira pamoja na miongozo ya uimarishaji wake. Jumla ya Tsh 3,860,473,000/= zinatarajiwa kutumika katika utekelezaji wa programu hii.

  1. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Programu hii ndogo ya Usimamizi wa Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi unajumuisha Mamlaka ya Mazingira na Idara ya Mazingira na utatekelezwa kwa mashirikiano na wadau mbalimbalikwa upande wa Mabadiliko ya Tabianchi.

HITIMISHO

  1. Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa sana naomba kuchukua nafasi hii kwa mara nyingine tena kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa ya kuwatumikia Wananchi wenzangu kupitia Wizara hii.
  2. Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Wizara na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, naomba kuchukua nafasi hii kutoa shukurani zangu za dhati kwa Nchi marafiki, Mashirika ya Kimataifa na yasiyo ya Kimataifa, Sekta binafsi, NGOs, CBOs na wananchi kwa jumla kwa mashirikiano makubwa waliyoyaonesha kwa Wizara yangu kwa misaada yao ya hali na mali waliyoitoa na wanayoendelea kutoa kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara hii. Washirika hao ni JAPAN, NORWAY, SWEDEN, CHINA, OMAN, FINLAND, UNICEF, UNESCO, UNDP, JICA, Sida, UN HABITAT, AfDB, TASAF, NORAD, BENKI YA DUNIA, RAK GAS TANZANIA, EU, pamoja na wale wote ambao kwa bahati mbaya hatukuweza kuwataja. Tumepata faraja kubwa sana kwa michango yao kwa maendeleo ya nchi yetu, tunaahidi kuienzi na kuiendeleza na kuithamini michango hiyo.
  3. Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein; kwa kuniamini na kunipa dhamana ya kuiongoza Wizara hii pamoja na miongozo yake mbali mbali anayoendelea kupatia ambayo inalengo la utendaji wetu katika kuimarisha sekta zetu muhimu zenye kugusa maisha ya kila siku kwa wananchi wetu.
  4. . Mheshimiwa Spika, Shukurani za pekee kwako Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, Mheshimiwa Mwenyekiti wa Baraza, Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Baraza na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza lako kwa kunisikiliza kwa utulivu na umakini wa hali ya juu.
  5. . Mheshimiwa Spika, shukurani maalumu nazitoa kwanza kwa Mwenzangu na Ndugu yangu Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Ndugu Juma Makungu Juma kwa mashirikiano yake makubwa anayoendelea kunipa katika kuongoza Wizara hii. Vile Vile shukurani kwa Katibu Mkuu Ndugu Ali Khalil Mirza, Katibu Mtendaji Kamisheni ya Ardhi, Wakurugenzi, Mameneja, Afisa Mdhamini, Wenyeviti wa Bodi, Mahakimu na Maafisa wa ngazi zote ambao walinipa mashirikiano yao ya hali juu kwa wakati wote na kutuwezesha kutekeleza malengo na majukumu yetu kwa ufanisi katika kipindi cha mwaka 2015/2016.
  6. . Mheshimiwa Spika, napenda kuishukuru sana familia yangu, mama, baba na mwanangu kwa msaada wao mkubwa ulioniwezesha kufanya kazi zangu vizuri katika kipindi hiki kigumu kwangu kilichonikabili.
  7. . Mheshimiwa Spika, naomba waheshimiwa wajumbe wa Baraza lako Tukufu wayapokee, wayajadili kwa kina, watushauri na kutuelekeza na hatimae wayapitishe makadirio haya. Tunaimani kubwa kuwa michango ya waheshimiwa wajumbe wa Baraza lako hili itatusaidia sana katika kutekeleza majukumu yetu ya kazi vizuri zaidi katika kipindi kijacho cha mwaka wa fedha 2016/2017.
  8. . Mheshimiwa Spika, ili Wizara yangu iweze kutekeleza programu kuu na programu ndogo nilizozieleza, naliomba Baraza lako Tukufu iidhinishe matumizi ya jumla ya Tsh Bilioni 57,456,186,000/= na pia naomba idhini ya kukusanya mapato ya Tsh Bilioni 6,100,000,000/= kutokana na vianzio mbali mbali vilivyomo ndani ya Wizara yangu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
Kwa ufafanuzi zaidi ninaomba muangalie kiambatanisho “H1, H2 na H3”

  1. . Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja






No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.