Habari za Punde

Mkuu wa Wilaya ya Mjini Unguja Ngeni Rasmin Uzinduzi wa Mabaraza ya Vijana Jimbo la Magomeni Zanzibar.

Brassbend ya Chipkizi ikiongoza maandamano ya Vijana wakati wa hafla hiyo ya uzinduzi wa mabaraza ya vijana Jimbo la Magomeni katika shamrashamra za uzinduzi wa mabaraza hayo uliofanyika uwanja wa Magae Meya Mjini Zanzibar.
Mwenyekiti wa mabaraza ya Vijana Jimbo la Magomeni Kassim Lila Msoma akimkaribisha mgeni rasmin katika uzinduzi wa mabaraza ya vijana wa Jimbo la Magomeni, Mkuu wa Wilaya ya Mjini Unguja Bi. Marina  Joel Thomas, mgeni rasmin wa hafla hiyo ya uzinduzi huo.
Mkuu wa Wilaya ya Mjini Bi. Marina Joel Thomas akizungumza na Vijana wa Jimbo la Magomeni katika uzinduzi wa mabaraza ya Vijana Jimbo la Magomeni kabla yakulizindua rasmin Baraza hilo Julay 16, (kulia) Mbunge wa Jimbo hilo Jamal Kassim Ali na (kushoto) Mwenyekiti wa mabaraza ya Vijana Jimbo la Magomeni Kassim Lila Msoma.
Baadhi ya Vijana wa mabaraza ya vijana Jimbo la Magomeni wakimsikiliza Mgeni rasmin Mkuu wa Wilaya ya Mjini Bi. Marina Joel Tomas hayupo (pichani) wakati wa uzinduzi huo.
Mkuu wa Wilaya ya Mjini Bi. Marina Joel Thomas na Mbunge wa Jimbo la Magomeni Mhe.Jamal Kassim Ali wakiwapungia mkono Vijana kuwaaga baada ya uzinduzi wa mabaraza ya Vijana Jimbo la Magomeni.(Picha na Makame Mshenga/Maelezo Zanzibar.

Na Maryam Kidiko/Maelezo Zanzibar. 
Mkuu wa Wilaya ya mjini Marina Joel Thomas amesema lengo la Serikali la kuunda Mabaraza ya Vijana ni kuona Vijana hao wanakaa pamoja ili kujadili mambo muhimu yanayowahusu na kupambana na changamoto zinazowakabili.
Ameyasema hayo katika hafla ya uzinduzi wa Baraza la vijana la jimbo la magomeni iliyofanyika katika uwanja wa magae meya wilaya ya mjini unguja.
Mkuu huyo amefahamisha kuwa mabaraza hayo yatasaidia Vijana hao kuandaa Maandiko ya Miradi mbali mbali  watakayoanzisha katika mabaraza yao kwa lengo la kujikwamua na maisha.
Vile vile amesema kukaa  pamoja vijana hao kutaiwezesha Serikali kupata urahisi wa kuwasaidia vijana kuliko kuwasaidia mmoja mmoja .
Amesema kuwa Fursa za kuwapatia ajira Vijana hao Serikalini ni chache sana hivyo vijana hao wanapaswa kujiunga pamoja na kutafuta namna ya kujiajiri wenyewe.
Aidha mkuu wa wilaya hiyo aliahidi kuwa serikali itakuwa karibu na Vijana hao sambamba na viongozi wa jimbo hilo ili kuzifanyia kazi changamoto zinazoyakabili  mabaraza  hayo.
 Nae Mbunge wa Jimbo la Magomeni Jamal Kassim Ally alisema atashirikiana na Vijana ili kuleta maendeleo katika jimbo lake na kuungana na Serikali ya wilaya pamoja ili kuweza kuinuwa  vipaji walivyokuwa navyo vijana katika jimbo lake  .
“Vijana wamejengewa jukwaa lao maalum la mabaraza ya vijana kuweza kujiendesha wenyewe, kujiajiri pamoja na kuweza kufanya shuhuli mbali mbali za kimaendeleo “Alisema Jamal .
Mbunge Jamal alisema baraza hilo halipo kichama hivyo kila kijana anahaki ya kujiunga katika baraza ili asiweze kupoteza haki zake za msingi kama kijana
Hata hivyo amewataka vijana hao kuitumia vizuri nafasi hiyo waliyoipata na kuepuka majungu yatayoweza kurudisha nyuma maendeleo yao.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa mabaraza ya vijana ya Jimbo la Magomeni Kassim lila Msoma ameiomba serikali kuwa karibu na vijana ili kuweza kuendeleza kutunza maadili yao.
“Serikali ni muhimu kusimamia tamaduni na mila za kizanzibar ili sisi vijana tuweze kufata njia walizopita viongozi wetu na sio kuvuruga mila hizo” Alisema Mwenyekiti huyo.
Akizitaja changamoto mbali mbali zinazowakabili katika jimbo lao alisema vijana hawana elimu ya kutosha ya ujasiriamali hivyo hupelekea vijana wengi kutegemea ajira kutoka Serikalini jambo ambalo hurejesha nyuma maendeleo ya vijana na kujiingiza katika utumiaji wa madawa ya kulevya pamoja na uhalifu .
Hata hivyo alisema vijana hawana ofisi, vianzio vya kuanzishia miradi pamoja na vitendea kazi vitavyoweza kuwaendeshea miradi mbali mbali katika mabaraza yao.
Uzinduzi wa mabaraza ya vijana umefikia mwisho kwa Wilaya ya Mjini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.