Habari za Punde

Tatizo la oxygen Mnazi Mmoja lamalizwa

Na Mwandishi wetu
MAMA wajawazito, watoto wachanga na wanaozaliwa wakiwa na uzito wa chini (njiti) katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja, sasa hawatakuwa na tatizo la upungufu wa hewa ya oxygen, baada ya Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) kutoa shehena kubwa ya hewa hiyo.

Benki hiyo imetoa mitungi mikubwa 150 yenye gesi hiyo, ambayo mbali ya kusaidia makundi hayo pia itatumika katika vyumba vya upasuaji na kwa wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU).

Kabla ya kukabidhiwa msaada huo, Mkurugenzi Mkuu wizara ya afya, Dk. Jamala Adam Taib, alisema hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa hewa ya oxygen na ilikuwa ikihitaji kama mitungi 300 ili kufanikisha utoaji huduma.

Alisema kwa kawaida gesi hiyo inaagizwa kutoka Dar es Salaaam, hata hivyo inachukua muda kuwasili kutokana na uhaba wa mitungi lakini pia tatizo la usafirishaji kwa kuwa inasafirishwa kwa majahazi.

Hata hivyo, alisema mpango wa baadae wa serikali ni kuzalisha kuzalisha gesi hiyo nchini.

Akikabidhi msaada huo kwa Waziri wa Afya, Mahmoud Thabit Kombo, Mkurugenzi Mtendaji wa PBZ, Juma Ameir, alisema msaada huo unalenga kuokoa maisha Wazanzibari.
Alisema PBZ ni benki ya wananchi, hivyo itatumia kila faida inayopata kusaidia miradi na huduma mbali mbali za wananchi ikiwemo huduma za afya.

Nae Waziri Mahmoud, alisema gesi hiyo itaelekezwa katika wodi ya wazazi, watoto na katika maeneo mengine muhimu ikiwemo vyumba vya upasuaji.

Aliipongeza PBZ kwa kuguswa na maisha ya wananchi hasa akina mama na kuzitolea wito taasisi nyengine za fedha kuiga mfano wa benki hiyo.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.