Habari za Punde

2.5 bn/- kujenga nyumba ya kumbukumbu ya Siti Bint Saad Fumba


Na Salum Vuai, MAELEZO
Katika azma ya kuuenzi mchango wa msanii na mwanaharakati mashuhuri wa Zanzibar marehemu Siti binti Saad, kumeandaliwa harambee kubwa kwa lengo la kukusanya fedha za kujenga jengo la kumbukumbu yake.

Mwenyekiti wa taasisi ya Bibi Siti Bint Saad Nassra Mohammed Hilal, amesema katika mkutano na waandishi wa habari kwamba harambee hiyo imepangwa kufanyika Septemba 24, katika hoteli ya Park Hyatt mjini Zanzibar.

Amesema mgeni rasmi katika harambee hiyo itakayoambatana na chakula cha usiku, anatarajiwa kuwa Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein, ambaye atawaongoza waalikwa mbalimbali kutoa michango.

Bi. Nasra amesema tayari taasisi yake imeshapatiwa eneo la kujenga nyumba hiyo katika kijiji cha Fumba Wilaya ya Magharibi B, alikozaliwa marehemu Siti Binti Saad mwaka 1870.

Mbali na harambee hiyo, Mwenyekiti huyo amesema Septemba 18 kutafanywa ziara ya kutembelea eneo hilo la Fumba, ambayo itaongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Ayoub Mohammed Mahmoud, na Septemba 20, Mkuu wa Wilaya ya Mjini Marina Joel Thomas, ataongoza ziara katika nyumba za wazee Sebleni na Welezo.

Aidha amesema mnamo Septemba 21, mwaka huu, taasisi yake imeandaa ziara katika eneo alilozikwa marehemu Siti hapo Rahaleo, mkabala na mkunazi, ambapo Meya wa Manispaa ya Zanzibar Abdulrahman Khatib atakuwa mgeni rasmi.

Siti binti Saad aliyefariki dunia mwezi Juni 1950 alikuwa msanii wa kwanza mwanamke kuimba taarab hadharani na kuitangaza Zanzibar kimataifa, ambapo pia nyimbo zake zilikuwa zikitetea hadhi ya mwanamke na kupiga vita dhuluma na udhalilishaji.

Kiasi cha shilingi bilioni mbili na milioni tano zinahitajika kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hiyo itakayokuwa na sanaa za aina mbalimbali, pamoja na sehemu za kufanyia tafiti za utamaduni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.