HOTUBA YA
MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR, MHE. BALOZI SEIF ALI IDDI WAKATI WA KUTOA HOJA YA KUAHIRISHA MKUTANO WA TATU
WA BARAZA LA TISA LA WAWAKILISHI SIKU YA IJUMAA TAREHE 30 SEPTEMBA, 2016
----------------------
1.
Mheshimiwa Spika, awali
ya yote, sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu na Mwingi wa Rehma kwa
kuendelea kuiweka nchi yetu hii katika hali ya amani, utulivu, umoja na
mshikamano mkubwa. Hali ambayo
imeiwezesha Serikali na wananchi kuendelea na shughuli zao za kila siku bila ya
mtafaruku wa aina yoyote. Aidha, nawaomba wananchi waendelee kuitunza na kuithamini
amani iliopo nchini.
2.
Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena, napenda
kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutukutanisha hapa tukiwa
katika hali ya uzima na afya njema na kutuwezesha kufanikisha vizuri Mkutano wa
Tatu wa Baraza hili Tukufu la Tisa la Wawakilishi, ulioanza tarehe 21 Septemba, 2016. Nimefarijika kuwa kazi zote
zilizopangwa katika ratiba yetu tumezikamilisha kwa wakati na kwa ufanisi
mkubwa.
3.
Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi
maalum kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa
Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kusimamia amani na utulivu hapa nchini pamoja na
kutekeleza kwa vitendo na umahiri mkubwa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Mheshimiwa Rais amekuwa muhubiri mkubwa wa
amani na utulivu wa nchi yetu. Amefanya
hivyo kwa kujua kuwa amani ni chachu ya maendeleo, bila ya amani hakuna
maendeleo. Nawaomba Wajumbe tuungane na
Rais wetu katika kuhubiri amani katika Majimbo yetu.
4.
Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kutoa pole kwa familia, Serikali na Wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kwa kifo cha aliyekuwa Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
wa Awamu ya Pili na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Marehemu Alhaj Aboud Jumbe Mwinyi kilichotokea tarehe 14 Agosti,
2016 na kuzikwa tarehe 15 Agosti,
2016. Marehemu Mzee Jumbe atakumbukwa
kwa michango yake mikubwa kwa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla hasa kwa
kuimarisha demokrasia ikiwemo kutungwa kwa Katiba ya Zanzibar, kuanzisha Baraza
la Wawakilishi pamoja na kuimarishwa mihimili mitatu ya dola, ndiyo maana leo
tunafurahia demokrasia aliyotuachia kupitia chombo hiki tukufu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya
Marehemu Aboud Jumbe mahala pema peponi – Amin.
5.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, napenda kutoa pongezi
za dhati kwa Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, kwa kufanikisha kwa wakati ahadi alizozitoa kwamba ifikapo tarehe 20
Septemba, 2016 Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania tayari itakuwa
imeshanunua ndege mbili mpya, ni
ukweli usiopingika tayari ndege mbili aina Bombadier Dash – 8 Q400
zimeshanunuliwa na kuwasili nchini Tanzania.
Hii imeonyesha imani na upendo wa dhati
alionao kwa wananchi wake wa Tanzania anaowaongoza, pia ndege hizi ni chachu ya kukuza uchumi wa
Tanzania, na zitasaidia usafiri wa uhakika wa Watanzania. Nawaomba watakao kabidhiwa dhamana ya
kuziendesha ndege hizi chini ya Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) waziendeshe
ndege hizo vizuri pamoja na Shirika lenyewe, ili ziweze kutuhudumia kwa muda
mrefu.
6. Mheshimiwa Spika, naomba pia kuchukua nafasi
hii kuwapa pole wananchi wa Tanzania,
Mkoa wa Kagera, kwa madhara waliyoyapata kutokana na tetemeko la ardhi
lilitokea tarehe 10 Septemba, mwaka huu lililosababisha vifo na majeruhi pamoja
na kuathiri miundombinu na makaazi ya watu pamoja na sekta muhimu za kijamii.
Natoa shukrani za dhati kwa Watanzania wote waliopo ndani na nje ya Tanzania,
pamoja na raia wengine wa nchi za nje wakiwemo wa nchi jirani kwa kuonesha
imani kubwa kwa waliopatwa na maafa hayo kwa misaada yao ya hali na mali. Natoa
wito kwa wananchi wote wa ndani na nje
ya Tanzania kuendelea kuchangia kwa hali na mali ili kurejesha hali ya
Mikoa iliyoathirika katika sura mpya.
7.
Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba mnamo tarehe 15 Februari, 2016 Serikali ilitoa
uamuzi wa kuwahamisha wafanya biashara wa makontena Darajani na wale wa jengo
la treni na kuwahamishia eneo la Saateni.
Zoezi hilo lilifanyika kuanzia tarehe 15 Februari, 2016. Uamuzi huo umetokana na haja ya kubadilisha
mandhari na haiba ya mji wetu na sio kuwakomoa wafanya biashara hao kama
inavyodaiwa na baadhi ya watu wasioitakia mema Zanzibar. Aidha, napenda kutoa taarifa kwamba zoezi
hili ni endelevu ambalo litaendelea katika maeneo mengine ambayo wafanya
biashara wameyavamia na kufanya biashara zao bila ya mpango maalum. Serikali ina nia ya dhati ya kuuletea mji wa
Zanzibar haiba inayostahili. Tunawaomba
wananchi waliunge mkono zoezi hili.
8.
Mheshimiwa Spika, nachukua furasa hii kwa niaba ya Baraza lako Tukufu kutoa masikitiko
yetu na pole zetu nyingi kwa wananchi wa Pemba waliokatiwa vipando vyao vya
mikarafuu na miti ya matunda pamoja na kubomolewa nyumba zao bila ya sababu
zozote za msingi. Tunakilaani kwa nguvu
zetu zote kitendo hicho kwani hakikuwa cha kiungwana wala ustaarabu bali
kilikuwa kitendo cha kifisadi tu.
9.
Mheshimiwa Spika,
katika kikao hiki jumla ya Maswali ya Msingi 74 na maswali ya nyongeza 181 yaliulizwa
na yalijibiwa. Naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe kwa
kutumia nafasi yao ya kuihoji Serikali pia natoa pongezi kwa Waheshimiwa
Mawaziri na Manaibu Mawaziri kwa namna walivyojibu maswali hayo na kutoa
ufafanuzi fasaha. Nawapongeza sana
Mawaziri hao wote.
10. Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukurani
na pongezi maalum kwa Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa namna
anavyosaidia katika kutoa ufafanuzi wa kisheria kila lilivyojitokeza jambo
ambalo lilihitaji ufafanuzi wa kisheria, amefanya kazi kubwa na nzuri na
ameonesha umahiri mkubwa katika fani yake ya sheria.
11. Mheshimiwa Spika, miongoni mwa mambo
yaliyojitokeza katika mkutano huu ni harambee ya kuchangia pesa kwa ajili
wananchi waliopatwa na maafa ya tetemeko katika Mkoa wa Kagera na Mikoa jirani.
Baada ya kujadiliwa na Baraza lako Tukufu, Waheshimiwa Wajumbe kwa pamoja
walikubali kuchangia posho ya siku moja kwa kila Mjumbe wa Baraza lako Tukufu
ili liwasilishwe katika Mikoa iliyopatwa na maafa ya tetemeko. Naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru
Waheshimiwa Wajumbe wote kwa uamuzi wao huo na wale wote waliofanikisha zoezi
hili. Michango hiyo ilionyesha
mshikamano wetu Watanzania kila maafa yanapotokea katika nchi yetu.
12. Mheshimiwa Spika, aidha katika mkutano huu,
jumla ya Miswada Minne (5) imejadiliwa na kupitishwa kuwa Sheria na Baraza lako
Tukufu. Miswada yenyewe ni:-
i Mswada wa Sheria ya Kuanzisha
Taasisi ya Elimu ya Zanzibar na Mambo mengine Yanayohusiana na Hayo.
ii Mswaada
wa Sheria ya Kurekebisha Sheria ya Chuo
Kikuu cha Taifa cha Zanzibar Nam. 8 ya 1999 kama ilivyorekebishwa na Sheria
Nam. 11 ya mwaka 2009 na Kuwekwa Masharti Bora Pamoja na Mambo Mengine
Yanayohusiana na Hayo.
iii Mswada
wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbali mbali na kuweka Masharti yaliyo Bora kuhusiana na mambo hayo.
iv Mswada wa sheria ya mafuta (utafiti na
uchimbaji) na gesi asilia.
v. Mswada wa Sheria wa kufanya marekebisho ya
11 ya Katiba ya Zanzibar inayohusu kifungu cha 66. Kwa kupitishwa Mswada huu, Rais kwa sasa
ataweza kuzitumia nafasi zake 10 bila ya kuwepo kwa masharti magumu ya Kikatiba
na hasa kuhusiana na nafasi mbili kwa ajili ya upande wa upinzani.
13. Mheshimiwa Spika, ni imani yangu kwamba Miswada hiyo mitano
tuliyoipitisha itasaidia kwa kuweka misingi bora ya utendaji na pia kukuza uchumi wa Zanzibar. Ni
ukweli usiopingika kwamba kupatikana kwa
mafuta na gesi kutaiwezesha nchi yetu kukua kwa haraka kiuchumi, kwa kuiongezea mapato Serikali na wananchi kwa
ujumla, na pia kuongeza ajira kwa wananchi wetu.
14. Mheshimiwa Spika, yote hayo yataweza kufikiwa iwapo Sheria
tulizozitunga katika Baraza hili tutashirikiana
katika kuifanya kazi kama inavyotakiwa, hata hivyo napenda kutanabahisha
kwamba tulichokuwa nacho hivi sasa ni sheria na sio mafuta na gesi. Baada ya
kukamilika kwa utafiti ndipo itajulikana kiwango gani cha mafuta na gesi asilia
kilichopo nchini.
15. Mheshimiwa Spika, kupitishwa kwa Mswada wa
mafuta na gesi asilia ni jambo la historia kwetu. Hivyo, Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi amekubali kuiweka saini Sheria hiyo mbele ya
Vyombo vya Habari pamoja na Kamati ya Katiba na Sheria ya Baraza la Wawakilishi
na Kamati ya Uongozi ya Baraza la Wawakilishi.
Nawaahidi Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kuwa
haitochukua muda mrefu kitendo hicho kufanyika.
Nawapongeza Wajumbe kwa kuipitisha Miswada hiyo kwa sauti moja.
16. Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua hofu
waliyonayo baadhi ya wananchi juu ya
mikataba ya masuala ya mafuta na gesi.
Kwa kulitambua hilo Serikali imejipanga vyema kuwa na mikataba bora
ambayo italeta tija kwa nchi yetu na watu wake.
Aidha, mikataba yote itakayohusiana na mafuta na gesi asilia itafanywa
kwa uwazi. Lengo ni kuwa na uwazi ambao
utaipatia heshima nchi yetu na kupunguza malalamiko na minong’ono isiyokuwa ya
lazima.
17. Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru wale wote
waliotuwezesha kukamilisha shughuli zilizopangwa kwenye Mkutano huu wa Tatu wa
Baraza la Tisa la Wawakilishi kwa ufanisi mkubwa. Pongezi hizo zaidi ziwafikie watendaji wote
wa Baraza hili la Wawakilishi wakiongozwa na Katibu, Ndugu Raya Issa
Msellem. Ni ukweli usiofichika kwamba
tumeanza vizuri na ninaamini tutaendelea vizuri. Mungu libariki Baraza hili, Mungu zibariki
Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Pia
nawapongeza wakalimani wetu wa lugha ya alama ambao wamewawezesha Waheshimiwa
Wawakilishi wenye ulemavu wa kusikia kufuatilia yote yaliyokuwa yakiendelea
ndani ya Baraza. Vile vile nawashukuru
Wanahabari kwa kufanya kazi ya kuwahabarisha wananchi wetu yale yaliyokuwa
yakiendelea Barazani hapa.
Mwisho,
Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe, Mhe. Naibu Spika na Wenyeviti wa Baraza kwa
kuliongoza vizuri na kwa ufanisi mkubwa Baraza hili. Hekima na busara zenu zimesaidia sana katika
kuumaliza mkutano huu salama.
18. Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia niwatakie
Waheshimiwa Wawakilishi kila la kheri na mafanikio mema katika kuwatumikia
wananchi wao Majimboni mwao. Aidha,
nawatakia safari njema na ya salama ya kurudi Majimboni mwao, na hasa
Wawakilishi wenzetu kutoka Pemba kwa sababu wao wana safari ndefu zaidi kuliko
wenzao wa Unguja.
19. Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo,
naomba sasa kwa heshima na taadhima kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu
liahirishwe hadi siku ya Jumatano tarehe 23 Novemba, 2016, saa 3.00 barabara za
asubuhi panapo majaaliwa.
20.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment