Naam
Mina ni Masha’aril Haraam mojawapo katika sehemu takatifu kwa Waislamu ni
sehemu ambayo ukiomba kwa Allaah ‘Azza wa Jall hutakabaliwa du’aa yako.
Nilijitahidi kuomba na kila Muislamu ninaemuona yumo katika maombi, au dhikr au
anasoma Qur’aan mpaka nafsi inanisuta mbona siku zote ulikuwa hufanyi Ibada
kama hivi? Nikaijibu nipo katika sehemu takatifu na nimekuja kwenye mafunzo ya
vitendo nafsi we. Naam nikajaaliwa kuzisali sala za Adhuhuri, Alasiri,
Magharibi na Isha pamoja na Alfajiri Jamaa kwa kupunguza Sala zenye rakaa nne
kama alivyofanya Mtume Swalla Allaahu ‘Alayhi Wasallam alipohiji.
Tulipoamka
Alfajiri siku ya pili ya mafunzo, Siku ya Arafah siku adhimu katika masiku ya
dunia, siku muhimu kwa mwenye kuhiji kwani ndiyo nguzo kuu ya Hajj ambayo
ikikosekana basi aliyefanya safari hii hana Hajj, tulijiandaa kuelekea Arafah
asubuhi na mapema kutoka Mina.
Tulipowasili
viwanja vya ‘Arafah, nilihakikisha nipo katika mipaka yake ili Ibada yangu
ikamilike. Tulibahatika mwaka huu siku ya ‘Arafah kuangukia Ijumaa kama
ilivyokuwa kwa kipenzi chetu Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam miaka 1435
iliyopita hivyo tukapata fursa mbili za kuweza kukubaliwa duaa, maombi, shida
na matlaba yetu – fusa ya ‘Arafah na fursa ya Ijumaa.
Ilipofika
muda wa kuanza ‘Arafah (baada ya Zawaal yaani jua kutenguka) tulisali Adhuhuri
na Alasiri jamaa ya kutanguliza na kupunguza kwa kuzisali rakaa mbili mbili.
Kisha tukatangaziwa kwamba ule muda ambao shetani anaukasirikia kadri ya
kukasirika umefika wa kupeleka maombi yetu, shahada zetu, maelezo yetu, CV zetu
kwa Allaah ‘Azza wa Jall umeanza.
Siku
ambayo Mtume wetu Swalla Allaahu ‘Alayhi wasallam ambaye tayari ameshasamehewa
madhambi yake yaliotangulia na yatakayokuja alisimama kuanzia adhuhuri mpaka
kuzama kwa jua akiomba tu huku mikono yake akiwa ameinyanyua kwa masaa takriban
sita. Nikajiuliza wapi mimi na Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam? Nikajiambia kimoyomoyo nijaribu kuiga mwenendo
wake nikatoka nje ya hema nikaelekea qiblah na kuanza kuomba kila dua
ninayoijua au niliyobahatika kuisikia na kuihakikisha si miongoni mwa dua
zilizokuwa na walakini.
Ni
siku ambayo niliingiwa na simanzi, mwili nikausikia una joto na huku chozi
likinitoka ninamuomba Allaah ’Azza wa Jall kwani niliwahi kuisikia hadithi ya
Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam inayosema jicho litalotoa machozi kwa
ajili ya Allaah halitogusa moto siku ya kiama! Naam licha ya jitihada zangu sikumfikia
au kuifikia rekodi ya Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi Wasallam.
Kulikuwa
na joto lakini sikujali, kwani sikuwa pekee yangu kwenye jua, mamilioni ya
waislamu tulikuwepo ‘Arafah sote tukifanya jambo moja tu; Kuomba. Joto ni kitu
gani mbele ya joto la moto wa Jahannam!
Naam
‘Arafah ni siku adhimu, ‘Arafah ni siku pekee ambayo haina mfano wake kwani
hakuna siku katika masiku ya dunia ambayo Allaah ‘Azza wa Jall huwaachia huru waja
wake na moto kwa wingi kama siku ya ‘Arafah. Ndio maana shetani huichukia.
Allaah
‘Azza wa Jall katika siku hii huwa karibu na Malaika na kuwauliza: “Wanataka
kitu gani waja wangu hawa?” Allaahu Akbar.
Naam
ikiwa ‘Allah ‘Azza wa Jall amewasamehe waja wake siku hii hata na mimi
nilipokuwa nimesimama ‘Arafah nilimhakikishia Allaah ‘Azza wa Jall kwamba
nimewasamehe wote walionikosea. Kwanini nisiwasamehe wakati nimehakikishiwa
ikiwa Hijja yangu itakubaliwa basi nitarudi kama ndio kwanza nazaliwa?
Nilipozaliwa sikuwa na niliemkosea wala alienikosea.
Kwanini
nisiwasamehe wakati Mtume Swalla Allaahu ‘alayahi wasallam alipofika Makkah na
kuikomboa aliwasamehe Maquraysh wote licha ya madhila, mateso na kila baya
walilowatendea waislamu na aliwauliza: “Mnadhani nitakufanyeni nini leo?”
Wakamjibu ‘Ndugu yetu uliye karimu , mtoto wa ndugu yetu aliye karimu’. Mtume
Swalla Allaahu ‘Alayhi wasallam akawaambia: “Nendeni nyote mko huru” Hili ni
darsa muhimu la kujifunza ndugu yangu tuwe ni wenye kusameheana kwa ajili ya
kupata radhi zake Allaah ‘Azza wa Jalla. Kama angelikuwa Allaah ‘Azza wa Jall
si mwenye kusamehe basi dunia hii isingelikalika ndio maana amejinasibu kuwa Yeye
ni Ghaafir – mwingi wa kusamehe na pia Ghaffaar - anaendelea kusamehe (kila
tukifanya makosa basi turudi kwake tuombe msamaha)
Ndugu
yangu katika imani unaeusoma waraka huu, ukitaka upate mafunzo
yatakayobadilisha mwenendo mzima wa maisha yako, jihimu uende Hijja na
ukasimame ‘Arafah. Ukitaka ujihisi upo karibu na Allaah ‘Azza wa Jall na huku
akisikia maombi na duaa zako, jihimu uende Hijja na umuombe Allaah ‘Azza wa
Jall siku ya ‘Arafah. Ukitaka kuachiwa huru na moto, jihimu uende Hijja na
uwepo katika viwanja vya ‘Arafah ukimuomba Allaah ‘Azza wa Jall maombi
yanayotoka ndani ya moyo wako, yaliyojaa Ikhlaas na kumthibitishia Allaah ‘Azza
wa Jall kwamba ni yeye pekee ndiye mwenye kupokea na kuyakubali maombi yote
yawe makubwa au madogo.
Itaendelea...
Itaendelea...
No comments:
Post a Comment