Habari za Punde

Kumbukumbu ya Hijja na athari zake - 3

Ilipofika magharibi mafunzo yetu yakaendelea kwa kwenda viwanja vya Muzdalifah kutekeleza moja katika mambo yaliyo wajibu katika Hijja.

Muzdalifah nimekutana na mafundisho kadhaa kama la kutakiwa kulala nje tena chini kwenye jangwa lisilo na kitu chochote. Ni fundisho kubwa sana kwani hapo kila aliyekuja Hijja bila ya kujali uwezo wake, ulwa wake, cheo chake anatakiwa kulala chini kama alivyolala Mtume wetu Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam na akatukumbusha kwamba: “chukueni kutoka kwangu matendo yenu ya Hajj”. Ndiyo nina kitanda cha sita kwa sita nyumbani lakini Muzdalifah nimelala chini kwa ajili ya kutekeleza Manaasik ya Hijja.

Muzdalifah hukutanika Mahujjaaj wote wakiwa dhalili wakiwa na shuka mbili tu licha ya utajiri waliojaaliwa nao, wakilala sehemu ya ardhi isiyokuwa na tandiko zaidi ya zulia au busati kwa atakayejaaliwa licha ya neema ambazo Allaah ‘Azza wa Jall amewajaalia baadhi ya waja wake. Yote ni kwa ajili ya kutufundisha fundisho muhimu katika maisha kwamba tuondokane na kiburi na majivuni kwani licha ya kujaaliwa kila tulichojaaliwa lakini utukufu ni wa Allaah ‘Azza wa Jall pekee - Mwenye nguvu na mshindi na kuwepo kwetu Muzdalifah tunauthibitisha utukufu huu kwa vitendo. Allaahu Akbar

Naam tulipofika Muzdalifah tukasali Magharibi na Isha kwa kuzichanganya na kupunguza Isha kwa kuisali rakaa mbili.

Kisha tukatakiwa kuokota vijiwe vidogo tu saizi ya kokwa ya ubuyu kwa ajili ya kupiga Minara ya Jamaraat. Nikaokota vijiwe sabini na kuongeza vichache.   Kwa nini sabini? Kwa sababu nitatakiwa kuvitumia kwa muda wa masiku matatu kama sina haraka na kama nina haraka ningetumia kwa masiku mawili. Ndivyo alivyotupa rukhsa Allaah ‘Azza wa jall katika Qur’aan.

Lakini nilipovipitia vitabu vikanikumbusha kwamba kama nikitaka hasa kumfuata Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam  yeye aliokota vijiwe saba tu Muzdalifah kwa ajili ya kupiga Jamaratul Kubra pekee ama vijiwe vyengine aliviokota Mina. Mina pia kumeruhusiwa kuokota vijiwe.

Nikapanda basi kurudi Mina nikitokea Muzdalifah huku nikiwapita maelfu na maelfu ya Mahujjaaj waliokuwa wakielekea Mina kwa miguu.! Namshukuru Subhaana kwa kujaaliwa usafiri lakini hapo nikajiuliza hivi Hijja yangu ni bora zaidi au Hijja ya waendao kwa miguu?


Nikamkumbuka Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam yeye alipohiji, alihiji akiwa juu ya Ngamia. Kwa hivyo nikajikinaisha kwamba ninaetekeleza Sunnah ya Mtume wetu Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam.

Itaendelea...

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.