Habari za Punde

Serikali itahakikisha maslahi ya wafanyakazi wa vyombo vya habari yanaboreshwa


 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                 19.09.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema Serikali itafanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya wafanyakazi wa  vyombo vya habari vya serikali yanaimarishwa ili kurejesha hadhi ya taasisi hizo.

Dk. Shein ambaye alivitembelea vyombo vya habari vya Redio pamoja na gazeti la Zanzibar Leo na kufanya mahojiano maalum na Shirika la Habari na Utangazaji Zanzibar ZBC, alisema ameridhishwa na utendaji wa kazi wa viongozi na wafanyakazi wa vyombo hivyo ambao amesema, wamekuwa wakijitahidi kufanya kazi vizuri licha ya changamoto kadhaa wanazokabiliana nazo.

Amesema Serikali imedhamiria kulifanyia marekebisho makubwa Shirika la Habari na Utangazaji Zanzibar na vyombo vyote vya habari vya Serikali sio tu kwa kuinua viwango vya mishahara ya wafanyakazi,  lakini vile vile kuweza kutoa tuzo maalum kila inapohitajika kufanya hivyo kwa wafanyakazi watakaofanya kazi zao vizuri kuinua ari na motisha wa wafanyakazi.

Ameongeza kuwa mchakato unaendelea wa kutayarisha na hatimaye kurejesha miundo ya utumishi “scheme of service” ambayo kwa kiasi kikubwa nayo iterejesha heshima ya kazi ambayo ilionekana kupungua siku za hivi karibuni ikilinganishwa na miaka iliyopita wakati ilipokuwa ikitumika vyema.

Amefahamisha kuwa katika hatua za awali kuelekea kuziimarisha taasisi za vyombo vya habari vya Serikali, Serikali imeshatoa agizo kuitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo kuandaa posho maalum kwa wafanyakazi ambao wanajulikana kuwa wanafanyakazi katika mazingira magumu.

Akizungumzia baadhi ya wafanyakazi ambao wameondoka kwenye vyombo vya habari vya Serikali kutokana na maslahi duni na mazingira yasiyoridhisha, Rais wa Zanzibar alisema ana matumaini makubwa kwamba wengi miongoni mwa wafanyakazi hao wataweza kurejea siku zijazo kama ambavyo wamekuwa wakifanya wengine wengi kwenye taasisi mbali mbali.

“nyumbani ni nyumbani, naamini iwapo tutaimarisha mazingira bora ya kazi watarejea, wengi tumewaona wakirejea kutokana na mapenzi yao na nyumbani” alisema.

Amesema pamoja na ukweli kwamba katika kipindi cha kwanza cha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya saba ilifanya mabadiliko makubwa ya mishahara ambayo hayajawahi kufanywa kabla, wapo baadhi ya watumishi wa umma ambao kwao bado viwango hivyo vya mishahara havijawaridhisha sana.

Hata hivyo Dk. Shein alielezea matumaini yake kwamba katika kipindi cha miezi sita au saba ijayo, hali ya vyombo vya habari vya Zanzibar itabadilika na kwamba watu wengi watavutiwa kufanyakazi kwenye vyombo hivyo.

Kuhusu gazeti la Zanzibar Leo, Rais wa Zanzibar alisema Serikali imeshanunua mitambo mipya ya kisasa ya uchapishaji ambayo itatumika pia, kuchapishia  gazeti hilo badala ya kuchapishwa nje ya Zanzibar, jambo linalosababisha mrundikano mkubwa wa deni la gharama za uchapishaji.

Nao wafanyakazi na watendaji wa vyombo hivyo vya habari walitoa pongezi zao za dhati kwa Dk. Shein kwa kufanya ziara yake hiyo ya hafla ya kuwatembelea pamoja na kuwasikiliza changamoto walizonazo.

Jumamosi iliyopita, Rais wa Zanzibar alikutana na uongozi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Uongozi wa Shirika la Habari na Utangazaji Zanzibar (ZBC) pamoja na Uongozi wa Zanzibar Leo  kuzungumzia njia ambazo zatasaidia kuimarisha zaidi matangazo ya Redio na TV za Shirika la Habari na Utangazaji Zanzibar – ZBC.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.