Habari za Punde

WEMA Yashauriwa Kuweka Mitaala ya Maadili

Na Mwanaisha Mohammed-Maelezo.
Wazara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar imeshauriwa kuanzisha mitaala itakayowafundisha wanafunzi mbinu za kujiepusha na vishawishi vya ngono vinavyoweza kuwaletea madhara na mbimba za umri mdogo.
Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA) Fatma Iddi Ali, amesema mafunzo hayo ni muhimu ili kuwalinda watoto wa kike dhidi ya watu waovu.
Ushauri huo ameutoa wakati akiwasilisha mada kwenye warsha ya mafunzo kuhusu vitendo vya udhalilishaji inayofanyika katika ukumbi wa Idara ya watu wenye ulemavu Kikwajuni mjini Zanzibar.
Fatma ametaja madhara yatokanayo na mimba za umri mdogo ikiwemo vifo vya mama na watoto na kuharibika kwa mfumo wa uzazi.
Alieleza kuwa kuathirika kwa kizazi husababisha mama kutolewa fuko la uzazi na  hivyo kumfanya asiweze kubeba ujauzito kabisa.
Aidha amewakumbusha wazazi wajibu wa kukaa na kuzungumzana watoto ili waweze kufahamu matatizo waliyonayo na kutafuta njia za kuyatatua mapema.
Mjumbe huyo wa ZAFELA pia amekumbusha jukumu la wazazi na wanajamii kurejesha malezi ya asili na kushirikiana katika kuwalea watoto ili wakue katika maadili mazuri.   
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa jumuiya hiyo Saada Salum Issa, amewahimiza wazazi kujenga utamaduni wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao maskulini, hasa katika masomo ya ziada (Tuitions) kwani baadhi yao huitumia fursa hiyo kujiingiza katika vitendo viovu.
“Pamoja na hayo, wazazi pia wanapaswa kutowadekeza mno watoto wao kwani  kufanya hivyo kutawapa kiburi na kuvuka mipaka ya nidhamu,” alisema.
Katika hatua nyengine, Mwenyekiti huyo amewaomba wazazi na walezi wasiwape simu watoto wakiwa wanafunzi, akisema teknolojia hiyo inachangia katika kuwapotosha kwa vile wanaitumia vibaya badala ya kujifunza mambo ya maana yaliyomo ndani yake.


IMETOLEWA NA IDARA YA HABARI MAELEZO

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.