Habari za Punde

Dk Shein aipongeza Wizara ya Kilimo, maliasili, Mifugo na Mazingira



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                     24.10.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amepongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Mazingira ikiwa ni pamoja na azma ya kuupandisha hadhi msitu wa Masingini kuwa msitu wa hifadhi.

Hayo aliyasema leo katika kikao maalum kilichofanyika,  Ikulu mjini Zanzibar ambapo Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Mazingira ilipowasilisha Taarifa yake ya  Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara  hiyo kwa kipindi cha Julai hadi Septemba katika Bajeti ya mwaka 2016-2017.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuziimarisha sekta za kilimo, mifugo na uvuvi kwa kutambua umuhimu wake mkubwa kwa maendeleo ya nchi pamoja na wananchi wake.

Dk. Shein alisisistiza haja ya kuendeleza mchakato wa kuanzisha kiwanda cha matreka hapa nchini kama ilivyoamua Serikali, kwani tayari hatua za awali zimeshafanyika kwa kuzingatia kuwa kilimo huimarika panapokuwa na huduma za matrekta.

Aidha, Dk. Shein  alisisitiza umuhimu wa kuwepo Baraza moja la kilimo ambalo litakuwa na nguvu kubwa ya kufanya kazi huku akitilia mkazo kuongezwa nguvu katika maendeleo ya mifugo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza haja kwa uongozi wa Wizara hiyo kuendelea na juhudi za kuulinda msitu huo wa Masingini ili kuepuka kuja kuvamiwa kwa ujenzi huku akitumia fursa hiyo kuitaka Wizara hiyo kusimamia na kudhibiti vyema maliasili zisizorejesheka ili kuepuka athari zaidi za hapo baadae.

Mapema Waziri wa Kilimo, Malisili, Mifugo na Uvuvi, Hamad Rashid Mohamed alisema kuwa sekta ya kilimo inajumuisha sekta ndogo za mazao, mifugo, uvuvi na misitu bado inaendelea kuwa ni mhimili mkuu wa uchumi wa Zanzibar na inatoa mchango wa moja kwa moja katika kujikimu kimaisha.

Alisema kuwa sekta hiyo imekuwa ikitoa ajira rasmi kwa wastani wa asilimia 40 na zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wanategemea sekta hiyo kwa njia moja au nyengine katika kujipatia kipato na kuimarisha maisha yao.

Alisema kuwa muelekeo wa Wizara hiyo ni kuendeleza mageuzi ya sekta ya kilimo kwa lengo la kukibadilisha kilimo kutoka cha kujikimu kuwa cha kibiashara pamoja na kuongeza tija na kipato kwa wazalishaji na kupunguza kuagiza chakula kutoka nje ya nchi.

Akieleza miongoni mwa mafanikio yaliopatikana Julai hadi Septemba mwaka huu, Waziri huyo alieleza kuwa ni pamoja na kuongeza idadi ya wafugaji wa ngombe wa kisasa, kufundisha mabwana mifugo binafsi wa vijijini, kuimarika huduma za ugani, kuongezeka kwa uzalishaji wa mayai, kuendeleza miundombinu ya utafiti na mengineyo.

Pamoja na hayo, Waziri huyo wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi alieleza kuwa Wizara kwa kushirikiana na uongozi wa Mikoa, Wilaya, Shehia na Jumuiya za wakulima inaendelea kuhamasisha wakulima wachangine kwa wakati huduma za matrekta ili kuwahi msimu wa kilimo cha mpunga.

Uongozi huo pia, ulieleza azma yake ya kuupandisha hadhi msitu wa Masingini kuwa msitu wa hifadhi kwani sifa zote za kuwa msitu wa hifadhi na umekuwa kivutio kikubwa cha watalii kutokana na vivutio vilivyomo ndani yake.

Nae Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd, aliipongeza Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpangokazi wake na kusisitiza haja ya kuendelea na mikakati ya kudhibiti misumeno ya moto kwa mashirikiano ya pamoja.

Dk. Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alielza haja y kwa uongozi wa Wizara hiyo kuwahamasisha wananchi katika matumizi ya majiko ya gesi ili kuepuka matumizi ya kuni na makaa.

Aidha, aliupongeza uongozi wa Wizara hiyo pamoja na watendaji wake kwa matayarisho mazuri ya Mpangokazi huo huku akitaka juhudi za makususdi ziendelee kuchukuliwa katika kulipatia ufumbuzi suala la bei ya kilimo cha mwani.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.