Mhe. Othman Chande, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania;
Mhe. George Masaju, Mwanasheria Mkuu wa Serikali;
Mhe. Jaji (Mstaaf)
Damian Lubuva; Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Taifa
Mhe. Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mhe. Bahame Nyanduga, Mwenyekiti wa Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora;
Wahe. Makamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora;
Ndugu Joseph Butiku, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya
Mwalimu Nyerere
Mwakilishi wa Ubalozi wa Sweden nchini Tanzania;
Mhe Amiri R.
Manento (Jaji Kiongozi Mstaafu), Mwenyekiti Mstaafu wa Tume ya Haki za Binadamu
na Utawala Bora;
Wahe. Viongozi wa Serikali na Wawakilishi wa Vyama vya
Siasa mliopo hapa;
Wawakilishi wa Asasi mbalimbali za Kiraia;
Viongozi na watumishi mbalimbali mliopo hapa;
Ndugu Wana Habari;
Ndugu Wananchi na Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana.
Habari za Asubuhi!
Napenda nianze,
kwa kutoa salamu kutoka kwa Mhe. Dr John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, ambaye ndiye alitegemewa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho
haya siku ya leo, lakini kutokana na
majukumu yake mengi ya kitaifa ameniagiza nimuwakilishe.
Nitumie nafasi
hii kuwakaribisha wageni waalikwa kutoka nje ya Nchi waliokuja nchini kwa ajili
ya maadhimisho haya, poleni na safari ndefu na karibuni sana Dar es Salaam. Niwapongeze
nyote mliofika mahali hapa naamini mmefanya hivi kutokana na sababu moja tu
kubwa, nayo ni kwamba; kila mmoja wenu anathamini na kujali umuhimu wa kujenga
taasisi za uwajibikaji na utawala bora. Binafsi nimefurahi kujumuika nanyi na
kuwa sehemu ya washiriki wa tukio hili muhimu na la kihistoria. Ni matumaini
yangu kuwa wageni wetu mkiwa hapa mtapata fursa ya kutembelea vivutio
mbalimbali vilivyoko Nchini mwetu, kama vile mbuga za wanyama, mji wa
kihistoria wa Zanzibar, mlima mrefu kupita yote Afrika Mlima Kilimanjaro na ni
matumaini yangu kuwa mtafurahia vivutio hivyo na kuwa kumbukumbu katika safari na
maisha yenu.
Niwashukuru Tume
ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Taasisi ya Mwalimu Nyerere (The Mwalimu Nyerere Foundation) kwa
jitihada zao kubwa za kuandaa, kuratibu na hatimaye kufanikisha Maadhimisho haya.
Hongereni sana!
Ndugu Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora, waheshimiwa viongozi na wageni waalikwa, Ni heshima kubwa kwa Taifa letu kuadhimisha kumbukumbu ya miaka hamsini katika
kushughulikia malalamiko ya Wananchi waliohisi wameonewa kupitia Tume ya Kudumu ya Uchunguzi hapo nyuma na
hivi sasa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.
Historia
inatukumbusha kuwa, baada ya kupatikana uhuru mwaka 1961, taifa letu likiwa
changa Serikali ilichukuwa hatua mbali mbali za kuunda vyombo vyake ili
kuwahudumia Wananchi wake. Kwa nia njema
kabisa, moja ya hatua hizo ilikuwa kuunda chombo chenye madaraka ambacho kitasimamia
utendaji wa Viongozi waliokuwa katika Chama, Serikali na Mashirika ya Umma. Hivyo pendekezo la kuundwa kwa Tume ya Kudumu
ya Uchunguzi lilitokana na Taarifa ya Tume ya Rais iliyoundwa Mwaka 1964 ili kukusanya
maoni kuhusu Muundo wa Serikali ya Kidemokrasia ya Chama kimoja cha siasa.
Katika taarifa
yake ambayo ilitolewa mnamo tarehe 22 Machi, 1965 Tume hiyo kwa kifupi
ilishauri kuundwa kwa Tume ya Kudumu ya Uchunguzi kama chombo ambacho kitadhibiti
matumizi ya madaraka waliopewa Viongozi na wakati huo huo kutetea Wananchi ambao
haki zao zitakuwa zimevunjwa au ziko katika hatari ya kuvunjwa.
Chama na Serikali
vilikubali pendekezo hilo na Tume ya Kudumu ya Uchunguzi ikaingizwa rasmi kwenye
Katiba ya Mpito ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Interim Constitution) ya Mwaka 1965. Mwaka 1966 Bunge lilipitisha Sheria (Act No.
25 of 1966) ya Tume ya Kudumu ya
Uchunguzi iliyoiwezesha kutekeleza shughuli zake za kila siku. Kwa kuwa chombo
hicho kilikuwa cha Muungano, Mwaka 1980 Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
iliridhia Tume ya Kudumu ya Uchunguzi kufanya kazi zake Zanzibar.
Ndugu
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Mwaka huu (2016)
Tanzania inaadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Tume ya Kudumu ya Uchunguzi
(TKU) au kwa neno maarufu “Ombudsman”. Neno “Ombudsman” ni neno lenye chimbuko la lugha
ya Sweden likiwa na maana ya “Mlinzi” au “Mtetezi wa haki za jamii”. Neno hilo lina asili ya Sweden kwani ndio nchi
ya kwanza duniani kuanzisha taasisi ya “Ombudsman” mwaka 1807. Nchi zingine za
Ulaya kama Uingereza zina mtambua Kiongozi wa taasisi hiyo kama “Kamishna wa
Haki”.
Majukumu ya
taasisi hizi za “Ombudsman” ni
kumlinda na kumtetea mwananchi mnyonge, kutokana na kuonewa na mifumo ya
kiutawala au matumizi mabaya ya madaraka ya watendaji wa Serikali. Kulingana na
maudhui ya taasisi ya “Ombudsman” Mwananchi
anayepeleka malalamiko hupata huduma bila malipo, tofauti na mfumo wa kutafuta
haki wa mahakama ambao umewekewa utaratibu unaohitaji malipo pale mtu anapotaka
kufungua kesi. Ofisi za “Ombudsman” hazina vikwazo (technicalities) katika kuwasilisha
malalamiko na kuyafanyia uchunguzi .
Nina furaha
kusema kuwa lengo kubwa la Serikali kuanzisha Tume ilikuwa ni kumlinda Mwananchi
na liliweza kufikiwa kwa kupitia takwimu za malalamiko yaliyopokelewa katika
kipindi cha miaka 35 ya Tume ya Kudumu ya Uchunguzi yaliyoshughulikiwa na
kukamilishwa kwa kupatikana haki. Katika kipindi cha kuanzishwa kwake, jumla ya
malalamiko 39,000 yalishughulikiwa.
Aidha malalamiko yaliyopokelewa katika kipindi cha miaka 15 (2001-2016)
ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ni 32,000 na hivyo kufanya idadi ya
malalamiko yote katika miaka 50 kufikia 71,000. Idadi hiyo inaonesha jinsi vyombo
hivi vilivyo na manufaa kwa Wananchi wanyonge. Baadhi ya malalamiko yaliyopokelewa yalihusu masuala
yafuatayo:-
·
Vitendo vya unyanyasaji,
·
Masuala ya Utumishi/malipo/mafao
·
Kuchelewa kutekeleza
wajibu
·
Kukataliwa kuomba rufaa
·
Kutofuata taratibu za
kisheria
·
Mirathi
·
Matumizi mabaya ya Mali
ya Umma
·
Migogoro ya ardhi n.k.
Matokeo ya
uchunguzi na mapendekezo ya Tume yalikuwa yanafanywa bila woga wala upendeleo
na yanawasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa maamuzi.
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Yapo mafanikio
mengi Nchi yetu inajivunia kwani pamoja na Wananchi kupata mwamko na
kuwasilisha malalamiko yao kwenye Tume, zilianzishwa pia taasisi mpya za
uangalizi (watch dog) kama Taasisi ya
Kupambana na Rushwa ambayo baadaye
ilibadilika kuwa Taasisi ya Kuzuzia na Kupambana na Rushwa- TAKUKURU na Sekretarieti
ya Maadili ya Viongozi wa Umma, ambazo zote ziliundwa kulinda utawala wa Sheria,
uwajibikaji, maadili na demokrasia.
Napenda nichukue
nafasi ya kipekee kumuenzi Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage
Nyerere kwa kuanzisha Tume ya Kudumu ya Uchunguzi. Napenda pia kuwaenzi na
kuwapongeza Wajumbe wa Tume iliyopendekeza kuanzishwa kwa Tume ya Kudumu ya
Uchunguzi. Napenda pia nitumie nafasi hii kutoa pongezi za kipekee kwa Wenyeviti,
Makamishna, Makatibu, na Watumishi wote waliotumikia Tume ya Kudumu ya
Uchunguzi. Kwa wale waliopo nasi leo nawapongeza sana. Kwa wale wote waliotangulia
mbele ya haki, pongezi hizi ziwafikie ndugu zao kwa niaba yao kwani mchango wao
uliwezesha Tume ya Kudumu ya Uchunguzi kuanzishwa kama taasisi ya kwanza ya
“Ombudsman”, barani Afrika, Kusini mwa
jangwa la Sahara na kuendelea kutumikia Umma wa Watanzania kwa miaka 35
kama Mlinzi au Mtetezi wa Umma.
Wakati chombo
hiki kikiendelea kufanya kazi kwa ufanisi kwa miaka zaidi ya 35, dhana ya haki za binadamu ikiwa sehemu muhimu ya
Utawala wa Sheria, iliingizwa katika Katiba
za mataifa mengi duniani. Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuona umuhimu huo ilianzisha mchakato wa
kurekebisha Katiba kwa kuingiza pamoja na mambo megine, masuala ya haki za
binadamu. Hivyo kutokana na mabadiliko
ya Katiba ya 13 ya Bunge la Katiba la
mwaka 2000 Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliingizwa kwenye Katiba. Kulingana
na mabadiliko hayo majukumu ya Tume ya Kudumu ya Uchunguzi yaliunganishwa na
majukumu ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, taasisi ambayo imeendelea
na uchunguzi wa malalamiko dhidi ya matumizi mabaya ya madaraka ambayo kama
tulivyo ona yalikuwa yanashughulikiwa na Tume ya Kudumu ya Uchunguzi.
Nitoe wito kwa
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kuyaenzi yale yote yaliyofanywa na
Tume ya Kudumu ya Uchunguzi kwa kuwa kazi zake bado zinahitajika sana katika
jamii. Serikali itaendelea kushirikiana na Tume na kuiwezesha kutekeleza
majukumu yake ya kulinda na kutetea misingi ya Utawala Bora na kulinda haki za
binadamu kwa mujibu wa Katiba na Sheria.
Aidha, napenda
kutoa wito kwa Watumishi wa Umma na Sekta Binafsi kuwahudumia Wananchi wote kwa
usawa na kwa wakati ili kuleta ufanisi katika Utumishi wa Umma kwa kuzingatia
Sheria za Nchi.
Kwa upande wa
jamii ya Watanzania kwa ujumla natoa wito kwamba Utawala wa Sheria unamtaka mtu
binafsi, taasisi za Umma, taasisi za Kitaifa, na Sekta Binafsi kuheshimu misingi yote ya Utawala Bora, kama
ilivyobainishwa na kauli mbiu ya maadhimisho haya kwamba “Utawala wa Sheria Ndio Nguzo Kuu
ya Utawala Bora.”
Baada ya kusema
hayo, kwa heshima na taadhima natamka kuwa; Kongamano la wadau kuadhimisha
Miaka 50 ya ‘Ombudsman,’ sasa
limefunguliwa rasmi.
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment