Tamasha kubwa la ngoma za jadi la
Tulia litakalojumuisha zaidi ya vikundi vya ngoma 84 kutoka wilaya za Rungwe,
Busokelo na Kyela linatarajiwa kufanyika tarehe 7 hadi 8 ya mwezi huu wa kumi
katika viwanja vya Tandale wilayani Tukuyu.
Tamasha hilo ambalo linafanyika kwa
mara ya kwanza, litajumuisha zaidi ya ngoma za aina tisa huku baadhi ya ngoma
zitakazoshiriki ni pamoja na Ipenenga, Ingo’ma na Maghosi.
Akizungumzia tamasha hilo, Naibu Spika
wa Bunge na mwanzilishi wa tamasha hilo, Dkt. Tulia Ackson amesema lengo la
tamasha hilo ni kukuza na kuendeleza tamaduni hasa za ngoma za asili.
‘Ngoma za asili zina sehemu kubwa
katika utamaduni wetu, na ndio maana ni muhimu sana kama taifa tutakajikita
katika kuhakikisha zinatambulika na pia zinaendelezwa’ alisema Dkt.Tulia.
Akielezea zaidi kuhusu ngoma hizo Dkt Tulia
alisema lengo la tamasha la ngoma za jadi ni kuzifanya ngoma hizo zijulikane,
na pia kuzipa umuhimu katika jamii na hivyo kuzifanya zisipotee.
‘Tamasha pia litatoa fursa ya kiuchumi
kwa vijana watakaoshiriki tamasha hilo kwa wao kuanza kuzitazama ngoma kama
chanzo cha kujipatia kipato’ alisema Dkt. Tulia.
Mashindano hayo yaliyoanza katika
ngazi ya kijiji, kata, halmashauri na kanda, huku jumla ya vijiji 393
vikichuana kupata fursa ya kushiriki katika kilele cha matamasha hayo,
yatahudhuriwa wageni mbalimbali kama mabalozi kutoka nchi mbalimbali pamoja na wakurugenzi
na wawakilishi kutoka makampuni mbalimbali.
Mshindi wa kwanza wa mashindano hayo
atarekodiwa albamu ya nyimbo zake kwenye DVD, pamoja na ufadhili wa kusomeshwa
katika chuo cha Sanaa cha Bagamoyo.
Mshindi wa pili atapata mashine ya
kusaga na watatu atapata zawadi ya bodaboda.
No comments:
Post a Comment