Habari za Punde

Mama ashikwa na Gongo pamoja na Bangi, Wete Pemba

Hassan Khamis, Pemba

JESHI la Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba, linamshikilia mama wa miaka (44) baada ya kukamatwa na lita 66. 5 za ulevi wa kienyeji aina ya gongo na bangi nyongo 61 pamoja na furushi moja kijiji cha Bungala Wilaya ya Wete Mkoani humo.

Kaimu kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, ambae pia ni Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Issa Juma Suleiman amemtaja mama huyo kua ni Rehema Mikwaba Mabanga mkaazi wa Bungala Wete.

Ameongeza kuwa Septemba 27, mwaka huu majira ya saa 7:15 mchana kijijini hapo, mama huyo alipatikana na madumu matatu yenye ujazo wa lita 20 kila moja, na chupa moja ya drop yenye ujazo wa lita moja na nusu ndani yake ikiwa na ulevi wa kienyeji aina ya gongo.

Kamanda Issa amefafanua, mara baada ya askari kufika nyumbani kwa mama huyo, wakiongozwa na sheha wa shehia ya Kinyasini na kufanikiwa kukamata gongo hiyo, waliendelea na upekuzi na walifanikiwa pia kupata nyongo 61 pamoja na furushi moja la bhangi.

Alisema waligundua madawa hayo yakiwa yamehifadhiwa katika mfuko wa plastiki uliokuwepo ndani ya nyumba ya mama huyo.

Kamanda Issa alifafanua kuwa, askari walipata taarifa kutoka kwa raia wema, kuhusu taarifa za mama huyo kujishughulisha na biashara ya madawa ya kulevya na pombe za kienyeji na kuamua kumuwekea mtego ambao ulifanikiwa.

“Ni taarifa za raia weme ndio ambazo zilitusaidia sisi kumkamata mama huyu, na hivi ndio ambavyo huwa tunawataka wananchi washirikiane na Jeshi letu kwa ajili ya kufichua uhalifu’’,alifafanua.

Ametoa wito kwa wananchi kushirikiana na jeshi la Polisi ili kupinga biashara ya madawa ya kulevya na kutoa taarifa polisi ili kuwafichua wale wote wanaojishughulisha na biashara haramu ya madawa ya kulevya.


Hata hivyo alisema kuwa mama huyo anatarajiwa kufikishwa mahakani mara tu upelelezi wa shauri lake utakapokamilika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.