STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 22.10.2016
WIZARA ya Afya imeeleza miongoni mwa juhudi zake
inazoendelea kuzichukua katika kuhakikisha sekta hiyo inaimarika ni pamoja na
kuwapeleka wataalamu wake wa fani mbali mbali masomoni ili kuendelea kujenga
uwezo na kuelekea kwenye kujitegemea.
Hayo yameelezwa na
uongozi wa Wizara hiyo, huko Ikulu mjini
Zanzibar katika kikao maalum kati ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza
la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein na uongozi wa Wizara hiyo ilipokuwa
ikiwasilisha Taarifa yake ya Utekelezaji
wa Mpango Kazi wa Wizara kwa kipindi cha
Julai hadi Septemba katika Bajeti ya mwaka 2016-2017.
Katika maelezo yake, Waziri
wa Wizara hiyo Mahmod Thabit Kombo alisema kuwa Wizara bado inaendelea kupata
mafanikio makubwa katika kuendeleza miundombinu yake hasa katika hospitali mpya
ya Abdalla Mzee na kuweka vifaa vipya na vya maabara.
Aidha, upanuzi wa
hospitali ya Mnazi Mmoja katika wodi ya watoto na kina mama pamoja na kuweka
vifaa vipya na vya kisasa katika jengo hilo jipya.
Pia, hospitali ya
Kivunge imeendelea kuimarishwa kwa kujenga jengo jipya la wagonjwa wa nje
pamoja na ukarabati wa maabara.
Waziri Kombo alitumia
fursa hiyo kueleza majukumu Makuu ya Wizara hiyo ambapo pamoja na majukumu hayo
Wizara imezingatia Sera, Mipango na mikakari mbali mbali ya Kitaifa na
Kimataifa ikiwa ni pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030, Dira ya
Zanzibar 2020, Sera ya Afya 2011, Mpango Mkakati wa III wa Sekta ya Afya pamoja
na Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwak 2015-2020.
Uongozi huo pia,
ulizipongeza juhudi za Dk. Shein anazozichukua katika kuwapa maelekezo na
ushauri ambao unaendelea kuwasaidia katika utendaji wao wa kazi.
Katika suala zima la
upatikanaji wa dawa katika vituo vya afya, uongozi huo umezipongeza juhudi
zilizochukuliwa na Serikali katika kuhakisha Bohari yake kuu inazo dawa za
kutosha.
Uongozi huo pia,
ulieleza juhudi za makusudi zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara hiyo katika
uanzishwaji wa Bima ya Afya pamoja na hatua zilizofikiwa.
Mapema Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alizipongeza juhudi
zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara hiyo katika utoaji huduma ya afya kwa
wananchi hapa nchini.
Dk. Shein alieleza
haja ya kuendelea na utaratibu wa kuwapa mafunzo watendaji wa Wizara hiyo
katika kada mbali mbali kwa lengo la kuja kutoa huduma kwa wananchi huku
akisisitiza azma ya Serikali kupitia Wizara hiyo kuendelea kutoa huduma mbali
mbali za upasuaji ambazo zitapunguza gharama za kuwapeleka wagonjwa nje ya nchi.
Aidha, Dk. Shein
alisisitiza umuhimu wa kulipa kipaumbele suala zima la utafiti ndani ya Wizara
hiyo huku akisisitiza suala zima la uzalendo na kueleza kuwa utaratibu wa
kuwapeleka watendaji wa Serikali kufanya kazi Pemba sio adhabu bali ni taratibu
za kiutumishi.
Nae Katibu Mkuu wa
Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Abdulhamid Yahya Mzee, aliipongeza
Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango Kazi wake huku akisisitiza umhimu wa
mikutano hiyo kwa manufaa ya Serikali sambamba na upangaji mzuri wa huduma za
maendeleo endelevu.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment