|
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Kitalu Na. 8, Mtaa wa Luthuli
S.L.P 2643, DAR ES SALAAM
Simu: +255 22 2135747/8; 2137125; 2135222
Faksi: +255 22 2111281
Tovuti: www.chragg.go.tz
|
Oktoba 05, 2016
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Tamko la Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kulaani
mauaji ya watafiti watatu huko Iringa-Mvumi, Dodoma
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kuuwawa kwa watafiti watatu (3)
wakiwa kazini, tukio lililotokea Oktoba mosi mwaka huu katika kijiji cha
Iringa-Mvumi, Wilayani Chamwino, Mkoa wa Dodoma.
Tume inalaani vikali mauaji haya ya
kikatili ya watu wasiokuwa na hatia na yenye kuitia aibu nchi yetu. Aidha,
inaungana na watanzania wengine nchini kuwapa pole wafiwa na wote walioguswa na
msiba huu.
Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya
habari watafiti hao kutoka Chuo cha Utafiti wa Udongo na Maendeleo ya Ardhi cha
Selian, Arusha wakiwa kijijini hapo kukusanya sampuli za udongo kwa ajili ya
utafiti walivamiwa na kundi la wanakijiji na kushambuliwa kwa mapanga na silaha
za jadi na kisha kuchomwa moto kwa imani kwamba eti walikuwa wanyonya damu.
Haki ya kuishi kama
zilivyo haki nyingine, inalindwa na sheria na hakuna mtu anayepaswa kuporwa
haki hii ya msingi kiholela. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 14, kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata
kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria.
Pia Mikataba mbalimbali
ya kimataifa na kikanda ambayo Tanzania imeridhia inatoa ulinzi juu ya haki ya
mtu kuishi. Baadhi ya Mikataba hiyo ni: Azimio la Kimataifa la Haki za
Binadamu la 1948 (Kifungu cha 3) na Mkataba wa
Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa 1966 (Kifungu cha 6) vinavyoeleza
kuwa kila mtu anayo haki ya asili ya kuishi, inayolindwa kisheria na hakuna
atakayenyimwa haki hii ya msingi kiholela.
Hivyo kuuwawa kwa watafiti hao
wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao kwa taifa ni kitendo kinachopaswa kulaaniwa
vikali na kila mwananchi anayethamini uhai na kuheshimu haki za binadamu.
Kumbukumbu zinaonyesha kuwa matukio
ya wananchi kujichukulia sheria mikononi mwao ni jambo linalojirudiarudia na
limekuwa likisababisha uvunjifu wa haki za binadamu na madhara makubwa kwa
jamii, hususan kwa wanawake na watoto.
Hivyo basi, Tume ya Haki za Binadamu
na Utawala Bora:
- Inaiomba Serikali kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali kudhibiti mauaji ya kiholela nchini na kulipatia ufumbuzi
tatizo la wananchi kutoheshimu sheria na kujichukulia sheria mkononi.
- Inawakumbusha wananchi kuwa vitendo vya ukatili,
mauaji, na matendo yote yanayokiuka Sheria yanayofanywa na raia wasio wema
ni ukiukwaji wa Sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala wa sheira; Hivyo
Tume inakemea matendo haya na kutaka yapigwe vita.
- Inawataka wananchi kuheshimu mamlaka zilizopo katika
maeneo yao na ngazi mbalimbali wakitambua kuwa ndio wenye dhamana juu ya
masuala mbalimbali ya kiutendaji katika maeneo husika.
- Inapendekeza Kamati za Ulinzi na Usalama katika
ngazi za vijiji, vitongoji na kata, wakiwemo watendaji watimize wajibu wao
ili kuepuka madhara kama haya kujirudia au kutokea katika maeneo mengine.
- Pia inapendekeza watendaji wa taasisi za Serikali na
binafsi wajitahidi kuzingatia utaratibu wa kutoa taarifa mapema,
ikiwezekana kwa maandishi kwenye ngazi mbalimbali za uongozi katika maeneo
wanayokwenda kufanyia kazi. Aidha, wazingatie utamaduni wa kujitambulisha
kwa viongozi wa ngazi za chini na kuomba kupatiwa watu wa kuambatana nao
katika kazi zao wawapo katika maeneo hayo.
- Vilevile inaona ipo haja ya elimu zaidi kutolewa kwa
umma juu ya masuala ya haki za binadmu na wajibu, sheria, utawala bora na
uraia.
- Inalipongeza Jeshi la Polisi kwa hatua za kuwakamata
watuhumiwa haraka. Aidha, inaliomba jeshi hilo lifanye uchunguzi wa kina
na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria wote watakaobainika kuwa
walihusika na mauaji na uharibifu wa mali uliotokea katika tukio hili.
- Mwisho, Tume inatoa wito kwa wananchi wa kijiji cha
Iringa-Mvumi na maeneo mengine kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi
katika kuhakikisha wote waliohusika na unyama huu wanakamatwa na
kufikishwa katika vyombo husika ili sheria ichukue mkondo wake.
Imetolewa
na:
(SIGNED)
Mhe. Iddi
Ramadhani Mapuri
Makamu Mwenyekiti
TUME YA
HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Oktoba 5,
2016
No comments:
Post a Comment