Habari za Punde

Mama Mwanamwema Amewataka Viongozi na Wananchi Mkoa wa Kusini Unguja Kuitumia Vyema Ardhi.

MKE wa Rais wa  Zanzibar Mama Mwanamwema Shein amewataka viongozi na wananchi wa Mkoa wa Kusini Unguja  kuitumia vyema ardhi ndogo iliyopo kwa kuzingatia Sheria ya Mipango Miji na Vijiji, sambamba na kujiepusha na migogoro ya ardhi ambayo husababisha uhasama na kuhatarisha amani.

Mama Shein aliyasema hayo leo kwa nyakati tofauti wakati akizungumza na akinamama, viongozi na wanachama wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT) wa Wilaya ya Kusini na Wilaya ya Kati Unguja katika ziara yake yenye lengo la kuwasalimia na kuwashukuru kwa kuendelea kuiunga mkono CCM, na kupelekea kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi uliopita.

Akiwa katika ukumbi wa Hoteli ya Karafuu, Michamvi Mkoa wa Kusini Unguja, Mama Shein alitoa nasaha zake kwa viongozi wa Mkoa na Wilaya pamoja na wananchi wa Mkoa huo kushirikiana katika kuihami misitu na miti ya asili ambayo ni muhimu katika kuyahifazi mazingira ambayo ni hazina kwa vizazi vilivyopo na vijavyo.

Mama Shein, ambaye katika ziara yake hiyo amefuatana na viongozi mbali mbali wakiwemo Wabunge na Wawakilishi wa Viti Maalum pamoja na wake wa viongozi wakiwemo Wabunge na Wawakilishi, alitumia fursa hiyo kusisitiza suala zima la amani na kueleza kuwa bila ya amani hakuna watakaokwenda kondeni, watakaojishughulisha na kilimo cha mwani, uvuvi wala utalii na kueleza kuwa watakaoathirika zaidi ni akinamama na watoto.

Hivyo, aliwataka viongozi na wananchi wa Mkoa huo wasichoke kuwakumbusha vijana wao umuhimu wa kuitunza amani na kujiepusha na vitendo vyote vya uvunjaji wa sheria na kuhatarisha amani kwani kuvunja amani ni mara moja lakini kuirudisha huchukua muda.

Mapema Mama Asha Balozi, Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwaeleza akinamama hao wa Jumuiya hiyo kuwachagua viongozi wenye uchungu na chama, nchi na wanachama wenzao katika uchaguzi wa Chama na Jumuiya zake hapo mwakani.  

Mama Asha alitumia fursa hiyo kuwataka akinamama wenzake kuwa karibu na watoto wao ili kuepuka vitendo viovu wanavyoweza kufanyiwa hasa vitendo vya ubakaji.

Nae Mama Fatma Karume aliwahamisisha wanawake kuchukua fomu za kugombania nafasi mbali mbali za uongozi ndani ya chama cha CCM bila ya kuogopa pingamizi za kutowapa nafasi waliokuwa hawakusoma na kueleza kuwa wengi wao waliofanya Mapinduzi na kuipa uhuru Zanzibar walikuwa hawana elimu hivyo hicho sio kisingizio.

Alieleza kusikitishwa na vijana ambao hupewa madaraka makubwa ndani ya serikali na kusahau wajibu na majukumu yao na badala yake kufanya hilba kwa lengo la kujineemesha wao wenyewe na pale wanapoondoka madarakani hukimbilia katika vyama vya upinzani.

Aliwaomba wale wote walioteuliwa na Dk. Shein kushika nyadhifa mbali mbali za uongozi kutomuangusha hasa wanawake ambao katika uongozi wake amewapa nafasi nyingi serikalini.

Katika risala yao wanachama wa Jumuiya ya UWT Wilaya ya Kusini Unguja , walitoa shukurani kwa Serikali kwa kuwapelekea mradi wa JOCDO kwa madhumuni ya kusaidia vikundi mbali mbali ili wajikwamue na hali ngumu ya maisha ambapo pia, UWT Wilaya imeanzisha vikundi vya Jumuiya katika Matawi kwa lengo hilo la kujikwamua kimaisha.

Aidha, walieleza kutokuwa nyuma katika kukiimarisha chama na kuleta maendeleo endelevu na kueleza juhudi walizozichukua katika kuhakikisha CCM inapata ushindi na kumuahidi Mama Shein kuwa katika Wilaya yao upinzani hautokuwa na nafasi milele.  

Walieleza kusikitishwa na suala zima la unyanyasaji wanawake na watoto huku wakitumia fursa hiyo  kumpongeza Dk. Shein kwa kuendelea kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Wakati huo huo, akiwa katika ukumbi wa  Kituo cha Elimu kiliopo Dunga, Wilaya ya Kati Unguja, Mama Shein aliwahimiza akinamama na vijana umuhimu wa kuanzisha na kuviendeleza vikundi vya maendeleo ili kujiimarisha kiuchumi.

Mama Shein aliwaahidi akinamama hao kuwa wake wa viongozi pamoja na waheshimiwa wabunge na wawakilisgi wataendelea kushirikiana na vikundi vya akinamama na vijana katika jitihada zao za kujiletea maendeleo.

Aidha, Mama Shein aliwataka wanajumuiya ya UWT kujitahidi kuzitumia vyema fursa ambazo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba inazitoa kwao kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi.


Nao wanajumuiya ya UWT Wilaya ya Kati waliahidi kuendelea kumuunga mkono Mama Shein katika juhudi zake hizo sambamba na kuendelea kukiunga mkono chama cha Mapinduzi ili kiendelee kushika hatamu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.