Bi. Lilian Mukasa ,Afisa wa Uwakilishi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa ambaye pia anahusika na masuala ya Uchaguzi ( Election Officer) akiwapigia kura wagombea ambao wameomba kuwa wajumbe wa Tume ya Kimataifa ya Sheria. Nyuma anaonekana Mgombea wa Tanzania, Profesa Chris Maina Peter ambaye alishindana na wagombea wengine 13 kutoka Afrika ambapo walitakiwa nane kati ya hao 13. Afisa Lilian kwa nafasi yake kama Election Officer alikuwa na jukumu kubwa la kusaidia na kufanikisha mgombea wa Tanzania anapata kura za kutosha.
Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Katika Umoja wa Mataifa Balozi Tuvako Manongi akiwa na Profesa Chris Maina Peter aliyesimama pamoja na baadhi ya Maofisa wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania mara baada ya kutangazwa kwa majina ya wagombea 34 ambao walishinda kwa kupigiwa kura ya siri na Wajumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuwa wajumbe wa Tume ya Kimataifa ya Sheria ( ILC) katika uchaguzi uliofanyika jana ( alhamisi) hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.
Na Mwandishi Maalum, New York
Profesa Chris Maina Peter , kutoka
Tanzania, ni kati ya wagombea
nane miongoni mwa wagombea 13 kutoka
Afrika, ambao jana ( alhamisi
) Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliwapiga kura ya siri ya
kuwachagua kuwa wajumbe wa Tume ya Kimataifa kuhusu masuala ya Sheria ( International Law Commission).
Ushindi
wa Profesa Maina ambaye ataitumikia Tume
hiyo wa miaka mingine mitano
kuanzia Januari 2017, pamoja na juhudi
zake binafsi za kujinadi, kujitangaza, kwa wajumbe 193 wa Baraza Kuu la Umoja wa Matifa, na akisheheni sifa na weledi mkubwa katika sheria za kimataifa.
Ushindi wake umechangiwa zaidi na kazi kubwa iliyofanywa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika
Umoja wa Mataifa Balozi Tuvako Manongi kwa kushirikiana na Maafisa wake ambao
walifanya kazi kubwa ya kumkampenia na
kumwombea kura.
Ingawa Profesa Maina anaingia kama
mtu binafsi katika kazi za
ILC anabeba jina na kuipeperusha bendera ya
Tanzania katika Tume hiyo. Na
kwa sababu hiyo, ushiriki wa
Serikali katika kupendekeza jina lake
pamoja na kumsaidia katika kampeni
ilikuwa ni sehemu kubwa ya
kufanikisha hatua hiyo muhimu ya kuendelea tena kuitumikia Tume
kwa pindi cha pili cha miaka mitano.
Katika
uchaguzi huo wa jana ambao
ulikuwa na ushindani mkubwa huku ukishuhudia
nchi kubwa kama Ufaransa
ikishindwa kufurukuta. Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitakiwa kuwachagua wajumbe
34 watakaohudumu katika
Tume hiyo kwa mgawanyo wa wajumbe
nane kutoka Afrika, wajumbe
Saba kutoka Asia-Pacific , wajumbe
wanne kutoka Ulaya ya Mashariki,
wajumbe saba kutoka Amerika ya
Kusini na Visiwa vya Caribbean
na wajumbe nane kutoka
nchi za Ulaya Magharibi na nchi
nyingine.
Baada ya
upigaji huo wa kura ya sira, washindi waliotangazwa kwa
upande wa Afrika, waliochaguliwa ni Chris Maina Peter(Tanzania) Ahmed Laraba
(Algeria), Tacouba Cissé (Ivory Coast), Dire D. Tladi (South Africa), Hussein
A. Hassouna (Misri), S. Amos Wako (Kenya), Charles C. Jalloh (Sierra Leone) na
Hassan Ouazzani Chahdi (Morocco).
Kutoka
Asia-Pacific waliochaguliwa
ni Ali bin Fetais Al-Marri (Qatar),
Mahmoud Daifallah Hmoud (Jordan), Huikang Huang (China), Shinya Murase (Japan),
Hong Thao Nguyen (Vietnam), Ki Gab Park (Jamhuri ya Korea ) na Aniruddha Rajput
(India).
Waliochaguliwa kutoka
Amerika ya Kusini na Caribbean ni
Carlos Argüello Gómez (Nicaragua), Juan Manuel Gómez-Robledo (Mexico),
Claudio Grossman Guiloff (Chile), Juan Jose Ruda Santolaria, (Peru), Gilberto
Vergne Saboia (Brazil), Eduardo Valencia -Ospina (Colombia) na Marcelo
Vázquez-Bermúdez (Ecuador).
Wajumbe
kutoka Ulaya ya Mashariki waliochaguliwa ni
Bogdan Aurescu (Romania), Kirumi Anatolyevitch Kolodkin, (Shirikisho la
Urusi), Ernest Petric (Slovenia) na Pavel Šturma (Jamhuri ya Czech).
Kwa
upande wa Ulaya Magharibi na nchi nyingine
waliopita ni , Concepción Escobar Hernández (Hispania), Patrícia Galvão
Teles (Portugal), Marja Lehto (Finland), Sean David Murphy (United States),
Georg Nolte (Ujerumani), Nilufer Oral (Uturuki), Agosti Reinisch (Austria) na
Michael Wood (United Kingdom)
Majukumu ya
Tume ya Kimataifa kuhusu sheria pamoja na mambo mengine, ni kukuza na kuendeleza sheria za kimataifa, kutoa ushauri wa kitafiti kuhusu sheria
mbalimbali, kupitia masuala yahusuyo sheria na
mikataba ya kimataifa.
No comments:
Post a Comment