STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 30.12.2016
![---](file:///C:/Users/user/AppData/Local/Temp/msohtmlclip1/01/clip_image004.gif)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj
Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa si vyema misikiti kuwa chanzo cha mizozo,
mivutano na migongano na badala yake iwe sehemu ya kuwaunganisha Waislamu kwani
hayo ndio mafunzo ya Mtume Muhammad (S.A.W).
Alhajj Dk. Shein
aliyasema hayo leo mara baada ya ufunguzi wa masjid Muhammad (S.A.W) uliopo Fujoni
Mzambarauni, Wilaya ya Kaskazini B, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Akitoa nasaha zake kwa
waumini wa Kiislamu wa Fujoni na vijiji vya karibu, Alhajj Dk. Shein aliwasisitiza
waumini hao kwamba kamwe haitakuwa jambo jema msikiti kuwa chanzo cha mizozo na
migongano kwani msikiti ni nyumba ya Mwenyezi Mungu.
Alhajj Dk. Shein
aliwataka waumini hao kuufanya msikiti huo kuwa sababu ya watu kuzidi kuwa
wamoja na kushikamana pamoja na kuendeleza masuala ya dini huku akiwataka
kutafuta uongozi madhubuti wa msikiti huo.
Katika nasaha zake
hizo, Alhajj Dk. Shein alieleza kusikitishwa kwake na tukio lililofanywa na baadhi ya waumini wa Kiislamu hivi karibuni
huko kisiwani Pemba la kuchoma moto msikiti, kuiba mashine ya kupandishia maji
sambamba na baadhi ya waumini kubaguana katika baadhi ya misikiti.
Aidha,, Alhaj Dk.
Shein alisema kuwa katika historia ya Uislamu, misikiti imetoa mchango mkubwa
katika kuuendeleza Uislamu kama chemu chemu muhimu ya elimu katika fani mbali
mbali za dini.
Vile vile, Alhajj Dk.
Shein alisema kuwa misikiti ina mchango muhimu katika kuwaunganisha wanajamii
wanaosali pamoja na huwapelekea kujuana na kushirikiana katika masuala mbali
mbali na kusisitiza umuhimu wa kuitunza misikiti ukiwemo msikiti huo mpya ambao
una sifa zote.
Aliwaeleza Waumini hao
kuwa ni jukumu lao wakiwa wazazi na walezi kuwalea watoto katika maadili mema
na mafundisho ya dini na kusisitiza kuwa ulinzi wa watoto ni pamoja na kuwapa
elimu, ili wajue mazuri na mabaya sambamba na kuwapatia hifadhi ya maisha yao
kwa kuwaepusha na vitendo vya udhalilishaji na unjanjasaji.
Akiendeleza nasaha
zake, Alhaj Dk. Shein alisema kuwa kuwapatia
watoto elimu ni jukumu la kila mzazi, hivyo wazazi pia wanapaswa kuwa
ushirikiano walimu kwa kila hali ili wapate moyo wa kuitekeleza kazi yao ambayo
inajulikana kuwa ni ngumu.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein aliwataka waumini wa dini ya Kiislamu kuyatumia mafunzo ya Bwana Mtume
(S.A.W) ili kuiepusha jamii na mifarakano kwa kuimarisha umoja, kwani umoja ni
nguvu.
Alhaj Dk. Shein
alisema kwua kila mmoja kwa nafasi yake ajue ana wajibu wa kuhakikisha jamii
inakuwa salama dhidi ya vitendo vya udhalilishaji wa watoto na kinamama pamoja
na vitendo vyote vya uhalifu ili jamii iendelee kuishi kwa mani.
“ Tushirikiane katika
kuvikabili vitendo vinavyosababishwa na kumongonyoka kwa maadili, malezi na
utamaduni wetu tulioachiwa na wazee wetu”,alisema Alhajj Dk. Shein.
Aidha, Alhaj Dk. Shein
aliwataka Waumini wa Dini ya Kiislamu, kila wanapopata wasaa waendelee
kukumbushana umihumu wa kujiepusha na makatazo ya Mwenyezi Mungu ili kujikinga
na adhabu zake na kuyafanya mambo yatakayowapa faida hapa duniani na huko
akhera waendako.
Katika hotuba yake kwa
Waumini hao, Alhajj Dk. Shein aliwaahdi kwamba maombi yao yamepokewa na
yatafanyiwa kazi na kuwataka kuendelea kuwa na subira kwa yale mambo ambayo
yanaweza kuchelewa katika utekelezaji kwa mashirikiano ya Mwakilishi wa Jimbo
hilo Balozi Seif Ali Idd..
Alhaj Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu wale wote walioshiriki katika
ujenzi wa msikiti huo azidi kuwafunguliwa milango ya riziki bna watilie baraka
katika kufanya shughuli zao.
Nae Makamu wa Pili wa
Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Mahonda Alhajj Balozi Seif Ali Idd, alieleza juhudi
zilizochukuliwa katika kuhakikisha msfadhili wa ujenzi wa msikiti huo
anapatikana ikiwa ni pamoja na kutumiza ahadi yake ya kutafuta mfadhili wa
msikiti huo.
Alhajj Seif Idd
aliwaeleza wananchi wa Fujoni kuwa kila muumini wa dini ya Kiislamu ana haki ya
kusali msikiti huo tena bila ya kuingiza ubaguzi wa aina yeyote zikiwemo
itikadi za kisiasa kwani hiyo ni nyumba ya Mwenyezi Mungu kila mmoja ana haki
kuitumia.
Nao wananchi wa Shehia
ya Fujoni katika risala yao walieleza
furaha yao kwa kujengewa msikiti huo mpya ambapo walieleza kuwa hapo
kabla msikiti uliokuwepo ulikuwa haukidhi haja kutokana na udogo wake, uchakavu
sambamba na kwenda masafa marefu kufuata misikiti kwa ajili ya sala za Idd na
Ijumaa.
Katika risala hiyo
iliyosomwa na Ustadhi Salmin Mbarouk, wananchi hao walitumia fursa hiyo
kumpongeza na kumshukuru Balozi Seif kwa kuchukua juhudi katika kutekeleza
ahadi yake ya kutafuta mfadhili wa ujenzi wa msikiti huo na kumpongeza mfadhili
huyo ambapo pia walitumia fursa hiyo kutoa maombi yao kwa Rais.
Mapema Sheikh Othman
Maalim akitoa mawaidha katika ufunguzi huo alieleza umuhimu kwa waislamu
kujenga misikiti sambamba na kuendeleza utamaduni wa kutoa sadaka kwa lengo la
kupata fadhjila za Mwenyezi Mungu na kufuata mienendo ya Mtume Muhammad
(S.A.W).
Sheikh Othman Maalim
alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Mfadhili wa msikiti huo Ali Buwardy
pamoja na msimamizi wa ujenzi wa msikiti huo Bwana Yakoub Othman huku akieleza
jinsi Allah (SW) anavyochukia wale wanaotumia kinyume fedha za ujenzi wa
misikiti.
Nae Sheikh Fadhil
Soraga alisisitiza umuhimu wa waislamu kujenga misikiti pamoja na kuepuka
mifarakano na migogoro katika kuiendesha msikiti hatua ambayo haileti tija kwa
waislamu na uislamu wenyewe huku akieleza haja kwa waumini kuwa na tabia njema itakayompwekesha Allah (S.W)
Viongozi mbali mbali
wa Serikali, viongozi wa dini ya kiislamu, wananchi na wageni kutoka ndani na
nje ya Zanzibar walihudhuria katika ufunguzi huo wa masjid Muhammad (S.A.W).
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment