Na Haji Nassor, Pemba
‘’KUANZIA umri wa miaka 10
hadi 19, yote ni hatari kwa mtoto wa kike kupata ujauzito kitaalamu.
Wataalamu
wa afya ya uzazi, wanasema kwa ujumla kuanzia siku ya mwanzo mimba inapotunga
hadi kufika siku ya kuzaliwa, huzungurukwa na matatizo, lakini kwa wale wenye
umri ni mdogo tatizo huwa kubwa zaidi.
Elimu
ya afya ya uzazi, imekuwa ikitolewa hata kwenye vituo vya afya na kliniki, ili
kuisadia jamii kujua athari za mimba za umri mdogo, lakini bado tatizo
linaendelea kuwepo.
Makala
haya ilikutana na daktari wa hospitali ya wilaya ya Chake Chake, Zeana
Abdull-aziz Ibrahim, ambae anasema mimba katika umri mdogo sasa ni tatizo
kubwa.
Anasema
kwa kawaida, huzigawa mimba katika misimu mitatu; miezi mitatu ya mwanzo, kati
na mwisho ambapo kila hatua huzunguruka tofauti na hatua nyengine.
Anasema
kwa mtu aliebeba ujauzito akiwa na umri
baina ya miaka 10 hadi 19, anaweza kushambuliwa na matatizo mbali mbali ambapo
kwa miezi mitatu ya mwanzo (first trimester) kuna mlolongo wa magonjwa yanayoweza
kumpata mama mjamzito.
Kwa
walio chini ya umri wa kitaalamu wa kuweza kubebea ujauzito na kuzaa, yaani
kuanzia miaka 20 na kuendelea, wanaweza kupata magonjwa ya kuambukiza.
Kwa
mfano kwa mtoto aliebeba mimba chini ya umri, anaweza kushambuliwa na wadudu
kama bacteria, fangasi na virusi ambao
wanashambuliwa njia za mkojo.
Mtaalamu
huyu anasema hata kinga ya mwili kwa mtu aliebeba ujauzito akiwa na umri mdogo
hupotea, ambapo hapo magonjwa kama malaria na hata Ukimwi huwa ni rahisi kwake,
tofauti na mwanamke aliepata ujauzito kwa umri unaoshauriwa kitaalamu.
Lakini
hata magonjwa ya zinaa, kama vile Ukimwi, kaswende hujitokeza kwa mjamzito
aliebeba mimba akiwa hajafikia umri, sambamba na mtoto kuwa na ukuaji usioridhisha.
Upungufu
wa damu kwa watoto wanaobeba mimba wakiwa na umri mdogo huwa la kawaida na hapo
mama mjamzito anaweza kupoteza maisha ndani ya wiki 12 za kwanza.
Kwenye
hatua ya pili ambazo ni kuelekea wiki 24, mama mjamzito ambae ameshabeba mimba
kabla ya mwili kuruhusu, damu kwa kipindi hiki huwa baina ya asilimia 9 hadi 7,
na sehumu ya pili huwa baina ya asailimia kati ya 7 hadi 6 na mwisho ‘sear via’
ambapo mjamzito huhitaji masaada wa damu.
Kwenye
miezi mitatu ya mwishio, mama mjamzito ambae ameolewa na kupata ujauzito akiwa
mdogo, hukabiliwa na ugonjwa wa presha
wa mara kwa mara.
Zile
wiki za kuanzia za 28 hadi 39, ambapo nguvu ya msukumo wa damu kwa kawaida huwa
baina ya mwendo wa 120 hadi 140, lakini kutokana na umri wake mdogo wa kubeba
mimba, hushuka hadi kufikia 90.
Kwa
walio chini ya umri wa kuweza kuzaa, mifupa ya uzazi hukumbana na adhabu kubwa
wakati mtu anapojifungua, na ndio maana kwa hawa ambao umri wao ni mdogo wakati
huo wa huweza hata kupoteza maisha.
Kwa
hospitali ya Chake Chake, uchunguzi umeonesha kuwa, wastani wa wasichana walio chini
ya umri wapatao 18, kila mwezi hulazimika kuongezewa njia ya uzazi ili waweze
kujifungua kutokana na mifupa yao kutopevuka.
Hospitali
hiyo ambayo huchukua wajawazito kutoka
wilaya ya Mkoani na Chake Chake, wastani wa mama wajawazito 300 kwa mwezi
hupokelewa, ambapo kati yao saba ambao ni chini ya miaka 18 hufanyiwa upasuaji.
Wakati
ni wanne walio chini ya umri na kujifungua kwa njia za kawaida, ingawa wapo
wengine 10 ambao njia zao kuchanwa ili kuongezewa nguvu.
Kubwa
zaidi ambalo hujitokeza kwa waliobeba mimba kabla ya kufikia umri, ni kukaa na
uchungu zaidi ya siku mbili jambo ambalo kwati huo huwezi kujitokeza hata
michubuko mtoto akizaliwa.
Na
wakati mwengine hukumbana na maradhi ya kukojoa mfululizo au haja ndogo na
kubwa zote kutoka seheumu ya siri ya mbele bila ya kizuizi.
Aidha
kwa watoto wanaoolewa na kisha kubeba ujauzito, pia wanaweza kukosa watoto
wenye uzito unaotakiwa, (normal weight) ambao ni kuanzia kilo 2.5, 3.0 ingawa
wengine wao huzaa watoto wenye uzito baina ya kilo 1.5, kilo 2.4 na kilo 2.0
Msichana
Sanura (17) ambae sio lake rasmi, wa Uwanadani wilaya ya Chake Chake ambae alijifungua
mwaka jana mtoto wake akiwa na uzito wa kilo 1.8 anasema, alipata mimba hiyo
kabla ya kuolewa na alikaribia kufa wakati wa kujifungua.
Anasema
tokea miezi mitatu ya mwanzo, baada ya kujificha sana ili wazazi wake
wasifahamu, alishindwa na kuamua kumueleza dada yake.
Yeye
anasema alikuwa anaona ‘kizungu zungu’ kila wakati na kuanzia miezi mitatu ya
mwanzo hakumbuki siku aliokula chakula akashiba kutokana na mwili wake, kukosa
hamu ya kula.
“Niliacha
skuli na madrasa mwenyewe, na mimi nikawa mtu wa kulala saa 24, maana sikuwa
natamani kufanya lolote kutokana na mwili kukosa nguvu,” alisema.
Anasema
mwezi wa kujifungua ulipofika, matatizo mwilini mwake yaliongezeka, na kila
siku moja hakuwa na hakika kwamba atakutana na siku ya pili.
Aliamua
kukaa karibu na hospitali kuu ya Chake Chake, ili lolote litakalojitokeza awe
karibu, ambapo siku mbili kabla ya kujifungua alipelekewa hospitali.
“Mimi
niliumwa na uchungu nadhani siku tatu na kisha sikuwa na nguvu ndipo madaktari
walipoamua kuniongezea damu hadi
nilipomzaa mwanangu,” anasema.
Ingawa
mwanawe ameshafariki miezi mitatu iliopita, lakini anasema anakumbuka mimba
hiyo jinsi ilivyomtesa na kisha mwanamme kuamua kuhakama Pemba hadi leo.
Mama
wa msichana huyu, anasema mwanawe wakati wa ujauzito wake aliwahi kutiwa damu
mara mbili, mara moja kabla ya wao kugundua na mara nyengine wakati akitaka
kujifungua.
Mkuu
wa mkoa wa kaskazini Pemba, Omar Khamis Othman, anasema kama wazazi hawakuwa makini wanaweza
kukosa watoto wao wakati wanapojifungua,
kutokana na tabia yao ya kuwaozesha waume mapema.
Mwananchi
Amini Haji Makame, anasema kama jamii haikuweka mikakati vifo vya watoto wa kike vitakuwa
vinaendelea.
Sheikh
Mohamed Adam wa Mkoani, anasema waislamu wamekatazwa kujitia katika maagamizi
kwa mikono yao, likiwemo la ndoa za utotoni.
“Kama ikionekana ndoa ikifungwa hata mtu mwenye umri mkubwa, basi uislamu umekataza aina hiyo, maana ndani yake mnamatatizo ya kiafya’’,alifafanua.
Uchunguuzi
umebaini, wapo watoto wa kike 240 wameripotiwa kukatishwa haki yao ya elimu kwa
kuolewa, ambapo idadi hiyo ni ile iliopatikana katika taasisi mbali mbali na
kuanzia 2013-2015.
Azimio
la Umoja wa Mataifa la kupunguza aina zote za udhalilishaji kwa wanawake
(CEDAW) haliruhusu watoto wenye umri wa chini ya miaka 18 kuolewa.
Kila
mwaka, watoto wa kike milioni 7.3 dunaini kote walio chini ya umri wa miaka 18, hushika mimba, hii
ni kwa mujibu wa ripoti Shirika la Idadi ya watu Duniani ya mwaka 2013.
No comments:
Post a Comment