Habari za Punde

Katibu Mkuu Kiongozi Zanzibar Dk Abdulhamid Yahya Azungumza na Waandishi wa Zanzibar leo.

Katibu Mkuu Kiongozi Dk Abdulhamid Yahya Mzee akizungumza na waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vilioko Zanzibar akitowa Taarifa ya Ukaguzi wa Mkaguzi Mkuu wa Serikali ya Zanzibar. kuhusiana na uchuguzi waliofanya, kushoto Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Ikulu Zanzibar Ndg Hassan Khatib. mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar.
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                             24.04.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika kuimarisha utendaji Serikalini na kukuza Utawala Bora alimuagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu (CAG) kufanya ukaguzi maalum wa matumizi ya fedha za mishahara katika Wizara na Taasissi za Serikali na kubainika mambo mbali mbali ambayo Serikali imeahidi kuyachukulia hatua.

Akitoa taarifa kwa Waandishi wa Habari, Ikulu mjini Zanzibar, Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisema kuwa baada ya Rais kukabidhiwa ripoti hiyo, alisema kuwa Rais Dk. Shein ameagiza wajuulishwe wananchi juu ya mambo yaliobainika katika ukaguzi huo na hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali.

Dk. Abdulhamid alisema kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali alifanya ukaguzi huo maalum kuanzia mwezi wa Juni, 2016 hadi Novemba, 2016 na kuwasilisha ripoti yake kwa Rais wa Zanzibar kama alivyoagizwa na kwa mujibu wa utaratibu wa kisheria.

Alisema kuwa katika ukaguzi maalum uliofanyika, mambo mbali mbali yalibainika ikiwa ni pamoja na kuwepo wka tofauti baina ya fedha zilizoingizwa kwa ajili ya mishahara na fedha halisi zilizotumika kulipwa mishahara hiyo katika baadhi ya taasisi za Serikali.

Jengine ni kubainika kwa watumishi ambao wamechukua likizo bila ya malipo ingawa bado wanaendelea kupokea mishahara, kubainika kwa watumishi ambao wameacha kazi au kustaafu lakini bado mishahara yao inaendelea kulipwa.

Aliongeza kuwa kutojitokeza kwa baadhi ya wafanyakazi katika zoezi la uhakiki na kushindwa kufika kuhakikiwa, kubainika kwa watumishi ambao wamefikia umri wa kustaafu kwa lazima lakini bado wanaendelea na utumishi wa umma na kulipwa pamoja na kubainika kwa watumishi ambao hawahudhurii kazini kwa muda mrefu na bado wanapokea mishahara.

Aidha, alisema kuwa  jambo jengine lililobainika ni kwa watumishi ambao hawawezi kufanya kazi kutokana na maradhi ya muda mferu lakini bado hawajastaafishwa kwa mujibu wa sheria na wanaendelea kulipwa, kubainika kwa fedha za mihshara zinazotumika kwa ajili ya matumizi mengine.

Pamoja na kubainika kwa wafanyakazi waliokwenda masomoni kwa muda mrefu na hawajarudi tena makazini lakini bado wanalipwa mishahara na Serikali.

Kufuatia hali hiyo, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisema kuwa pamoja na mambo mengine Serikali inafanya uchunguzi wa kina dhidi ya wale wote waliodaiwa kuchukua fedha za umma kinyume na utaratibu ili endapo itathibitika hatua za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa.

Alisema kuwa Serikali imeziagiza taasisi zinazohusika kusitisha mara moja malipo kwa wafanyakazi walioacha kazi, kustaafu au kuchukua likizo bila ya malipo lakini bado wanaendelea kulipwa mishahara na maslahi mengine.

Pia, Katibu Mkuu huyo wa Baraza la Mapinduzi alisema kuwa Serikali itahakikisha kuwa fedha zote zilizochukuliwa kinyume na taratibu zirejeshwe na inawataka wale wote waliolipwa au kuchukua fedha za umma kinyume cha utaratibuwazirejeshe mara moja na vyenginevyo hatua kazi za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.

Aliongeza kuwa Serikali itawapeleka wagonjwa wa muda mrefu katika Bodi ya Uchunguzi wa Afya (Medical Board) na endapo watathibitika kwamba hawawezi kuendelea na kazi watastaafishwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utumishi wa Umma.

Pamoja na hayo, Serikali itafanya uhakiki maalum kw awatumishi walioko masomoni kwa muda mrefu ili kujiridhisha kama bado wanaendelea na masomo au vyenginevyo na hatua muafaka kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utumishi wa Umma zitachukuliwa dhidi ya watumishi watakaobainika wameshamaliza masomo lakini bado hawajaripoti makazini.

Serikali pia, itawastaafisha kwa mujibu wa Sheria wafanyakazi wote ambao wameshapita umri wa kustaafu lakini bado hawajastaafishwa na wanaendelea na kazi pamoja na kufanya uchunguzi juu ya matumizi tofauti ya fedha zinazozidi wakati wa zoezi la kulipa mishahara ili kujua namna zinavyotumiwa na Taasisi za Umma na kama zinatumiwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Fedha au vyenginevyo.

Sambamba na hayo, alisema kuwa Serikali itawachukulia hatua muafaka kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utumishi wa Umma wafanyakazi ambao hawahudhurii kazini kwa muda mrefu bila ya udhuru ama sababu zinazokubalika kisheria.

Pia, alisema kuwa Serikali itahakiki upya mishahara ya wafanyakazi ambao hawakujitokeza kabisa kuhakikiwa na kujiridhisha endapo wafanyakazi hao wapo kiuhalisia au vyenginevyo na kujua sababu zilizowazuia kutojitokeza kuhakikiwa wakati zoezi la uhakiki lilipofanyika.

Aliongeza kuwa Serikali itafanya uchunguzi wa kina kwa watumishi wote waliohusika kwa namna moja au nyengine ama kwa uzembe au makusudi katika kusababisha matumizi ya fedha za umma kinyume na ilivyostahiki na kuchukuliwa hatua kazi za kinidhamu wale wote watakaothibitika kuhusika.

Katika mkutano huo na waandishi wa Habari, Dk. Abdulhamid alisema kuwa taarifa hiyo ni ya awali na matarajio ya kuwepo taarifa nyengine ambayo itataja kiasi cha fedha zilizopotea na itatolewa kwani bado uhakiki unaendelea katika Mawizara.

Alizitaja miongoni mwa Wizara ambazo zimegundulika kwa kiasi kikubwa na kadhia hiyo kuwa ni Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Wizara ya Afya na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.