Habari za Punde

Makamu Mwewnyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Shein Azindua Gari za Jimbo la Mfenesini za Abiria Zilizotolewa na Mbunge wa Jimbo Hilo.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                                23.04.2017
---
MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amewasisitiza WanaCCM na wananchi kuwachagua viongozi wazalendo walio mstari wa mbele katika kuwaletea maendeleo sambamba na kutekeleza ahadi zao kwa vitendo.

Dk. Shein ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliyasema hayo leo katika sherehe ya uzinduzi wa gari nane za abiria za Jimbo la Mfenesini zilizotolewa na Mbunge wa Jimbo hilo Kanali Mstaafu, Masoud Khamis, sherehe zilizofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Z Ocean Bububu Kihinani Mkoa wa Mjini Magharibi.

Katika hotuba yake, Dk. Shein alisema kuwa ni wajibu wa kiongozi kuhakikisha pale anapotoa ahadi yake basi huitekeleza, na kusifu moyo wa Mbunge huo kwa kutoa kiasi cha fedha zipatazo Tsh. Milioni 192,000,000 kwa ajili ya kununua gari hizo.

Dk. Shein alimpongeza Mbunge huyo kwa kuendeleza na kudumisha mashirikiano ya dhati kati yake na wananchi wa Jimbo hilo sambamba na mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo hilo.

Aliongeza kuwa kiongozi ni lazima apende kuwasikiliza wananchi wake pamoja na kufanya kazi na watu na awe mbunifu, anaependa kusikiliza watu, kuwaona watu na hatimae kutekeleza kwa vitendo hasa yale anayoyaahidi na kuwataka wanaCCM na wananchi kuwaunga mkono viongozi kama hao.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar aliwataka WanaCCM na viongozi wa Chama hicho pamoja na wananchi wa Jimbo hilo kuendelea kuwaunga mkono na kuwanao viongozi hao wa Jimbo hilo ili Mfenesini iwe mpya na izidi kunawirika na kuwaeleza kuwa hawakufanya kosa kumchagua Mbunge huyo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa gari hizo zitasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza tatizo la ajira kwa vijana na kueleza imani yake kuwa gari hizo zitaendeshwa vizuri na zitatunzwa na kueleza kuwa jambo hilo liwe mfano kwa viongozi wa Majimbo mengine hapa nchini.

Katika sherehe hiyo Dk. Shein nae kwa upande wake alimuunga mkono Mbunge huyo wa Jimbo la Mfenesini kwa kuahidi kuzilipia Bima gari hizo zote nane ambazo zilikuwa bado hazijalipiwa Bima lakini tayari taratibu nyengine zote zilikuwa zimeshafanyiwa kazi.

Aidha, Dk. Shein aliwaeleza wananchi wa Jimbo hilo kuwa barabara za ndani zilizopo katika Jimbo hilo zitatengenezwa huku akieleza juhudi za Serikali katika ujenzi wa barabara kuu Unguja na Pemba sambamba na ufumbuzi wa tatizo la maji kwa Mkoa wa Mjini Magharibi na kusema kuwa karibuni tatizo hilo litakuwa historia.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliendelea kuwaeleza viongozi wa CCM kuyaeleza mafanikio yaliopatikana ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Nae  Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar alieleza mashirikiano mazuri yaliopo kwa viongozi wa chama hicho Majimboni mwao na kuahidi kufanya kazi kwa mashirikiano na kuwataka WanaCCM wasikubali kusikiliza kasumba kutoka katika baadhi ya vyama vya upinzani.

Mapema Mbunge wa Jimbo hilo Kanali Mstaafu  Masoud Khamis alimkabidhi kadi zote nane za gari hizo na kueleza kuwa kuazia leo gari hizo sio zake ni gari za CCM kupitia uongozi wa Jimbo hilo na matawi yake yote chini ya Bodi ya udhamini ya Jimbo hilo huku akisisitiza kuwa kwa dereva yeyote atakaekiuka taratibu zilizowekwa ajue hana kazi.

Mbunge huyo alieleza kuwa kukabidhi kwa gari hizo ni kutekeleza kwa vitendo ahadi yake aliyoahidi wakati akitafuta ridhaa ya wananchi kumchagua katika uchaguzi Mkuu uliopita huku akisema kuwa ni kawaida yake kutoa ahadi kwa yale anayoyamudu ambayo yamo katika uwezo wake na kuchelea kuahidi mambo ambayo hana uwezo nayo

Nao viongozi wa CCM, Mkoa, Jimbo, Wilaya pamoja na WanaCCM wa Jimbo hilo katika maelezo yao walitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kuendelea kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama hicho ya mwaka 2010-2020 ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa ukusanyaji wa mapato.

Katika maelezo yao viongozi hao walitumia fursa hiyo kumpongeza Dk. Shein kwa kutekeleza ahadi yake kwa vitendo ya kuwapandisha mshahara wafanyakazi wa sekta ya umma kuazia mwezi huu wa Aprili ambapo tayari ameshatekeleza na wafanyakazi wamepongeza hatua hiyo.

Gari hizo nane yaliotolewa na Mbunge huyo ni kwa ajili ya Matawi Manane ya CCM yaliyomo katika Jimbo hilo lkiiwemo Tawi Chuini, Tawi la Kihinani, Tawi la Mfenesini, Tawi la Bumbwisudi, Tawi la Mwakaje, Tawi la Mwachalale, Tawi la Kitundu na Tawi la Kama.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.