Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Aipongeza China Kwa Msaada Wake Ujenzi Unwanja wa Kisasa wa Mao Tse Tung Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                               19.08.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa kutokana na kasi ya Serikali anayoiongoza katika kuimarisha miundombinu ya michezo ana matumaini makubwa kuwa sekta hiyo itazidi kuimarika na kuitangaza zaidi Zanzibar katika medali ya michezo ndani  na nje ya nchi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo alipofanya mahojiano na waandishi wa Habari mara baada ya kukagua ujenzi wa Uwanja wa Mpira wa MaoTse Tung, uliopo mjini Unguja, ambao unajengwa upya kwa msaada wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, wakati akiwa katika ziara yake katika Mkoa wa Mjini Magharibi.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa Serikiali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika juhudi kubwa za kuimarisha miundombinu ya michezo vikiwemo viwanja vya mpira ambavyo vitajengwa katika Wilaya zote Unguja na Pemba pamoja na kuvifufua vya zamani kama kiwanja hicho cha Mao Tse Tung.

Dk. Shein alisema kuwa uwanja huo utakapokamilika mbali ya kuwa na viwanja vya mpira wa miguu viwili pia, kutakuwemo na viwanja vyengine vya michezo ya ndani pamoja na viwanja vya mpira wa kikapu, mpira wa mikono, mpira wa meza kiwanja cha mazoezi ya kunyajua vitu vizito na mashine zake pamoja na michezo mingine midogo midogo.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa kiasi cha TZS Bilioni 11 zinatarajiwa kutumika kati ujenzi wa kiwanja hicho hadi kumalizika kwake ikiwa ni msaada kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo ukiwemo mradi huo  wa ujenzi wa uwanja wa Mao Tse Tung na kusisitiza kuwa China ni marafiki wa kweli.

Alieleza kuwa Serikali ya Jamahuri ya Watu wa China imezidi kuvutika na ujenzi huo hasa kutokana na historia ya uwanja huo ambao una jina la kiongozi wa kwanza wa Taifa hilo marehemu Mao Tse Tung.

Dk. Shein alieleza kuwa ujenzi wa uwanja huo ni miongoni mwa mafanikio ya utekelezaji wa ahadi za Serikali ya China iliyotokana na ziara yake aliyoifanya nchini humo ambapo mbali ya mradi huo pia, kulikuwemo na miradi mingine ukiwemo mradi wa ujenzi wa Bandari ya Mpaigaduri pamoja na jengo la abiria katika uwaja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.

Aliongeza kuwa kukamilika kwa uwanja huo kutatoa nafasi kubwa ya kutekeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya michezo hapa nchini.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa  michezo ina faida kubwa ikiwa ni pamoja na kupelekea watu kujuana, kupendana pamoja na kushirikiana sambamba na kujenga udugu.

Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Omar Hassan King alieleza kuwa katika eneo hilo kutakuwa na viwanja viwili vya mpira wa miguu ambavyo viwanja hivyo vitakuwa na sifa zote za kimataifa vitakavyokuwa na urefu wa mita 105 kwa 68.

Aidha, aliongeza kuwa kiwanja hicho kitakuwa na eneo la Wageni Mashuhuri (VIP), uwanja ambao utakuwa na milango sita pamoja na majukwa ambayo yatakuwa na uwezo wa kuchukua watazamaji 1500.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa uwanja huo unatarajiwa kumalizika mwezi Machi mwakani kwa mujibu wa makubaliano na Kampuni ya Ujenzi kutoka nchini China iitwayo ZHENGTAI GROUP huku akisisitiza kuwa ujenzi huo unaendelea vizuri.

Nae Balozi Mdogo wa China anaefanya kazi zake hapa Zanzibar Xie Xiuowu alimuhakikishia Dk. Shein kuwa uwanja huo utamalizika kwa wakati. 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.