STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 29.08.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, viongozi pamoja
na wananchi wake wataendelea kuiunga mkono Kamisheni ya Kiswahili ya Jumuiya ya
Afrika Mashariki kwa lengo la kuiimarisha lugha ya Kiswahili ambayo inaendelea
kujipatia umaarufu mkubwa duniani kote.
Dk. Shein aliyasema
hayo wakati alipokuwa na mazungumzo na Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya
Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki Profesa Kenneth Linyani Simala, Ikulu
Mjini Zanzibar.
Katika Mazungumzo hayo,
Dk. Shein alisema kuwa kuna kila sababu ya kuendelea kuiunga mkono Kamisheni ya
Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo kwa hivi sasa Makao makuu yake yapo
hapa Zanzibar kwa kutambua kuwa asili na chimbuko la lugha ya Kiswahili ni Zanzibar.
Alieleza kuwa Zanzibar
imefarajika kwa kiasi kikubwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki kufanya uwamuzi
wa makusudi wa kuyaweka makao makuu ya Kamisheni hiyo hapa Zanzibar kwani
Zanzibar inahistoria kubwa ya lugha ya Kiswahili.
Alisisitiza kuwa Afika
Mashariki ndio wenye Kiswahili hivyo ni jambo la busara kuwepo kwa Kamisheni hiyo ambayo itaendeleza na kukikuza
Kiswahili ili kizidi kuimarika.
Dk. Shein alisema kuwa
Kiswahili ni lugha tajiri na maarufu sana ulimwenguni hivyo kuna haja ya
kuchukua juhudi za makusudi katika kuhakikisha lugha hiyo inazidi kuimarika na
kupata mafanikio makubwa zaidi.
Aidha, Dk. Shein
alieleza matumaini yake makubwa ya uongozi wa Katibu Mtendaji huyo Profesa
Simala katika kuiendeleza na kuiongoza Kamisheni hiyo muhimu kwa nchi za Afrika
ya Mashariki.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein alieleza haja ya kukiimarisha zaidi Kiswahili pamoja na kukipa hadhi yake
katika kukizungumza hasa katika mikutano ikiwemo ya Jumuiya hiyo na mengineyo
huku akieleza kusikitishwa kwake na baadhi ya mikutano inayowashirikisha
wahusika wengi waswahili hapa nchini lakini huendeshwa kwa lugha ya kiengereza
kwa kisingizo cha udhamini wa mikutano hiyo.
Dk. Shein alieleza
kuwa hali hiyo ni kinyume na nchi nyengine duniani ambazo zinakuza, zinathamini
na kuimarisha lugha zao ambazo huzipa kipaumbele kwa kutambua umuhimu wake
katika kuzipa hadhi lugha zao.
Kutokana na hali hiyo,
Dk. Shein alieleza haja ya kukizungumza Kiswahili ili kizidi kuimarika na
kukijengea heshima na hadhi yake kama ilivyo kwa baadhi ya nchi nyengine
duniani ambazo hutumia lugha zao kama lugha za taifa ambapo hutumia hata
kusomeshea katika vyuo vyao vikiwemo vyuo vikuu.
Nae Katibu Mtendaji wa
Kamisheni ya Kiswahili ya Jumuiya ya
Afrika Mashariki Profesa Kenneth Linyani Simala alitoa shukurani za dhati kwa Dk. Shein kwa
juhudi kubwa zilizochukuliwa na Serikali yake anayoiongoza kwa kuipokea
Kamisheni hiyo pamoja na kuipa jengo ambalo kwa sasa ndio makao makuu ya
Kamisheni hiyo.
Kutokana na juhudi
hizo za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, pamoja na zile za Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Katibu Mtendaji huyo alieleza kuwa mafanikio
makubwa yatapatikana katika kukiimarisha Kiswahili kutokana na mashirikiano
hayo.
Aidha, Profesa Simala
alimueleza Dk. Shein kuwa Kamisheni hiyo imeweza kukutana na wadau mbali mbali
na kuunda mpango mkakati ambao utazinduliwa katika Kongamano la Kiswahili la kwanza
linalotarajiwa kufanyika hapa Zanzibar.
Aliongeza kuwa
Kongamano hilo linatarajiwa kuwashirikisha wajumbe 150 kutoka nchi wanachama
zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na wajumbe kutoka Uturuki, Burundi,
DRC Congo, Burundi, Rwanda, Namibia, Wanahabari, wanasiasa na washiriki wadau wengine
kutoka nchi mbali mbali duniani.
Alieleza kuwa miongoni
wma mambo ambayo wajumbe hao watajifunza ni pamoja na kuijua historia ya
Zanzibar na baadae ripoti itatolewa kwa viongozi wa nchi zote za Jumuiya ya
Afrika Mshariki.
Profesa Simala
alitumia futsa hiyo kumueleza Rais Dk. Sheinazma ya Kongamano hilo la kwanza la
Jumuiya ya Afrika Mashariki ambalo linatarajiwa kufanyika hapa Zanzibar kwa
mara ya kwanza kuanzia tarehe 6 hadi tarehe 8 mwezi ujao.
Sambamba na hayo,
Profesa Simala alimueleza Dk. Shein miongoni mwa majukumu ya Kamisheni hiyo
kuwa ni kuwaweka pamoja wadau wa lugha hiyo ya Kiswahili huku akieleza kuwa
tayari kwa upande wa nchi za nje ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki zimeshatambua
umuhimu wa lugha ya Kiswahili ikilinganshwa na nchi husika za Jumuiya hiyo.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment