Habari za Punde

Wajumbe wa Kamati ya Ardhi na Mawasiliano ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar Wasifu Kazi Nzuri Inayofanywa na TMA Katika Kutoa Huduma za Hali ya Hewa Zanzibar.

 
Mwenyekiti wa kamati ya Ardhi na Mawasiliano wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mhe. Hamza Hassan Juma (mwenye koti jeusi) akielezea jambo wakati wa ziara ya kamati hiyo ilipokutana na mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri-TMA na menejiment ya TMA (hawapo pichani), kwenyea ukumbi wa mikutano wa TMA, Ubungo Plaza.
 
Siku ya Ijumaa, tarehe 25/08/2017, Kamati ya Ardhi na Mawasiliano wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar ilitembelea Makao Makuu ya Ofisi za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) yaliyopo jengo la Ubungo Plaza Dar es salaam  ili kuona na kupata taarifa mbali mbali za taasisi hiyo.

Taarifa ya utendaji ya TMA iliwasilishwa na ndugu Selemani Selemani (Mchumi) pamoja na mambo mengine aliwafahamisha wajumbe wa kamati hiyo kuwa Mamlaka imepokea ‘Certificate of Appreciation’ toka Idara ya kukabililiana kamisheni ya kukaliana na maafa  na Mamlaka ya usafiri wa majini (ZMA) kwa kazi nzuri inayofanywa ya kutoa huduma za hali ya hewa katika visiwa vya Unguja na Pemba.

Akizungumza kwa niaba ya wajumbe, Mwenyekiti wa kamati hiyo ya Ardhi na Mawasiliano wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mhe. Hamza Hassan Juma alisifu kazi nzuri inayofanywa na mamlaka katika kutoa huduma za hali ya hewa Zanzibar. Aliielezea menejiment ya TMA kuwa, huduma za hali ya hewa nchini zinazidi kuimarika hususan kwenye usahihi wa taarifa zinazotolewa kama vile utabiri wa kila siku na tahadhari, hivyo kuongeza imani kwa wananchi katika ufuatiliaji wa taarifa za hali ya hewa ukilinganisha na hapo  awali ambapo jamii ilikuwa na hulka ya kupuuzia taarifa hizo.

Mhe. Juma alifahamisha mchango wa TMA unatambuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) akitolea mfano wa pongezi zilizotolewa kwa Mamlaka na Makamu wa Pili wa Rais Mhe. Balozi Seif Ali Iddi kwenye Baraza la Wawakilishi la Zanzibar

Kwa upande mwengine, Mwenyekii wa Bodi ya Ushauri ya TMA Dkt. Buruhani Nyenzi aliwashukuru wajumbe hao kwa pongezi zilizotolewa na kuahidi kuisaidia Mamlaka kufikia malengo ya juu zaidi katika utoaji huduma kwa kuboresha miundo mbinu. Aidha aliwaeleza wajumbe hivi karibuni alikuwa na ziara ya kutembelea vituo vya hali ya hewa vya unguja na pemba ili kujionea hali halisi, hivyo wananchi wategemee huduma bora zaidi kwa kuwa lengo la Mamlaka ni kuongeza na kuviboresha vituo vyake na kuongeza usahihi wa takwimu za hali ya hewa zinazokusanywa.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi aliwashukuru wajumbe na kueleza utendaji kazi wa Mamlaka kwa kuzingatia weledi na ushirikiano uliopo baina ya wafanyakazi wenyewe na wadau wa hali ya hewa, Aidha, Dkt. Kijazi alijivunia uwepo wa wataalam wa sayansi ya hali ya hewa wenye sifa za kitaifa na kimataifa ambao mchango wao mkubwa umeonekana katika kuongeza usahihi wa taarifa zitolewazo.

IMETOLEWA NA: MONICA MUTONI, AFISA HABARI, MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.