Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameiagiza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kutatua changamoto zilizopo nchini ambazo huwasababisha mahujaji wa Tanzania kushindwa kushiriki na kutekeleza ibada ya Hija kikamilifu.
Balozi
Seif ameyasema hayo katika ofisi yake iliyopo Dar es salaam mtaa wa Magogoni baada
ya kutembelewa na Naibu waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki Mheshimiwa Dkt. Susan Kolimba.
Mheshimiwa
Balozi Seif ameagiza wizara hiyo na
kusisitiza ufuatiliaji wa karibu wa taratibu zote zinazopaswa kufuatwa kwa
ajili ya matayarisho na maandalizi ya
Ibada Hijja kwa waumini wa dini ya Kiislamu. Ameyasema hayo kwa kujua kuwa Wizara
hiyo ndiyo yenye mamlaka kamili ya kufuatilia na kushughulikia utaratibu kwa watu
wote wanaoenda nje ya nchi.
Hivyo wizara haina budi kulifuatilia suala
hilo na kutatua changamoto zilizopo ambazo zimekuwa ni kero kwa waumini wa dini
ya Kiislamu kila ifikapo kipindi cha kushiriki na kuitekeleza ibada hiyo,
ambayo ni nguzo ya tano kwa waislamu na ni faradhi kutekelezwa kwa kila mwenye
uwezo.
Balozi
Seif amesema kumejitokeza ishara mbali
mbali kwa waandaaji wa safari hizo ambazo zinaashiria dalili za kitapeli jambo
ambalo husababisha hasara kwa mahujaji au kushindwa kutimiza azma zao.
Aidha
Balozi Seif amesema imekuwa ni kawaida sasa kwa viongozi wa vikundi mbali mbali
wanaondaa safari hizo kuwa na malumbano na misuguano ya mara kwa mara kila
ifikapo kipindi cha kutekeleza ibada hiyo hasa wanapofika nchini Saudia Arabia
jambo ambalo linaitia fedheha nchi yetu.
Naye
Naibu waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Africa Mashariki Dkt.
Susan Kolimba amethibtisha kwamba changamoto zilizopo ni za muda mrefu na
zimekua zikijirudia kila ifikapo wakati wa matayarisho ya kutekeleza Ibada ya
Hija kwa waislamu. … Mheshimiwa Susan Kolimba ameahidhi
kuitisha kikao haraka iwezekanavyo kwa wadau wote wanaojishughulisha na safari
za hija nchini.
Na
kutoa ahadi mbele ya Mheshimiwa Makamu wa pilli wa Zanzibar kuzitatua
changamoto zilizopo haraka iwezekanavyo kabla ya kuanza taratibu za
kujiandikisha kwa ajili ya kutekeleza ibada hiyo.
Amesema
imekuwa ni kawaida sasa kwa waandaji wa safari za Hija hasa wa Tanzania Bara
kwa kuwa na misuguano ya mara kwa mara kila ifikapo kipindi cha kutekeleza
ibada hiyo sambamba na kushindwa kutekeleza taratibu zinazofaa kabla ya
kuelekea nchini Saudia Arabia. Changamoto hizo zimekuwa kero kwa waumini wa
dini ya kiislamu hususan kwa Mahujaji.
Aidha
amesema kupitia kikao hicho Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki inategemea kujifunza kwa waandaji wa Safari hizo kutoka Zanzibar
kwani wamebaini kuwa Zanzibar ina ueledi na uelewa mkubwa wa maandalizi hayo ya
safari za Hija.
“kuna makundi ambayo hayaelewi
jinsi ya kufanya taratibu za hija ndio maana wanapata usumbufu wakati wa safari
zao”
Sharifa Barki Juma
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar
No comments:
Post a Comment