Habari za Punde

Serikali Wilayani Ileje yatambua mchango wa wakulima wazalishaji mbegu.

Na Mwandishi Wetu, Ileje- Mbeya. 
SERIKALI Wilayani Ileje Mkoani Mbeya imepongeza jitihada zinazofanywa na wakulima wadogo wa Vikundi vya Amkeni Msiha na Sogea Ntembo kwa kuzalisha mbegu bora za mahindi ya aina ya Situka za daraja la kuazimiwa ubora -QDS ambayo kwa sasa zimeanza kutumiwa na wakulima wengi Wilayani humo.

Akizungumza hivi karibuni na Timu ya tathimini na ufuatiliaji toka Shirika la PELUM Tanzania, Afisa Kilimo na Umwagiliaji wa Halmashauri hiyo, Herman Njeje amesema uwepo wa wazalishaji hao wa mbegu umekuwa chachu ya mafanikio kwa makundi makubwa ya wakulima kuhitaji wa mbegu hizo kwa ajili ya kujitosheleza wakati wa msimu.

Aidha amesema kuwa kuwepo kwa vikundi hivyo vimeweka alama katika Wilaya ya Ileje kupitia uzalishaji huo na hivyo kuihakikishia Halmashauri hiyo uhakika wa mbegu na udhibiti wa uingizwaji ama ununuzi wa mbegu feki jambo ambalo limekuwa likiathiri tija na uzalishaji wa mazao ya kilimo.

“Wakulima hawa wameonyesha juhudi kubwa na za kipekee katika kuhakikisha uzalishaji wa mbegu hii ya mahindi aina ya situka unakuwa endelevu hivyo basi sisi kama Halmashauri kuwaongezea kununua hakali mbili za ardhi kama njia mojawapo ya kuwaongezea eneo la uzalishaji wa mbegu na hii ni baada ya kuona kuna uhitaji mkubwa wa mbegu hizi kwa jamii inayowazunguka wakulima hawa,” alisema Njeje.

Kwa mujibu wa Njeje Ameongeza pia kutokana na juhudi hizo za uzalishaji wa mbegu, Halmashauri hiyo kupitia wataalamu wake wa kilimo wameendelea kuwa karibu na wakulima hao katika kuhakikisha kuwa hawapati vipingamizi wakati wa uzalishaji na usafirishaji wa mbegu yao kuanzia hatua za uaandaaji wa shamba la mbegu hadi kufungasha mbegu.

Ameongeza kuwa Halmashauri pia imekua ikiwapeleka kushiriki katika maonyesho  mbalimbali kwa ajili ya kutangaza na kuuza mbegu hizo pamoja na kutoa msaada wa kitaalamu pale inapohitajika na kuwaunganisha na wataalamu wa SIDO kwa ajili ya upatikanaji wa vifungashio bora.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi huo wa mbegu, kutoka shirika la Intergrated Rural Development Organization (IRDO-Ileje), Sinda Gasheka  amesema mbegu hiyo inayozozalishwa na wanavikundi hao imekuwa msaada mkubwa kwa wakulima wengi toka kata ya Chitete wilayani Ileje kutokana na kuwapatia mavuno mengi.

Mmoja wa wakulima wazalishaji wa mbegu hiyo, Maison Siwale amesema kuwa mbegu hiyo imeonyesha uzalishaji mzuri jambo linalochangia wakulima wengi kuwa na uhitaji nayo tofauti na mbegu za asili kwa kuwa mbegu hiyo inastahimili hali ya hewa pia na kukomaa mapema.

Kwa upande wake meneja miradi wa shirika la PELUM Tanzania, Rehema Fidelisi ameishukuru Halmashauri ya Ileje kwa kuwa karibu na wakulima hao na kusema kuwa ushirikano huo utawezesha vikundi kuendelea kuzalisha mbegu bora za mahindi na hivyo kuimarisha uhakika wa chakula na kipato.

Mradi huu wa uhakika wa mbegu kwa uhakika wa chakula na kipato unaofadhiliwa na watu wa Bread for the World na kusimamiwa na Shirika la PELUM Tanzania, unatekelezwa kwenye Mikoa nane ambayo ni Kilimanjaro, Morogoro, Dodoma, Kigoma, Songwe, Mbeya, Manyara na Shinyanga.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.