Habari za Punde

Urafiki kati ya China na Zanzibar wazidi kuimarika kwenye sekta ya elimu na utamaduni

 Balozi wa China Xie Xieo Wu wa katikati akitoa maelezo kwa waandishi wa habari na Viongozi wa Chuo cha Uandishi wa Habari Zanzibar kuhusu mikakati waliyojipangia juu ya kuisaidia Serikali ya Zanzibar Kuzidi kupiga hatuwa ya maendeleo , huko Ofisini kwake  Mazizini.
PICHA ya pamoja iliyojumisha Viongozi mbali mbali akiwemo Balozi wa China Xie Xieo Wu wa Tano Kulia, Viongozi wa Chuo cha Uandishi wa Habari Zanzibar pamoja na Viongozi wengine.(Picha na Maryam Kidiko Maelezo Zanzibar.  

Na Mwashungi Tahir / Maryam Kidiko -Maelezo 
USHIRIKIANO katika Sekta ya Elimu na Utamaduni kati ya China na Zanzibar umeelezwa kuwa umesaidia sana katika kuendeleza urafiki baina ya wananchi wa nchi hizo mbili.

Balozi  mdogo wa China aliepo Zanzibar Xie Xiao Wu alieleza hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari  katika Ubalozi  wao  uliopo Mazizini ikiwa ni maadhimisho ya siku ya Walimu Nchini China.

Alisema utamaduni wa China na Zanzibar unafanana na wananchi wa nchi hizo mbili wamekuwa wakishirikiana katika masuala mbali mbali ikiwemo biashara na makampuni ya China kuaminika katika kujenga Ofisi za Serikali na watu binafsi.

Balozi Xie  alisisitiza kuwa  China itaendelea kuisaidia Zanzibar katika harakati zake za kiuchumi na hivi sasa wanasimamia ujenzi wa viwanja viwili vya michezo Mao tse tung na  wanatarajia kujenga bandari mpya katika eneo la Mpigaduri Mjini Zanzibar.

Aliwapongeza vijna wa Zanzibar kwa kuwa na mwamko wa kujifunza lugha ya kichina katika Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar na Chuo cha Uandishi wa Habari  na ameeleza matumaini yake kuwa katika miaka michache ijayo vijana wengi watakuwa na uwezo wa kuitumia lugha hiyo na kupanua wigo wa biashara kati ya China na Zanzibar.

“Kila mwaka vijana 200 hadi 300 wanajiunga katika kujifunza lugha ya kichina na wamekuwa wakifanya vizuri katika mitihani yao, haya ni maendeleo makubwa,”alisema Balozi mdogo wa China.

Mkuu wa Chuo  cha Uandishi wa Habari Zanzibar Chande Omar Omar aliishukuru Jamhuri ya Watu wa China kwa msaada wa kuleta walimu kufundisha lugha hiyo  katika chuo hicho na mafanikio yameanza kuonekana kwani baadhi ya vijana wanauwezo wa kusoma na kuzungumza lugha hiyo.

Alisema hivi sasa zaidi ya wanafunzi 30 kutoka chuo cha Undishi wa Habari  wamepata nafasi ya masomo ya nchini China  baada ya kufanya vizuri mitihani ya lugha ya kichina chuoni hapo.                                              

Aliongeza kuwa mbali na wanafunzi hao, wanafunzi wengine tisa wa Chuo hicho wanatarajiwa kuondoka hivi karibuni kuelekea nchini China kwa mafunzo zaidi ya lugha na fani ya uandishi wa habari na watakaporejea watakuwa walimu wa wenzao katika vyuo mbali mbali vya Zanzibar .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.