Habari za Punde

Hutuba ya Mhe Samia Wakati wa Uzinduzi wa Sera Hiyo Dodoma.


Hotuba ya Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, Katika Hafla ya Uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2016,na Mkakati wa Utekelezaji wa Sera Hiyo Tarehe 23 Oktoba, 2017
Dodoma. 
Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb.), Waziri wa Fedha na Mipango;
 Mhe. Suleiman Jafo; Waziri TAMISEMI;
Jabir Shekimweri; Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mhe. Hawa Ghasia; Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge Bajeti;
Mhe. Ashatu Kijaji; Naibu Waziri Fedha na Mipango;
Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Kamati ya Bajeti;
Mhe. Mstahiki Meya wa Dodoma;
Makatibu Wakuu na Naibu Katibu Wakuu wa Wizara mliopo;

Mwakilishi wa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
Viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali;
Watendaji Wakuu wa Taasisi za Huduma za Fedha nchini;
Washirika wa Maendeleo mliopo hapa;

Waandishi wa Habari;

Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;

Habari za mchana.

Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na Amani kwa kutujalia uzima na afya njema na hivyo kuniwezesha kujumuika nanyi katika uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji  wa Sera hiyo.

Nitumie fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango (Mb), Waziri wa Fedha na Mipango na Kamati ya Maandalizi, kwa kunialika kushiriki kwenye tukio hili muhimu kwa ustawi wa   nchi   yetu   na   mustakbali   wa   sekta   ya fedha nchini.


Vilevile   nimpongeze   Dkt. Bilinith  Mahenge kwa kuchaguliwa
kuwa     Mkuu      wa       Mkoa      wa      Jiji      la    Dodoma.
Asante kwa mapokezi  mazuri  na nikutakie heri na mafanikio katika majukumu yako mapya na ninaamini utamudu vyema majukumu haya.

Pia nichukue fursa hii kuwatakia kila la heri wanafunzi wetu wa kidato cha nne wanaoanza mitihani yao leo. Ni imani yangu mmetayarishwa na mmejitayarisha vya kutosha. Hivyo niseme kila heri and all the best our dear students.

Sasa niruhusuni niendelee na hotuba yangu kwa kuipongeza Wizara ya Fedha kwa kutoa kipaumbele na msukumo mkubwa katika kufanyia mapitio na kuandaa sera hii. Niwasihi muendelee hivyo kwa sababu bado tunalo jukumu la kuhakikisha tunaandaa sera nyingi zaidi kwa masilahi mapana ya Taifa letu.

Kwa namna ya pekee, niwashukuru Wahisani wetu wa Maendeleo walioshirikiana na Serikali katika kusaidia ukamilishaji wa Sera hii. Kwa niaba ya Serikali ninawaahidi kwamba Sera hii itatumika ipasavyo na kuwanufaisha zaidi walengwa wa Sera hii ambao ni wananchi wa kipato cha chini.

Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Siku ya leo ni siku muhimu sana kwa Sekta ya Fedha Nchini. Hii ni kutokana na dhamira ya Serikali ya kuinua uchumi wa wananchi wa kipato cha chini. Uzinduzi wa Sera hii ni mwendelezo wa utekelezaji wa Ilani ya CCM inayosisitiza kupambana na umaskini hasa kwa kuwekea mkazo kwenye urasimishaji wa biashara na kuwapatia wafanyabiashara wadogo maeneo rasmi ya kufanyia biashara  ikiwa ni pamoja na kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu. (kifungu 6 (d) cha flani).

Hivyo, tukio hili ni kudhihirisha utayari wa Serikali kuweka mazingira wezeshi kwa wajasiriamali wadogo na wananchi wenye mahitaji maalum ili kujiwezesha kiuchumi. Hivyo, tunayo kila sababu ya kujivunia hatua hii, na nitumie fursa hii kuwasihi wadau wote wa sekta ya fedha nchini, kuendelea kutuunga mkono ili tuweze kupeleka mbele maendeleo ya nchi yetu.

Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama alivyobainisha  Mhe. Waziri wa Fedha na Mipango kuwa  Serikali iliamua kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2000 kwa kutunga Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wa Sera hiyo kwa kipindi cha miaka 10 ili kutatua upungufu na changamoto zilizojitokeza katika sekta ndogo ya fedha. Changamoto hizo ni pamoja na:
   i.       Ongezeko la idadi ya watoa huduma ndogo  za   fedha
ikiwa ni     pamoja      na     Benki     na     Taasisi     za
Fedha,   Programu   na Mifuko ya Serikali, Vikundi vya Fedha vya Kijamii kama vile Village Community Banks -VICOBA na Vyama vya Akiba na Mikopo Vijijini (VSLA), Kampuni za Simu, Asasi za Kijamii na Wakopeshaji binafsi;
 ii.       Ukosefu wa mfumo wa sheria na kanuni wa kusimamia taasisi zisizochukua amana na vikundi vya fedha vya kijamii;
iii.       Uelewa mdogo wa masuala ya fedha;
iv.       Ukosefu wa  takwimu katika sekta  ndogo ya fedha;
 v.       Kukosekana kwa mfumo wa kumlinda mtumiaji wa huduma ndogo za fedha;
vi.       Kutokuwepo na uwazi katika  vigezo na masharti ya utoaji mikopo; na
vii.       Viwango vya juu vya riba.
Pamoja na changamoto hizo, tafiti zilizofanywa kwengineko Duniani zimeonesha kwamba wakopaji maskini wamekuwa wakiishi na mikopo baada ya mikopo bila kuweza kujiwekea akiba na kukuza biashara zao.
Imeonekana kwamba mikopo imewezesha angalau watu maskini kuweza kuweka akiba ya kuwasaidia wanapokubwa na shida za familia zao.
       Imebaini pia kwamba katika maeneo kadhaa ya duniani mikopo nafuu haikuweza kutimiza malengo yaliyowekwa na mkutano wa Umoja wa Mataifa uliozungumzia masuala ya kuwezesha watu maskini kwa kutumia mikopo nafuu wa 1997.
       Umoja wa Mataifa uliweka malengo manne makubwa ikiwemo, mikopo iwafikie maskini wa maskini (mafukara); Kuongeza kipato cha maskini kwa kuwawezesha kujiajiri, Taasisi za Fedha ziweze kujijengea akiba kubwa ya kutosha kuendelea kukopeshana na kufanikiwa na kuwawezesha wanawake hasa wa Vijijini.  Vile vile, kuna maneno yaliyotumika bila kuwa na tafsiri ya kueleweka na kila mtu, kwa mfano, "umaskini wa maskini" - vipimo vyake ni vipi?  "Uwezeshaji wa Wanawake" - sio kiuchumi  tu, masuala  ya  mila Potofu,   Ujuzi wa   Biashara,

       Elimu ya Afya na Afya ya uzazi, kujua kusoma na kuandika n.k.  Taasisi za mikopo za faida na zisizo na faida - mipaka yao ni ipi?  Mambo haya tunapaswa nasi tuyaangalie kwa makini katika Sera zetu.

Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kwa kutambua umuhimu wa   Sekta Ndogo ya Fedha katika kupunguza Umaskini na Kukuza Uchumi, napenda kuchukua fursa hii kuwaomba wadau mbalimbali kutoa ushirikiano kwa Serikali ili kufanikisha utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017. Ili kutekeleza azma hii, ni matumaini yangu kuwa Wizara ya Fedha na Mipango itaendelea  kuratibu, kusimamia na kutathmini maendeleo ya sekta ya fedha ikijumuisha sekta ndogo ya fedha kwa kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya utekelezaji wa Sera hii.

Kwa kuwa walengwa wengi wa Sera hii ni wananchi wa kipato cha chini na wanafanya kazi katika maeneo na mifumo isiyo
rasmi, hivyo basi ni muhimu  kutoa elimu ya fedha na ujasiriamali. Kwa kulitambua hili, ningependa kuona  Mamlaka za Serikali za Mitaa zikiteleza yafuatayo:
   i.                    Halmashauri kutenga asilimia 10 ya mapato yao kama inavyotakiwa vikundi vya kina mama (asilimia 5) na vijana (asilimia 5) na kuhakikisha kuwa fedha hizi zinatumika ipasavyo na kuwanufaisha wote;
 ii.                    Zinatenga maeneo na kuweka mifumo rasmi itakayowawezesha wajasiriamali wadogo, vijana, wanawake na makundi maalum ili waweze kujiajiri;
iii.                     Zinahamasisha wananchi kuunda vikundi vya fedha vya kijamii na SACCOS pamoja na kuhakikisha kuwa wanasajili vikundi hivi rasmi; kufuatilia shughuli zao na kuhakikisha wanaweka fedha hizi kwenye mifumo rasmi ya kibenki;
iv.                     Zinajumuisha   masuala ya huduma ndogo za fedha kwenye mipango yao  ya maendeleo; na
 v.                    Zinaratibu  na kuandaa taarifa ya upatikanaji wa huduma za fedha kuanzia ngazi za kata hadi Mkoa.
vi.                    Kufanya tahthmini kila baada ya muda ili kubaini maendeleo ya Changamoto za utekelezaji wa Sera hii.

Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ili kufanikisha  lengo la Sera hii ambalo ni  kuimarisha huduma jumuishi za fedha kwa kujenga mazingira wezeshi yatakayoleta ufanisi wa utoaji wa huduma ndogo za fedha nchini kwa wananchi wenye kipato cha chini na, ili kutekeleza azma hiyo, nawasihi watoa huduma za fedha nchini kuangalia namna bora ya kupunguza riba za mikopo na tozo mbalimbali zinazotozwa kwenye upatikanaji wa huduma za fedha.

Aidha, ninawaomba muongeze ubunifu katika kutoa huduma zinazohitajika na wananchi wa kipato cha chini pamoja na kupeleka huduma hizo katika maeneo  yaliyo karibu na makazi yao au biashara zao. Vilevile nazitaka taasisi za huduma za fedha kuwaelimisha wananchi kabla ya kutoa huduma hizo ili kupunguza athari wanazozipata wananchi.

Ni matarajio yangu kuwa, Wizara ya Fedha na Mipango itashirikiana na wadau katika kutekeleza Sera hii  na kuhakikisha malengo ya Sera ambayo ni  kukuza uchumi na kupunguza umaskini yanafikiwa. Nimefurahi kuwaona wadau wa FSDT wakitoa mada kwa kuwa ni hivi karibuni tu walizindua Finscope Report ya mwaka 2017 ambayo ilionesha kuwa tumepiga hatua kwenye suala zima la huduma jumuishi za fedha (financial inclusion) na kufikia asilimia 72 kwa 2017,
na changamoto kuu waliyoianisha ni elimu/uelewa mdogo wa huduma za fedha. Hivyo basi nitoe rai kwa wadau wengine wa Serikali kuweza kusaidiana nasi katika kuhakikisha kuwa changamoto hii na zingine zilizobainishwa kwenye ripoti hii ya Finscope zinafanyiwa kazi ili  kuboresha sekta ya fedha nchini iweze kuwa na maendeleo endelevu kiuchumi.

Suala la utoaji elimu kwa wananchi kuhusu usimamizi bora wa fedha llitakuwa endelevu na Serikali itazidi kuboresha maslahi ya wataalamu wetu  na kufanya mapitio ya mara kwa mara kwenye sera zetu za fedha. Vilevile tutaweka mazingira wezeshi kwa vikundi mbalimbali vya kijamii vya kuweka na kukopa ili viweze kuinua kipato cha wafanyabiashara na wajasiriamali wadogo.

Hata hivyo, juhudi zetu hizo hazitakuwa na maana endapo hakutokuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha. Hivyo, natoa wito kwa watumishi wa umma, wadau wa sekta ya fedha na jamii kwa ujumla kusimamia kwa ukamilifu matumizi sahihi ya fedha za umma, ili tujenge Taifa la wananchi wenye uchungu na rasilimali zetu na uzalendo kwa nchi yao.
Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana;
Nilipata fursa kidogo ya kupitia Sera hii na nimefurahi kuona kuwa Sera hii imewapa kipaumbele makundi yenye uhitaji maalum kama wanawake na vijana kwa kuhakikisha kuwa itahamasisha matumizi ya teknolojia na ubunifu kwenye huduma za fedha zinazokidhi makundi haya; itatoa elimu kwa makundi haya, pamoja na kuhakikisha kuwa  itahamasisha ujumuishwaji wa watoa huduma ndogo za fedha wasio rasmi kwenye mfumo ulio rasmi kwa kuunganisha vikundi vya fedha vya makundi haya  na Taasisi   za   Fedha   kama   vile   Benki;
Mifuko   ya   Jamii,  Masoko   ya   Hisa   na   Mitaji   na   Bima.

Huduma hizi mara nyingi zimekuwa zikiwaacha watu ambao hawapo kwenye mfumo rasmi wa ajira  na hivyo kuachwa nyuma kimaendeleo. Kwa kuweka huduma hizi itahakikisha hamna mwananchi atakayeachwa nyuma kwenye maendeleo.

Jambo jingine lililonifurahisha kwenye Sera hii ni kuhusu Huduma za kibenki kwa mitandao (Mobile Banking) ambayo naamini ni huduma muhimu kwetu sote na hamna hata mmoja wetu hapa ambae hajaitumia wala hajanufaika na huduma hii. Naamini wengi siku hizi hatuwapi tena watu fedha mkononi wawapelekee ndugu na jamaa zetu waliopo vijijini bali tunatumia huduma hii kutuma fedha hizo. Nimefarijika kuona kuwa kwenye tamko la Sera katika Mobile Banking imezungumzia kuboresha kanuni za usimamizi wa sekta ndogo hii ya  fedha; kuwalinda watumiaji wa huduma hii pamoja na kuboresha miundombinu ya ubadilishanaji taarifa kati ya wasimamizi wa sekta hii ndogo ya fedha. Maana wote tunajua kuwa sekta hii isipokuwa na usimamizi basi wengine hutumia mianya iliyopo kufanya yao.

Nihitimishe kwa kurudia tena kuwa Uzinduzi wa Sera hii Mpya na yale yaliyomo katika sera hii ni ushahidi tosha wa dhamira ya Serikali  na ya wenzetu wote tulioshirikiana nao katika kutayarisha sera hii kuona huduma za kifedha nchini zinazidi kuimarika na kuwa bora zaidi. Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, najua wewe ni Bwana wa Mipango kama jina lako hivyo ni matumaini yangu kuwa wewe pamoja na wadau wengine mtahakikisha kuwa sheria ya sekta ndogo ya fedha inakamilika mapema iwezekanavyo.  Hivyo niwaambie kuwa tufanye ya wakati; wakati tuna wakati; utakuja wakati tukitaka kufanya ya wakati, wakati hatuna wakati! Basi wakati ni huu wa kutekeleza haya yote tuliyoyapanga.

Baada ya kusema haya machache, nirudie kwa kuwashukuru kwa kazi kubwa ya kuandaa sera hii.  Na sasa napenda kutamka kuwa  Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017 pamoja na Mkakati wa Utekelezaji wa Sera hiyo imezinduliwa rasmi.

ASANTENI SANA.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.