STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
10.10.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa katika kipindi cha hivi karibuni dhamira njema
ya kuwapa eka tatu wananchi kwa ajili ya kilimo iliyooneshwa na uongozi wa
Serikali tangu awamu ya Kwanza hadi hii ya Saba, imeanza kuharibiwa na baadhi
ya wananchi kwa kuziuza eka hizo na wengine kuzikata viwanja vya kujenga nyumba
na kuwauzia watu.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika ufunguzi wa maonesho ya
Siku ya Chakula Duniani, yaliofanyika huko Kizimbani na kuhudhuriwa na wananchi
pamoja na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali
Idd, Mama Mwanamwema Shein na viongozi wengine wa vyama vya siasa na Serikali.
Katika hotuba yake,
Rais Dk. Shein alisema kuwa kitendo hicho si kizuri kwani kinavunja mwelekeo wa
azma ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 sambamba na kupelekea vizazi
vijavyo kukosa sehemu za kilimo na hatimae kuagiza vyakula nje ya nchi.
Aliongeza kuwa ipo
haja ya kuzingatia matumizi mazuri ya ardhi ndogo iliyopo kwa kutenga maeneo ya
kilimo, maeneo ya makaazi na shughuli nyengine za kiuchumi sambamba na
kuzingatia sheria za Mipango Miji na Vijiji.
Aliongeza kuwa hivi
sasa Zanzibar ina watu milioni 1.4 hali hiyo inachangia kuwa na matrumizi
makubwa ya ardhi hasa kwa ajili ya makazi na kupnguza ardhi ya kilimo, hivyo
wananchi wanapotaka kujenga ni vyema wakapeka maombi yao katika Wizara ya
Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira ili waelekezwe taratibu ziliopo.
Alisema kuwa hivi sasa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kufanya Mapinduzi ya Kilimo kwa
kukifanya kilimo kuwa cha kisasa na cha kitaalamu hatua ambayo imeanza kuzaa
matunda kwa kuongezeka kwa kiwango cha mavuno na mazao mbali mbali hasa mazao
ya chakula yanayolimwa hapa nchini.
Alieleza kuwa mavuno
ya mpunga yameongezeka kutoka wastani wa tani 33,655.06 mwaka 2013 hadi tani
39,000, zilizovunwa mwaka huu, 2017 kiwango ambacho hakijawahi kufikiwa kwa
takriban miaka kumi iliyopita.
Dk. Shein alieleza
kuwa kwa upande wa mazao ya matunda mavuno yake yameongezeka kutoka wastani wa
tani 15,000 mwaka 2015/2016 hadi wastani wa tani 27,000 mwaka 2016/2017,
mafanikio haya yametokana na matumizi ya mbinu za kilimo cha kisasa na
kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa kilimo.
Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Serikali inazingatia umuhimu wa kilimo cha umwagiliaji maji hasa
kwa zao la mpunga ambapo kwa kushirikiana na Benki ya Exim ya Korea, Serikali
itatumia wastani wa Dola za Kimarekani milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa
miundombinu ya umwagiliaji wa hekta 1,524.
Alisisitiza kuwa lengo
la Serikali ni kuongeza mavuno ya mpunga nchini, kupunguza na hatimae kuondoa
kabisa utegemezi wa kupata mchele kutoka nje ya nchi ambapo hivi sasa kwa kila
mwezi Serikali inaingiza wastani wa tani 7,259 za mchele.
Kwa upande wa zana za
kilimo, Dk. Shein alisema kuwa katika kuziendeleza na kuziimarisha huduma za
matreka, Serikali imeandaa Mpango madhubuti wa Kiwanda cha Matrekta cha Mbweni
kuwa Wakala kwa mujibu wa sheria na kukipa hadhi yake inayostahiki katika kilimo
ambapo imekubaliana na Kampuni ya Mahindra Mahindra ya India kwa lengo la
kuleta matrekta mapya 100, zana nyengine
za kilimo na hivi karibuni Serikali imesaini matrekta 20 kwa kuanzia na tayari
yamepokewa matrekta 10 kutoka Serikali ya Libya.
Kwa maelezo ya Dk.
Shein alisema kuwa Serikali inaendelea na dhamira yake ya kujenga soko kubwa
jipya la kisasa la uvuvi katika eneo la Malindi kwa kushirikiana na Shirika la
Maendeleo la Japan (JICA).
Kadhalika, Dk. Shein
alsiema kuwa Serrikali imeanzisha kampuni ya Uvubvi ya Zanzibar (ZAFICO) kwa
mtaji wa TZS Bilioni 7 kutoka kwenye mashirika ya Serikali na katika muda mfupi
ujao Serikali inatarajia kuansiha shughuli za uvuvi kwa kununua meli 2 za
kisasa kwa kuanzia ambazo zitatoa ajira kwa vijana.
Pamoja na hayo, Dk.
Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiaja na
Serrikali ya Korea chini ya usimamizi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja
wa Mataifa (FAO) inajenga kituo cha kutotolea vifaranga vya samakli huko katika
eneo la Beit Ras.
Dk. Shein pia, aliwataka
vijana kuzitumia fursa zilizopo za kujiajiri katika sekta ya kilimo kwani
kilimo kinatoa fursa kubwa na ya pekee inayompa mwananchi fedha nyingi kwa
kipindi kifupi sambamba na kuwa na uhakika wa chakula na maendeleo ya nchi.
Baada ya hotuba hiyo Dk.
Shein alipata fursa ya kutembelea mabanda ya maonesho na kujionea shughuli za
kilimo, ufugaji na uvuvi huku akisisitiza haja ya Taasisi ya uvuvi wa Bahari
Kuu kushirikiana na Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika
kuimarisha uvuvi wa Bahari Kuu.
Mapema Waziri wa
Kilimo , Maliasili, Mifugo na Uvuvi Hamad Rashid Mohamed alisema kuwa maonyesho
hayo ni katika kutekeleza maagizo waliyopewa na Dk. Shein katika kutayarisha
maonyesho hayo yanayoendana na sikukuu ya wakulima ya nanenane huku akieleza
haja ya kuwepo kiwanja kama hicho huko kisiwani Pemba kwa madhumuni kama hayo.
Katibu Mkuu wa Wizara
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Joseph Abdalla Meza alisema kuwa eneo hilo
limetengwa kuwa ni eneo la kudumu lenye heka 16 ambapo miongoni mwa shughuli
zilizofanyika ni kwuez uzio, njia, miundombinu ya maji, umeme na kugharimu TZS
milioni 89 na hadi kukamilika kwa majengo ya kudumu kutagharimu TZS milioni
223.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment