Habari za Punde

Rais Dk Shein, Amtumia Salamu za Pongezi Rais wa wa Kenya Uhuru Kenyatta.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                 29.11.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amemtumia salamu za pongezi Rais wa Jamhuri ya Kenya Uhuru Muigai Kenyatta kwa kuapishwa kuwa Rais na kuendelea kuiongoza nchi hiyo kwa kipindi cha pili.

Sherehe za kuapishwa kwa Rais Kenyatta zilifanyika hapo jana Novemba 28, 2017 katika uwanja wa Kasarani Mjini Nairobi na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi na viongozi mbali mbali wa Kimataifa wakiwemo baadhi ya Marais kutoka nchi za Afrika ambapo kwa Tanzania Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan alimuwakilisha Dk. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika salamu hizo za pongezi Dk. Shein alimueleza Rais Kenyatta kuwa wananchi wa Zanzibar wanaungana na ndugu zao wa Kenya katika kusherehekea ushindi wa kiongozi huyo pamoja na kuahidi kuendelea kumuunga mkono kiongozi huyo ili aendelee kuiongoza vyema nchi hiyo kwa amani na utulivu.
Salamu hizo zilieleza kuwa ushindi wa Rais Kenyatta wa asilimia 98.2 ya wananchi waliomchagua katika uchaguzi wa marudio uliofanyika nchini humo umeonesha wazi kuwa Rais Kenyatta anakubalika kwa wananchi wa nchi hiyo kutokana na juhudi zake za maendeleo kwa nchi yake na nchi zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa jumla.

Aidha, Dk. Shein alimuhakikishia Rais Kenyatta kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano mkubwa uliopo kati yake na Kenya sambamba na kuimarisha udugu uliopo kati ya wananchi wa nchi hiyo na wananchi wa Zanzibar.
  
Sambamba na hayo, salamu hizo zilieleza kuwa kuchaguliwa kwake Rais Kenyatta kwa mara ya pili ni fursa adhimu aliyopewa na wananchi wa Kenya kwa ajili ya kuendeleza dhamira yake ya kulitafutia maendeleo ya haraka Taifa hilo, kuimarisha Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Taasisi mbali mbali za Kimataifa.

Hivyo, Dk. Shein alimtakia uongozi mwema, afya njema kiongozi huyo wa Taifa la Kenya, pamoja na kuendeleza maendeleo endelevu yaliopatikana nchini humo.

Rais Kenyatta aliyezaliwa Oktoba 26 mwaka 1961 akiwa mtoto wa kwanza wa Rais Mzee Jomo Kenyatta na mkewe Mama Ngina Kenyatta alichaguliwa tena kuwa Rais wa Kenya baada ya kuibuka mshindi katika kinyanganyiro cha kuwania urais kwa silimia 98.2 ya Kura katika uchaguzi wa marudio wa Oktoba 26 mwaka huu.
Katika hotuba yake aliyoitoa hapo jana mara baada ya kuapishwa Rais Kenyata alitangaza kuwa kuanzia sasa raia wa nchi za Afrika Mashariki kwa kutumia vitambulisho vyao vya uraia wa nchi zao wataweza kufanya kazi, kumiliki mali, shamba, kuoa na kuolewa sambamba na kuishi nchini humo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.