Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Shein Apokelewa Kwa Shangwe Afisi ya CCM Mkoa wa Mjini Amani Zanzibar.

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amewataka viongozi wote wa Chama Cha Mapinduzi kutekeleza majukumu yao ili kuendelea kukipa ushindi chama hicho katika chaguzi zijazo na kuendeleza wimbi la ushindi.

Makamu huyo wa Mwenyekiti wa CCM Zanzibar aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa CCM Amani, Mkoa wa Mjini katika  hafla ya kumpokea na kumpongeza baada ya kuchaguliwa kwa kura zote kuendelea kuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar katika mkutano Mkuu wa Tisa wa CCM Taifa uliomalizika hivi karibuni huko mjini Dodoma.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa kuchaguliwa kwake kwa kura zote na kupata ushindi wa asilimia mia moja ni deni ambalo malipo yake ni kuhakikisha anashirikiana kikamilifu na viongozi wa CCM katika ngazi zote ili waweze kushinda kwa kishindo katika uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 Tanzania Bara na Zanzibar.

Makamu Mwenyekiti huyo aliahidi kuwa katika kutekeleza jukumu walilompa atahakikisha kwamba uchumi wa Zanzibar unaendelea kuimarika sambamba na kudumisha amani, umoja na mshikamano miongoni mwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa jumla.

Dk. Shein alisema kuwa kazi hiyo anaiweza na ataifanya kwa bidii na kuongoza kwa uadilifu katika kuhakikisha CCM kinazidi kuimarika hasa kutokana na ukongwe kwa chama hicho na ndio maana watu walio wengi wanakipenda.

Alieleza kuwa kazi ya uongozi wa achama hicho ni ya watu wote na kusisitiza haja kwa wale wote ambao wan aharibu kutokana na wanayoyasema sio wanayoyatekeleza

“Naahidi kwa dhati ya moyo wangu na kwa mapenzi niliyonayo kwa wananchi wote wa Tanzania na Chama changu kwamba nitaendelea kulitekeleza jukumu hilo vizuri, kwa uadilifu na kwa nguvu zangu zote’,alisema Dk. Shein.

Aidha,alisisitiza haja ya kuwa imara katika kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 ambayo hivi karibuni yanatimia miaka 54 na kusisitiza kuwa kwa yeyote tule ambaye atayabeza atashughulikiwa sambama na kudumisha Muungano uliopo.  

Pamoja na hayo, aliwataka viongozi waCCM kuhakikisha kwamba ratiba ya kazi za chama, mikutano na ziara zinafanywa kama kalenda ya chama inavyoonesha na kusisitiza kuwa huu si wakati wa kuyafunga kufuli Matawi ya chama hicho na wala sio wakati wa kuwangojea viongozi wakuu wa CCM wafanye ziara na wao wafuate nyuma.

Sambamba na hayo, aliwataka viongozi wa CCM wote kufuata taratibu zilizowekwa na chama hicho katika kukosoana ikiwa ni pamoja na kuvitumia vikao vyao vya chama.

Alieleza kuwa kwa kila aliepewa nafasi anapaswa aiweke mbele CCM, aipe heshima yake huku akiwataka kuzingatia hotuba ya Mwenyekiti wa CCM Taifa Dk. John Pombe Magufuli aliyoitoa wakati wa ufunguzi na ufungaji wa Mkutano Mkuu wa Tisa wa CCM uliofanyika Disemba 18 mwaka huu huko Dodoma.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwaeleza wanaCCM waliohudhuria mkutano huo mipango ya Serikali ya kujenga miji mipya ukiwemo mji wa Chumbuni na  Kwahani huku akieleza kuwa hivi karibuni ujenzi wa jengo la abiria katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, Zanzibar ujenzi wake utaanza na kuchukua muda wa miezi 18 sambamba na hatua za ujenzi wa Bandari ya Mpigaduri zinavyoendelea.

Pia, alieleza azma yake ya kufanya ziara na kukutana na Mabalozi wa Wilaya zote za Unguja na Pemba mara baada ya kumalizika sherehe za miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Nao viongozi wa chama hicho wakieleza kwa niaba ya viongozi wenzao wakiwemo Makatibu wa Mikoa, Wenyeviti wanaCCM wote wa Zanzibar na wananchi kwa jumla walitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa mafanikio yaliopatikana sambamba na utekelezaji wake mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015-2020.

Aidha, viongozi hao walimueleza Dk. Shein kuwa kutokana na uongozi wake uliotukuka ndani ya CCM hapa Zanzibar umepelekea kuimarika kwa uchumi na kuongezeka kwa mapato ya chama hicho huku wakimwagia sifa kutokana na uwamuzi wake wa kuwalipa Pencheni Jamii wazee wote kuanzia miaka 70 bila ya kujali itikadi zao za kisiasa sambamba na kuongeza mishahara.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.u

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.