Habari za Punde

Zanzibar Kuimarisha uhusiano wake na Morocco


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu ameeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kukuza na kuimarisha uhusiano kati yake na Morocco hasa katika masuala ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni kwa faida ya nchi mbili hizo pamoja na watu wake.

Waziri Gavu aliyasema hayo leo katika mkutano maalum uliohudhuriwa na viongozi wa Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Balozi wa Ufalme wa Morocco katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Abdelilah Benryane, mkutano uliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo,  alimuhakikishia Balozi Benryane kuwa Zanzibar itaimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati yake na Morocco huku akieleza kuwa Zanzibar ina mambo mengi ya kujifunza kutoka nchini humo.

Waziri Gavu alisema kuwa ziara ya kiongozi wa nchi hiyo, Mfalme Mohammed VI aliyoifanya hapa nchini mnamo mwezi Oktoba mwaka jana imeonesha dalili za uhusiano na ushirikiano mwema kati ya Tanzania ikiwemo Zanzibar na Morocco sambamba na ziara iliyofanywa na baadhi ya watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar aliowaongoza Waziri Gavu nchini humo mnamo mwezi Agosti mwaka huu.

Aliongeza kuwa katika ziara hiyo muhimu iliyofanywa na Mfalme huyo wa Morocco hapa nchini Tanzania iliweza kusaini makubaliano takriban 22 ya ushirikiano kati yake na Morocco katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo kilimo, gesi, mafuta, utalii na sekta nyenginezo.

Waziri Gavu alimueleza Balozi huyo kuwa ziara hizo kutokana na umuhimu wake zimeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha mashirikiano na uhusiano kati ya Zanzibar na Morocco na kuna kila sababu ya kuendelezwa kwa hatua hizo muhimu.

Aidha, Waziri Gavu alimueleza kiongozi huyo juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutekeleza makubaliano yaliofikiwa sambamba na kusisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo hasa ikizingatiwa kuwa Morocco ni miongoni mwa nchi za Bara la Afrika iliyopiga hatua kubwa katika sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya utalii.

Sambamba na hayo, Waziri Gavu alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji wa Morocco kuja kuekeza Zanzibar katika sekta mbali mbali ikiwemo sekta ya uvuvi hasa wa bahari kuu na kumueleza balozi huyo wa Morocco haja ya kuitangaza Zanzibar nchini mwake kiutalii.

Nae Balozi wa Ufalme wa Morocco katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Abdelilah Benryane alieleza kuwa Morocco inajivunia uhusiano na ushirikiano mwema uliopo kati yake na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Balozi Benryane alisema kuwa Morocco iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo na kumuhakikishia Waziri Gavu pamoja na viongozi wengine wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa nchi yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Pamoja na hayo, Balozi huyo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa juhudi za makusudi atazichukua katika kuhakikisha anajenga mashirikiano mazuri nchini mwake kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano na Zanzibar katika sekta muhimu za maendeleo zikiwemo elimu, afya, kilimo, uvuvi, utalii na nyenginezo

Morocco imepiga hatua kubwa katika sekta ya utalii ambapo hivi sasa inapokea watalii milioni 16 kwa mwaka kufuatia program ijulikanayo ‘Azur Blue’ iliyoanzishwa na kiongozi wa nchi hiyo Mfalme Momamed VI ambapo pia, katika programu ya pili wamejiwekea hadi kufikia mwaka 2020 watapokea watalii wapatao milioni 20.

Hivyo, kuwepo kwa mashirikiano na uhusiano kati ya Zanzibar na nchi hiyo hasa katika sekta ya Utalii ambapo Zanzibar nayo imo katika mikakati ya kuiimarisha sekta hiyo sambamba na mafanikio na kuwepo wka vivutio vingi hapa nchini kutasaidia kuitangaza Zanzibar kiutalii.

Mkutano huo umeweza kuzungumzia masuala mbali mbali ya kuimarisha uhusiano kati ya Morocco na Zanzibar ambapo ujumbe kutoka nchini Morocco unatarajiwa kuzuru Zanzibar mapema mwakani ikiwa ni katika kutekeleza ushirikiano baina ya pande mbili hizo.

Mkutano huo pia, ulihudhuriwa na Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa Mshauri wa Rais, Ushirikiano wa Kimataifa, Fedha na Uchumi, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Salum Maulid na Mohamed MA Elainine kutoka Ubalozi wa Morocco, Dar-es-Salaam nchini Tanzania.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449.  Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.