Habari za Punde

Rais Dk Shein atuma salamu za rambirambi vifo vya wanajeshi 14 nchini Kongo



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Dodoma                                                                  11.12.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amemtumia salamu za rambi rambi Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dk. Hussein Ali Mwinyi kufuatia vifo vya wanajeshi 14 wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania vilivyotokea tarehe 7 Disemba, 2017 katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambako walikuwa katika shughuli za kusimamia amani.

Katika salamu hizo za rambirambi Dk. Shein alimueleza Waziri Dk. Hussen Mwinyi kuwa  amepokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa hiyo ya vifo vya wanajeshi wa Jeshi la Wananachi wa Tanzania vilivyotokea tarehe 7 Disemba, 2017 katika Jamhuri ya Kongo.

Kuufuatia tukio hilo Rais wa Zanzibar alieleza kwua yeye binafsi, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wote wa Zanzibar wanawakumbuka wanajeshi hao kwa ujasiri na uzalendo wao katika kuhakikisha amani inapatikana katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na maeneo yote ya Maziwa Makuu.

Aidha salamu hizo za rambirambi Dk. Shein alizitoa kwa Dk. Hussein Ali Hassan  Mwinyi, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa pamoja na  Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, familia za marehemu, ndugu, jamaa na marafiki pamoja na wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutokana na msiba huo.

Salamu hizo zilimuomba MwenyeziMungu awape malazi mema mashujaa hao pamoja na kuwaombea wanajeshi waliojeruhiwa wapate nafuu ya haraka na kurejea katika hali zao za kawaida.

Sambamba na hayo, salamu hizo za rambirambi zilimuomba MwenyeziMungu awape Watanzania wote moyo wa subira na uvumilivu katika kiipndi hiki kigumu cha msiba huu.

Tukio hilo limetoa katika Kambi ndogo ya Semuliki iliyopo Kaskazini Mashariki mwa Wilaya ya  Beni katika Jimbo la Kivu baada ya kuvamiwa na waaasi wa kundi la ADF katika eneo hilo la Mashariki mwa nchi hiyo ya Kongo.

Tukio hilo limeelezwa kuwa ni baya zaidi kuwahi kutokea kutekelezwa na waasi dhidi ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa (UN) katika historia ya miaka ya hivi karibuni.

Katika kipindi cha miezi sita tukio hili ni la pili kutokea baada ya Oktoba mwaka huu wanajeshi wawili wa JWTZ waliokuwa katika kundi la walinda amani kuripotiwa kuuwawa na wengine 18 kujeruhiwa.

Mbali na hao askari wengine wawili pia, waliripotiwa kuuawa mwezi Mei 2015 katika eneo la Kivu Mashariki mwa Kongo na mwengine wawili hawakujulikana  walipo baada ya kuvamiwa na waaasi.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  (UN) Antonio Guterres alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kulaani vikali shambulio hilo ambalo halijawahi kutokea tokea JWTZ lianze kushiriki ulinzi wa amani nchini DRC mwaka 2011.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.