Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Shein Aipongeza Zanzibar Heroes Kwa Kuipatia Zanzibar Heshima Kwa Kuonesha Kiwango Safi cha Soka.


RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameendelea kutoa pongezi kwa timu ya Taifa ya Zanzibar, ‘Zanzibar Heroes’ kwa kuirudishia Zanzibar heshima yake na sasa imekuwa inasemwa vizuri kutokana na jinsi timu hiyo ilivyoonesha kiwango safi cha kusakata soka.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar katika chakula maalum cha mchana alichowaandalia wachezaji wa Timu ya Zanzibar Heroes pamoja na viongozi wake wote baada ya kufanya vyema katika mashindano ya mwaka huu ya Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati ‘CECAFA’ yaliofanyika nchini Kenya.

Katika hotuba yake fupi kwenye hafla hiyo, iliyohudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali,akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, viongozi wa ZFA na waalikwa wengine, Dk. Shein alieleza kuwa vijana hao wa ‘Zanzibar Heroes’ pamoja na kocha wao mkuu wa timu hiyo wamefanya kazi nzuri na ya kupongeza hatua ambayo itaendelea kuipa heshima kubwa Zanzibar.

Aliongeza kuwa wachezaji hao wa ‘Zanzibar Heroes’ wamewanawa uso Wazanzibari wote kutokana na uwezo na nguvu ya mpira waliouonesha na hadi kufikia fainali za mashindano hayo ya CECAFA.

Dk. Shein alieleza kuwa watu waliowengi hawakuifikiria timu hiyo ya Zanzibar kama itafika ilipofika na pia baadhi ya watu hawakuwa wakiisema vizuri lakini hatimae imedhihirisha kuwa Zanzibar ina historia nzuri ya soka na kuondosha usemi kuwa ‘Chenga twawala’.

“Lazima watambue kuwa wakiona vyaelea wajue kama vimeundwa kwani wachezaji wetu hawa wamefanya kazi kubwa na wameiletea heshima kubwa Zanzibar na hivi sasa Zanzibar inasemwa vizuri kunzia tarehe 17 hadi leo”,alisema Dk. Shein.

“Watu walikuwa wanaulizana ndio wale hawa tunaowajua au... kocha mkuu hajatuambia siri yake na wala asituambie kwani amefanya kazi kubwa”,alisema Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa haikuwa bahati kwa timu hiyo ya Zanzibar Heroes kupata kombe la ushindi wa mwanzo lakini jitihada kubwa walizifanya wachezaji hao na kuwapelekea Wazanzibar na Watanzania wote kwa jumla kufurahi.

Alieleza kuwa Zanzibar imeshawahi kuchukua vikombe vingi katika mashindano mengi ya siku za nyuma tokea kombe la Goseji, hivyo, haikuwa bahati kwa mwaka hu kupata ushindi huo licha ya juhudi hizo kubwa zilizochukuliwa na vijana hao mahiri.

Dk. Shein ambaye yeye mwenyewe ni mpenda michezo na aliwahi kuwa mwanamichezo maarufu hapa nchini hapo siku za nyuma alieleza kuwa hamasa na bidii za wachezaji hao pamoja na kocha wao mkuu zimesaidia kwa kiasi kikubwa na kuipelekea timu hiyo kuwa tishio katika mashindano hayo.

Dk. Shein alieleza jinsi alivyotoa salamu zake za pongezi kwa timu hiyo baada ya kuingia fainali ya kombe hilo na baada ya kumalizika kwa mashindano hayo na hatimae timu hiyo kuibuka kuwa mshindi wa pili.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa kuwaandalia chakula hicho cha mchana hivi leo ni mwanzo tu wa pongezi zake lakini kuna zawadi tatu kubwa amewaandalia ikianzia taarab maalum ya kikundi cha Taifa cha Zanzibar pamoja na zawadi nyengine mbili kubwa ambazo hazijawahi kutokea na kukataa kuzitaja hii leo na kuahidi kuzitaja hapo kesho atakapozitoa.

“Hii leo ni bashrafu tu, mchezo kamili utakuwa hapo kesho tukijaaliwa usiku na tumeamua kufanya hivi kwa mapenzi makubwa na furaha kwa timu yetu hii”,alisema Dk. Shein huku akisisitiza kuwa taarab hiyo ya kikundi cha Taifa huwa ni taarab maalum kwa watu maalum na kwa wakati maalum.

Nae Kocha Mkuu wa Zanzibar Heroes Hemed Suleiman Moroko alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein pamoja na kwa viongozi wengine wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kocha Abdulkhani Msoma pamoja na Mwalimu Abdalla Mwinyi kutokana na nasaha zake za kutaka wachezaji wawe na silka na hulka za Kizanzibari wakiwa katika mashindano hayo ambazo ndizo zilizowasaidia.

Moroko aliongeza kuwa kilichompa ari ya ushindi huo walioupata ni kutokana na kuwa anajua Rais wa Zanzibar amecheza mpira na anaujua mpira hivyo alihakikisha kuwa hamuangushi Rais pamoja na Wazanzibari wote.

Pamoja na hayo, Kocha mkuu huyo alitoa ombi maalum kwa Rais Dk. Shein kumualika Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika Ahmad Ahmad kuja Zanzibar ili kufanya mazungumzo nae kwa ajili ya kuzungumza mustakbali wa Zanzibar katika soka kimataifa.

Timu ya mpira wa miguu ya Zanzibar Heroes  imefanikiwa kushika nafasi ya pili ya michuano hiyo ya ‘CECAFA’ baada ya kupata matokeo ya kufungwa magoli 3-2 kwa changamoto ya mikwaju ya penanti baada ya kwenda sare ya goli 2-2 kwa dakika 12 na timu ya Taifa ya Kenya.

Baada ya matokeo na ushindi huo sambamba na juhudi kubwa zilizofanywa na timu hiyo, mapokezi makubwa ya kihistoria yalifanywa hapa Zanzibar na wananchi kutoka maeneo mbali mbali waliipokea timu hiyo huku pongezi kutoka kwa viongozi na wananchi zikitolewa, ambapo Dk. Shein akiwa Mkoani Dodoma alitoa pongezi zake kwa timu hiyo na hvi leo amewaandalia chakula cha mchana na kesho atawaandalia tafrija maalum itakayoendana na Taarab ya kikundi cha Taifa cha Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.