RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameendelea kutoa
pongezi kwa timu ya Taifa ya Zanzibar, ‘Zanzibar Heroes’ kwa kuirudishia
Zanzibar heshima yake na sasa imekuwa inasemwa vizuri kutokana na jinsi timu
hiyo ilivyoonesha kiwango safi cha kusakata soka.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo huko katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar katika chakula maalum cha
mchana alichowaandalia wachezaji wa Timu ya Zanzibar Heroes pamoja na viongozi
wake wote baada ya kufanya vyema katika mashindano ya mwaka huu ya Vyama vya
Soka Afrika Mashariki na Kati ‘CECAFA’ yaliofanyika nchini Kenya.
Katika hotuba yake
fupi kwenye hafla hiyo, iliyohudhuriwa na viongozi mbali mbali wa
Serikali,akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, viongozi wa ZFA na
waalikwa wengine, Dk. Shein alieleza kuwa vijana hao wa ‘Zanzibar Heroes’
pamoja na kocha wao mkuu wa timu hiyo wamefanya kazi nzuri na ya kupongeza
hatua ambayo itaendelea kuipa heshima kubwa Zanzibar.
Aliongeza kuwa
wachezaji hao wa ‘Zanzibar Heroes’ wamewanawa uso Wazanzibari wote kutokana na
uwezo na nguvu ya mpira waliouonesha na hadi kufikia fainali za mashindano hayo
ya CECAFA.
Dk. Shein alieleza
kuwa watu waliowengi hawakuifikiria timu hiyo ya Zanzibar kama itafika
ilipofika na pia baadhi ya watu hawakuwa wakiisema vizuri lakini hatimae
imedhihirisha kuwa Zanzibar ina historia nzuri ya soka na kuondosha usemi kuwa
‘Chenga twawala’.
“Lazima watambue kuwa
wakiona vyaelea wajue kama vimeundwa kwani wachezaji wetu hawa wamefanya kazi
kubwa na wameiletea heshima kubwa Zanzibar na hivi sasa Zanzibar inasemwa
vizuri kunzia tarehe 17 hadi leo”,alisema Dk. Shein.
“Watu walikuwa
wanaulizana ndio wale hawa tunaowajua au... kocha mkuu hajatuambia siri yake na
wala asituambie kwani amefanya kazi kubwa”,alisema Dk. Shein.
Rais Dk. Shein
alieleza kuwa haikuwa bahati kwa timu hiyo ya Zanzibar Heroes kupata kombe la
ushindi wa mwanzo lakini jitihada kubwa walizifanya wachezaji hao na
kuwapelekea Wazanzibar na Watanzania wote kwa jumla kufurahi.
Alieleza kuwa Zanzibar
imeshawahi kuchukua vikombe vingi katika mashindano mengi ya siku za nyuma
tokea kombe la Goseji, hivyo, haikuwa bahati kwa mwaka hu kupata ushindi huo
licha ya juhudi hizo kubwa zilizochukuliwa na vijana hao mahiri.
Dk. Shein ambaye yeye
mwenyewe ni mpenda michezo na aliwahi kuwa mwanamichezo maarufu hapa nchini
hapo siku za nyuma alieleza kuwa hamasa na bidii za wachezaji hao pamoja na
kocha wao mkuu zimesaidia kwa kiasi kikubwa na kuipelekea timu hiyo kuwa tishio
katika mashindano hayo.
Dk. Shein alieleza
jinsi alivyotoa salamu zake za pongezi kwa timu hiyo baada ya kuingia fainali
ya kombe hilo na baada ya kumalizika kwa mashindano hayo na hatimae timu hiyo
kuibuka kuwa mshindi wa pili.
Aidha, Dk. Shein
alieleza kuwa kuwaandalia chakula hicho cha mchana hivi leo ni mwanzo tu wa
pongezi zake lakini kuna zawadi tatu kubwa amewaandalia ikianzia taarab maalum
ya kikundi cha Taifa cha Zanzibar pamoja na zawadi nyengine mbili kubwa ambazo hazijawahi
kutokea na kukataa kuzitaja hii leo na kuahidi kuzitaja hapo kesho atakapozitoa.
“Hii leo ni bashrafu
tu, mchezo kamili utakuwa hapo kesho tukijaaliwa usiku na tumeamua kufanya hivi
kwa mapenzi makubwa na furaha kwa timu yetu hii”,alisema Dk. Shein huku
akisisitiza kuwa taarab hiyo ya kikundi cha Taifa huwa ni taarab maalum kwa
watu maalum na kwa wakati maalum.
Nae Kocha Mkuu wa
Zanzibar Heroes Hemed Suleiman Moroko alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein pamoja
na kwa viongozi wengine wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kocha Abdulkhani
Msoma pamoja na Mwalimu Abdalla Mwinyi kutokana na nasaha zake za kutaka
wachezaji wawe na silka na hulka za Kizanzibari wakiwa katika mashindano hayo
ambazo ndizo zilizowasaidia.
Moroko aliongeza kuwa
kilichompa ari ya ushindi huo walioupata ni kutokana na kuwa anajua Rais wa
Zanzibar amecheza mpira na anaujua mpira hivyo alihakikisha kuwa hamuangushi
Rais pamoja na Wazanzibari wote.
Pamoja na hayo, Kocha
mkuu huyo alitoa ombi maalum kwa Rais Dk. Shein kumualika Rais wa Shirikisho la
Soka Barani Afrika Ahmad Ahmad kuja Zanzibar ili kufanya mazungumzo nae kwa
ajili ya kuzungumza mustakbali wa Zanzibar katika soka kimataifa.
Timu ya mpira wa miguu
ya Zanzibar Heroes imefanikiwa kushika
nafasi ya pili ya michuano hiyo ya ‘CECAFA’ baada ya kupata matokeo ya kufungwa
magoli 3-2 kwa changamoto ya mikwaju ya penanti baada ya kwenda sare ya goli
2-2 kwa dakika 12 na timu ya Taifa ya Kenya.
Baada ya matokeo na
ushindi huo sambamba na juhudi kubwa zilizofanywa na timu hiyo, mapokezi
makubwa ya kihistoria yalifanywa hapa Zanzibar na wananchi kutoka maeneo mbali
mbali waliipokea timu hiyo huku pongezi kutoka kwa viongozi na wananchi
zikitolewa, ambapo Dk. Shein akiwa Mkoani Dodoma alitoa pongezi zake kwa timu
hiyo na hvi leo amewaandalia chakula cha mchana na kesho atawaandalia tafrija
maalum itakayoendana na Taarab ya kikundi cha Taifa cha Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment