HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA
MAPINDUZI, MHE. DK. ALI
MOHAMED SHEIN, KATIKA KILELE CHA SHEREHE ZA MAADHIMISHO YA MIAKA 54
YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR, UWANJA WA AMAAN
TAREHE:
12 JANUARI, 2018
Mheshimiwa
Dk. John Pombe Joseph Magufuli;
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan;
Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa;
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi;
Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar,
Waheshimiwa Marais Wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Waheshimiwa Viongozi Wakuu Wastaafu Mliohudhuria,
Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Mheshimiwa Job Ndugai;
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid;
Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar,
Mheshimiwa Profesa Ibrahim Khamisi Juma,
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu,
Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya
Kimataifa,
Mheshimiwa Ayoub Mohamed Mahmoud;
Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi,
Waheshimiwa Viongozi mbali mbali wa Serikali na Vyama
vya
Siasa Mliohudhuria,
Ndugu Wananchi,
Mabibi na Mabwana,
Assalamu Aleikum
Kwa unyenyekevu
mkubwa namshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba Mbingu na Ardhi na vyote viliomo ndani
yake, kwa kutujaalia uhai na afya njema na tukaweza kukusanyika hapa hivi leo,
kwa ajili ya kuadhimisha miaka 54 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, ya tarehe
12 Januari, 1964.
Kwa niaba ya
Wananchi wa Zanzibar, natoa shukurani zangu za dhati, kwako Mheshimiwa Dkt.
John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa
kuungana nasi katika sherehe hizi.
Kadhalika, natoa shukurani zangu za dhati kwa viongozi wote wa Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
waliopo madarakani na waliostaafu kwa kuhudhuria kwenu. Vile vile,
nawashukuru Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa, Viongozi
wa dini na vyama vya siasa na wananchi wote kwa kuhudhuria kwa wingi katika
sherehe hizi muhimu na adhimu. Ahsanteni
sana kwa mahudhurio yenu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Leo ni siku
muhimu sana katika historia ya wananchi wa Zanzibar, ambapo miaka 54 iliyopita,
waliikata minyororo ya utawala wa kisultani na vibaraka vyao. Wananchi wa Zanzibar, walikataa madhila
makubwa ya kutawaliwa waliyotendewa na utawala wa Kisultani, wakoloni,
mabwanyenye na mabepari ya kunyimwa haki zao za msingi katika kuendesha maisha
yao. Walibaguliwa katika kupata huduma
za afya, elimu, fursa za kuitumia ardhi yao, walinyimwa fursa za kazi zenye
staha na heshima ya mwanadamu, walinyimwa makaazi bora, walidhulumiwa mashamba
yao na kukosa nafasi ya kuendesha maisha yao na kadhalika. Kwa lengo la kukabiliana na uonevu huo, Chama
cha Afro-Shirazi kilichoongozwa na Rais wake Marehemu Mzee Abeid Amani Karume,
kilivinjari na kilisimama imara kwa ajili ya kuwakomboa wanyonge wafanyakazi na
wakulima wa Zanzibar.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Leo
tunapoadhimisha sherehe za Mapinduzi kwa kutimiza miaka 54, hatuna budi
kuwakumbuka na kuwashukuru wazee wetu waasisi wa Chama cha Afro-Shirazi,
walioongozwa na Rais wake wa Kwanza Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, kwa
ushujaa wao wa kuzipigania haki zetu, kuleta usawa na maelewano na kuondosha
kila aina ya pingamizi walizokuwa wakizipata wananchi wa Unguja na Pemba. Leo
ni siku ya kumbukumbu ya ushindi wa wananchi wa Zanzibar na kwamba Mapinduzi
yaliuinua na yaliusimamisha utawala wa wanyonge, wakulima na wafanyakazi; yaliweka usawa na
kuwakabidhi tena wafanyakazi na wakulima wa Zanzibar, heshima yao na utu wao,
katika nchi yao.
Namuomba
Mwenyezi Mungu amrehemu Jemadari wa Mapinduzi yetu Matukufu ya tarehe 12
Januari, 1964, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, pamoja na waasisi wengine wa
Mapinduzi hayo, waliotangulia mbele ya haki,
awabariki na awaweke mahali pema peponi, Amin. Kwa wale waliohai, Mwenyezi Mungu awape umri
mrefu na afya njema. Siku zote
tutawakumbuka, tutawaenzi, tutawashukuru na tutawaombea dua kwa kujitolea kwao
muhanga kwa ajili ya kutukomboa. Kutokana na jitihada zao na mapenzi kwa nchi
yao, hivi sasa tupo huru na tutaendelea kuwa huru wakati wote.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Leo tunafikia
kilele cha Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 54 ya Mapinduzi ya tarehe 12
Januari, 1964, tukiwa na furaha kubwa na kusherehekea kwa vifijo na hoi hoi,
kama tulivyojionea wenyewe hapa uwanja wa Amaan. Pamoja na hayo, sherehe hizi zinatukumbusha
umuhimu wa kuendelea kuyalinda, kuyatetea na kuyadumisha Mapinduzi yetu, kama
tulivyofanya katika miaka iliyopita kwa mafanikio makubwa.
Vile vile,
tunasherehekea umoja wetu uliotokana na Muungano wa nchi mbili zilizokuwa huru;
Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na kuzaliwa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, tarehe 26 Aprili, 1964.
Muungano wetu ulianzishwa
kutokana na sera sahihi za vyama viasisi
vya TANU na ASP na sasa CCM pamoja na uongozi bora na thabiti wa waasisi wa
nchi yetu Marehemu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Marehemu Mzee Abeid
Amani Karume na viongozi wa awamu nyengine waliofuata baadae.
Katika kipindi
hiki cha miaka 54 ya Mapinduzi,
tunasherehekea kuwepo kwa hali ya amani, umoja na maendeleo makubwa
yaliyopatikana. Tuna wajibu mkubwa wa
kuuenzi na kuuendeleza umoja na mshikamano wetu, ambao ndio siri kubwa ya
kuendelea kuwepo kwa hali ya amani na utulivu yenye kuimarisha maendeleo
yetu.
Nnafarijika
sana kuona wananchi wa Zanzibar wameungana na Serikali yao katika kipindi cha
miaka 54, kwa kuyatekeleza malengo ya Mapinduzi yetu na kupatikana maendeleo ya
kisiasa, kiuchumi na kijamii. Kwa hakika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
imeweza kuyatekeleza na kuyaendeleza malengo ya Mapinduzi kwa ufanisi
mkubwa.
Mafanikio
yaliyopatikana katika Awamu zote Saba, ni ushahidi ulio wazi unaodhihirisha
kuwa katika miaka 54 iliyopita, tumeweza kufanya mambo mengi kwa mafanikio na
ni haki ya kila mmoja wetu kujivunia mafanikio hayo na kuyaendeleza kwa manufaa
yetu na vizazi vya baadae.
Katika sherehe
za mwaka huu, jumla ya miradi ya maendeleo 33 mbali mbali ilizinduliwa na
miradi 15 iliwekewa mawe ya msingi, Unguja na Pemba. Ufunguzi na uwekaji wa mawe ya msingi ya
miradi hio inahusisha Umeme, Masoko, Barabara, Majengo ya Idara ya Serikali,
Vituo vya Afya, Studio ya Televisheni, Skuli, Tamasha la Biashara na kadhalika.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Katika mwaka
huu wa tatu, wa kipindi cha pili 2017/2018, cha Awamu ya Saba, Serikali
imetekeleza vizuri Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020, MKUZA III
na Dira ya Maendeleo 2020 na kupata mafanikio ya kuridhisha.
Juhudi kubwa
zilizochukuliwa na Serikali katika kuimarisha uchumi zimewezesha kuongezeka kwa
ukusanyaji wa mapato. Jumla ya TZS.
bilioni 548.571 zilikusanywa katika
mwaka 2017 ikilinganishwa na TZS. bilioni
487.474 zilizokusanywa katika mwaka 2016. Katika mwaka 2017, mapato
yameongezeka kwa TZS bilioni 61.097, ikilinganishwa
na makusanyo ya kipindi cha mwaka 2016, ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia
12.5. Natoa pongezi kwa Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) na Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB), kwa juhudi zao katika
ukusanyaji wa mapato. Kwa upande mwengine, Pato la Taifa limeongezeka kutoka
thamani ya TZS. bilioni 2,308 mwaka 2015 na kufikia thamani ya TZS. bilioni
2,628 kwa mwaka 2016. Pato hii
lilikadiriwa kufikia TZS. bilioni 2,827, mwaka 2017, kwa bei za soko. Katika
jitihada tulizoanza kuzichukua mwaka 2011/2012, hivi sasa, utegemezi wa bajeti
yetu kwa mwaka 2017/2018, umefikia asilimia 7.3, ikilinganishwa na asilimia
30.2 katika mwaka 2010/2011. Mafanikio
haya tuliyopata ni makubwa na ya kupigiwa mfano.
Kasi ya ukuaji
wa uchumi wetu kwa bei halisi, imekua kwa asilimia 7.0 kwa mwaka 2017, ikilinganishwa
na asilimia 6.8 kwa mwaka 2016. Aidha, Pato la Mtu Binafsi nalo
limeongezeka na kufikia TZS. 1,806,000
ikilinganishwa na TZS 1,632,000 kwa mwaka 2015. Kasi ya mfumko wa bei ilifikia asilimia 5.6
katika mwaka 2017 kutoka asilimia 6.7 mwaka 2016. Lengo letu ni kuimarisha
uchumi, kupunguza umasikini na kuifanya Zanzibar kuwa miongoni mwa nchi zenye
uchumi wa kiwango cha kati ifikapo mwaka 2020.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Katika kipindi
cha Januari hadi Septemba, 2017 jumla ya miradi 25 iliyopangwa kuingiza mtaji
wa US$ milioni 276.84 iliidhinishwa na Serikali. Miradi hii itakapokamilika
inategemewa kutoa ajira zisizopungua
915. Katika mwaka 2017, ujenzi wa mji mpya wa kisasa wa Fumba na Nyamanzi imeendelezwa,
kwa lengo la kuimarisha maisha ya
wananchi na kubadilisha taswira ya Zanzibar.
Jumla ya nyumba 170 zimejengwa katika Mradi wa ujenzi wa “Fumba
Satellite City” na nyumba 60 katika Mradi wa “Fumba Town Development”,
Nyamanzi.
Kadhalika,
mradi wa nyumba za kisasa katika eneo la Mbweni
unaotekelezwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) wa ujenzi wa
majengo 18 yenye urefu wa ghorofa 7 unatarajiwa kukamilika, hivi karibuni. Vile vile,
mradi wa ujenzi wa hoteli ya
kisasa ‘Verde’ ya nyota tano,
inayojengwa huko Mtoni Unguja ambao unaotekelezwa na Kampuni ya SS Bakhressa,
umekamilika. Hatua inayofuata ni ya uwekaji wa samani. Mradi huu unatarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni.
Uimarishaji wa
miji yetu umeendelezwa kupitia mradi mkubwa wa Huduma za Jamii Mijini (Zanzibar
Urban Services Project - ZUSP). Awamu ya kwanza ya Mradi huu, imeshatekelezwa
kwa mkopo wa US$ milioni 38 kutoka Benki ya Dunia ambapo ulijumuisha ujenzi wa
miundombinu mbali mbali, ikiwemo misingi ya maji, uwanja wa Mnazi Mmoja,
majengo, ununuzi wa magari kwa Unguja na Pemba na ujenzi wa ukuta unaolikinga eneo la Forodhani lisiathiriwe na
bahari. Ujenzi wa Awamu ya pili ya mradi huu umeshatayarishwa
na Benki ya Dunia imekubali kutoa mkopo wa US$ milioni 55.
Huduma za jamii
zimeimarishwa kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF). Jumla ya kaya 32,478 zimepatiwa TZS bilioni
4.45 katika utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kupitia TASAF III. Vile vile, TASAF III imetekeleza miradi ya
kutoa ajira za muda kwa kaya 27,044 Unguja na Pemba.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Sekta ya utalii
imeendelea kuimarika, ambapo
jumla ya watalii 433,116 waliingia nchini katika mwaka 2017, ikilinganishwa na
idadi ya watalii 379,242 walioingia nchini katika mwaka 2016. Hili ni ongezeko la asilimia 14.2, kwa
kipindi cha mwaka mmoja. Kuongezeka kwa
idadi ya watalii wanaoingia nchini, kunaonesha wazi kwamba lengo la kufikia
watalii 500,000 ifikapo mwaka 2020, litafikiwa kabla ya mwaka huo.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Kwa upande wa
biashara, jumla ya bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni 145.76, zilisafirishwa
kwenda nje ya nchi, mwaka 2017, ikilinganishwa na bidhaa zenye thamani ya TZS
bilioni 94.94, mwaka 2016. Bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni 211.42,
ziliingizwa nchini kutoka nje ya nchi, ikilinganishwa na bidhaa zenye thamani
ya TZS bilioni 167.09 zilizoingizwa mwaka 2016.
Biashara kati ya Zanzibar na Tanzania Bara inaendelea vizuri, ambapo
bidhaa zenye thamani ya TZS billioni 32.32 zilisafirishwa kwenda Tanzania Bara
na bidhaa zenye thamani ya TZS bilioni
184.84, zilisafirishwa kutoka Tanzania Bara kuja Zanzibar katika kipindi cha Januari hadi Disemba, 2017.
Juhudi za
Serikali za kufufua zao la karafuu zinaendelea kupata mafanikio mazuri. Hadi kufikia tarehe 5 Januari, 2018, jumla
ya tani 8,182.04 za karafuu zenye
thamani ya TZS bilioni 114.17 zilikuwa zimenunuliwa kutoka kwa wakulima, katika
mwaka wa fedha 2017/2018. Kwa upande wa
mauzo, katika msimu wa mwaka 2017/2018, Serikali imeshauza jumla ya tani 5,881
zenye thamani ya TZS bilioni
103.49. Uamuzi wa kuwalipa wakulima
asilimia 80 ya bei ya soko la dunia unaendelezwa. Mwaka huu ni wa sita mfululizo ambapo
Serikali inanunua karafuu kwa wakulima
kwa bei ya TZS. 14,000 kwa kilo moja.
Nawashukuru
wakulima wa karafuu kwa kuziuza karafuu zao katika Shirika la ZSTC. Navipongeza vikosi vya Ulinzi na Usalama na
Idara Maalum za SMZ kwa kuyadhibiti magendo ya karafuu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Mchango wa
sekta ya viwanda, katika Pato la Taifa umefikia TZS. bilioni 487.9 kwa mwaka
2016, ikilinganishwa na TZS. bilioni 417.0 mwaka 2015. Hili ni ongezeko la asilimia 17
ikilinganishwa na mwaka 2015. Kadhalika,
mchango wa sekta ya viwanda katika jumla ya Pato la Taifa umeongezeka kutoka
asilimia 18.1 mwaka 2015 hadi asilimia 18.6 mwaka 2016.
Mamlaka ya
Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) imeshaidhinisha ujenzi wa viwanda
vinne, katika eneo la Viwanda Vidogo Vidogo Amani pamoja na Maruhubi. Viwanda hivyo vinajumuisha, Kiwanda cha
Mafuta ya Nazi, Kiwanda cha Mafuta ya Kupikia pamoja na Kiwanda cha Vipodozi,
Kadhalika, ujenzi wa viwanda vitatu vipya vitakavyojengwa huko Fumba
umeshaidhinishwa na ZIPA. Serikali itaendelea na juhudi za kushajihisha
wawekezaji wa ndani na nje, kuja kuwekeza katika sekta ya viwanda.
Serikali
kupitia Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS) imeendelea kuchukua hatua za
kudhibiti ubora wa bidhaa mbali mbali zinazotengenezwa au kuingizwa Zanzibar
kwa ajili ya matumizi ya wananchi. Jumla
ya viwango 143 vimetangazwa kupitia Gazeti Rasmi la Serikali na
vinatumika. Hadi mwezi Disemba 2017,
jumla ya bidhaa 12 zimepatiwa cheti cha matumizi ya alama ya ZBS. Ujenzi wa Ofisi na maabara za ZBS
unaendelea katika eneo la Maruhubi.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Katika kipindi
cha miaka 54 ya Mapinduzi tunajivunia kuimarika kwa huduma za elimu ambapo kabla ya Mapinduzi ya 1964, zilikuwa chache,
zikitolewa kwa ubaguzi na zilikuwa za kulipia.
Hivi leo, skuli
za msingi zimeongezeka mara saba, skuli za sekondari zimeongezeka mara 53 na
idadi ya wanafunzi wa skuli za Msingi na Sekondari imeongezeka mara 14, kutoka
wanafunzi 25,372 mwaka 1963 hadi wanafunzi 378,211 mwaka 2017. Tatizo
walilotutengenezea wakoloni kwamba watoto wa wafanyakazi na wakulima tusiingie
sekondari na kupata elimu ya juu, leo halipo tena. Haya ni mafanikio makubwa ya
kupigiwa mfano.
Katika jitihada
ya kuongeza madarasa, mwaka 2017, Serikali ilianza ujenzi wa skuli 9 za ghorofa
za sekondari kwa Unguja na Pemba, ambapo ujenzi wake, pamoja na vituo vya mafunzo ya amali kwa Mkoa
wa Kusini Unguja na Mkoa wa Kaskazini Pemba unaendelea. Aidha, ujenzi wa jengo jipya katika Taasisi ya
Karume ya Sayansi na Teknolojia umefikia asimilia 85.
Pamoja na hatua
hizo, Serikali inaendelea kulishughulikia suala la ununuzi wa madawati yote kwa
ajili ya skuli zote za Unguja na Pemba.
Kutokana na hatua maalum tunazozichukua za kukusanya fedha,
tunatarajia tatizo la upungufu wa madawati, litamalizika mwaka huu. Kuanzia mwezi wa Julai, 2018 Serikali itaanza
kutekeleza azma ya kurudisha utaratibu wa kutoa elimu bure katika skuli za
sekondari, ili kutekeleza lengo la Mapinduzi.
Kwa hivyo, elimu ya Msingi hadi Sekondari itatolewa tena, bure, bila ya malipo.Hapatakuwa
na mzee hata mmoja atakaetakiwa kulipa na mzigo wote utabwebwa na Serikali.
Mipango yetu ya
elimu imepata mafanikio makubwa ambapo sasa
Zanzibar inavyo Vyuo Vikuu Vitatu
vinavyoendeshwa na wataalamu wetu wenyewe. Kiasi cha wanafunzi 1,800 wa
fani mbali mbali wanahitimu kwenye Vyuo Vikuu vya Zanzibar, kila mwaka. Kwa
hivyo, Zanzibar itajitosheleza kwa kuwa na wataalamu wake wenyewe hivi
karibuni.
Ndugu Viongozi na Ndugu Wananchi,
Juhudi kubwa na
za makusudi zinaendelea kuchukuliwa katika kuziimarisha huduma za afya. Sera
mpya ya Afya ya mwaka 2014 inatekelezwa katika kuwapa wananchi huduma za afya
bila ya malipo kutokana na malengo ya Mapinduzi. Hivi sasa huduma za afya
zinatolewa katika hospitali za Serikali 12, badala ya hospitali 5 na vituo vya
afya 158, badala ya 36 vilivyokuwepo kabla ya Mapinduzi. Vile vile, huduma za afya zinatolewa na
hospitali za vyombo vya Ulinzi na Usalama pamoja na Idara Maalum za SMZ, mpango
ambao kabla ya Mapinduzi haukuwepo.
Kutokana na
upungufu wa madaktari mabingwa, madaktari na wataalamu wengine wa fani ya afya,
Serikali imefanya jitihada maalum za
kuwasomesha madaktari na wataalamu mbali mbali wa sekta ya afya. Hadi mwishoni mwa mwaka 2017, jumla ya
madaktari 46 wanasomea masomo ya Uzamili ya Udaktari bingwa, wanafunzi 340 wanasoma Shahada ya Kwanza ya Udaktari, miongoni mwao,
195 wanasoma katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA). Kadhalika, wanafunzi 1,416 wanasomea fani
mbali mbali za afya katika kiwango cha Shahada na Stashahada katika vyuo
tofauti vya ndani na nje ya nchi.
Ndugu Viongozi na Ndugu Wananchi,
Idadi ya
madaktari wanaotoa huduma katika hospitali na vituo vya afya, Unguja na Pemba,
imeimarika sana. Hivi sasa, daktari mmoja
anatoa huduma kwa watu Elfu nane
mia tano na tisiini na mbili (I:8592),.
Kutokana na kuongezeka kwa idadi ya
madaktari na wafanyakazi wa fani mbali mbali, kupanuka kwa huduma za tiba na
kinga na kuongezeka majengo ya kutolea huduma; mafanikio makubwa yamepatikana. Vifo vya akinamama wanaojifungua vimepungua
kutoka 237/100,000 mwaka 2016 mpaka 195/100,000 mwaka 2017. Vifo vya watoto wachanga, navyo vimepungua
kutoka 54/1,000, mwaka 2010/2011 hadi 43/1,000, mwaka 2016/2017.
Kuhusu UKIMWI,
pamoja na mafanikio tuliyoyapata, katika kupambana na maambukizo mapya ya
virusi vya UKIMWI, mipango madhubuti imeandaliwa katika kukabiliana na maradhi
hayo thakili. Kwa hivyo, tatizo la
UKIMWI bado lipo, ambapo inakadiriwa Zanzibar hivi sasa ina watu wanaoishi na
virusi vya UKIMWI, ikiwa ni asilimia 0.4 ya watu wote wa Zanzibar. Mapambano dhidi ya maambukizo mapya
yanahitaji jitihada za kila mmoja wetu.
Kadhalika,
kiwango cha malaria na kasi ya kuenea kwake, kimeendelea kudhibitiwa na
kimeendelea kubaki asilimia 0.4 kwa mwaka 2017.
Serikali
imekabiliwa na idadi kubwa ya wagonjwa na wazazi wanaohudhuria kwenye hospital
na vituo vya afya kwa ajili ya kupata
huduma. Idadi ya wagonjwa wanaotibiwa na
kurudi nyumbani (wagonjwa wa nje) imeongezeka kutoka 533,703 mwaka 2010
na kufikia 705,589 hadi Novemba
2017. Hili ni ongezeko la asilimia 32.21. Wagonjwa wanaolazwa nao wameongezeka,
kutoka 51,641 mwaka 2010 hadi kufikia 68,158 hadi Novemba, 2017. Hili ni
ongezeko la asilimia 32.0. Ingawa idadi
ya wagonjwa imekuwa ikiongezeka, lakini bado Serikali inaendelea kutekeleza
Sera ya Matibabu bila ya Malipo katika
hospitali za umma hadi leo. Pamoja na kuwa upo upungufu wa vifaa, nyenzo, dawa na
kadhalika, lakini Serikali imeongeza nguvu zake katika kulishughulikia suala
hili.
Kwa mfano, tumepata
mafanikio ya kutia moyo katika ununuzi na upatikanaji wa dawa na vifaa vya
utibabu, ambapo katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali ilitenga jumla ya TZS
bilioni 4.9, kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa vya
utibabu na katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga jumla ya TZS
bilioni 7.0. Zaidi ya hayo, katika mwaka
wa fedha 2018/2019, Serikali itatenga kwenye bajeti ya Wizara ya Afya, jumla ya
TZS bilioni 12.0. Uamuzi huu wa Serikali
unatarajiwa kulipatia ufumbuzi wa uhakika wa tatizo la upatikanaji wa dawa na
vifaa vya utibabu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Pamoja na
jitihada za Serikali inazochukua katika kuimarisha huduma za upatikanaji wa
maji safi na salama, bado mahitaji ya maji ni makubwa. Jumla ya lita za maji milioni 234.45
zinahitajika kila siku kwa Unguja na Pemba, ambapo uzalishaji kwa siku ni lita
milioni 162.82 sawa na asilimia 67 ya upatikanaji wa maji safi na salama. Kwa upande wa Mkoa wa Mjini Magharibi
upatikanaji wa maji ni asilimia 63, Mkoa wa Kaskazini Unguja asilimia 48 na
Mkoa wa Kusini Unguja asilimia 50. Kwa upande wa Pemba Mkoa wa Kaskazini
asilimia 83 na Kusini asilimia 87.
Katika
kutekeleza Mradi wa Maji wa Mkoa wa Mjini Magharibi kutokana na mkopo wa US$
23.673 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), visima 9 vipya vimeshachimbwa na visima 23
vya zamani vimefanyiwa matengenezo.
Mabomba yenye urefu wa kilomita 68 yatalazwa na ujenzi wa matangi
utafanywa. Mradi huu utatekelezwa na
Kampuni ya STECOL ya China na kumalizika mwezi Aprili, 2019. Kumalizika kwa
Mradi huu kutaongeza upatikanaji wa maji safi na salama kutoka lita milioni 67 na kufikia lita
milioni 81, sawa na ongezeko la asilimia 20.9.
Kampuni ya
CRUCS kutoka India inasimamia mradi wa maji, wenye thamani ya mkopo wa US$
milioni 92 ikiwa ni mkopo kutoka Benki ya Exim ya India. Kampuni hiyo, tayari imeanza maandalizi ya mradi huo kwa kufanya
upembuzi yakinifu. Maeneo yatakayofaidika na Mradi huo ni Wilaya ya Magharibi A
na B.
Kadhalika, Mradi wa
maji unaotekelezwa na Kampuni ya “First Highway Engineering” ya China kwa ajili
ya vijiji vya Mkoa wa Kusini na Kaskazini Unguja, umekamilika Disemba, 2017.
Kuhusu visima 150
vilivyochimbwa katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba, kwa msaada wa
Serikali ya Ras Al Khaimah, visima 26 tayari vinatoa maji na yanatumika na
visima 14 viliendelea kutayarishwa, katika mwaka 2017.
Katika mwaka
2017, Serikali iliendeleza mazungumzo na
Kampuni ya RAK Gas ya Ras Al Khaimah, kwa madhumuni ya kuanza kazi ya
utafiti wa Mafuta na Gesi Asilia. Awamu
ya Kwanza ya utafiti huo ilifanywa mwezi wa Machi, 2017 kwa kutumia ndege ya
Kampuni ya “Bell Geospace Enterprises” ya Uingereza iliokabidhiwa kuifanya kazi
hio. Awamu ya pili ya utafiti huo
ilifanywa kuanzia tarehe 27 Oktoba, 2017 na Kampuni ya BGP Explorer ya
China. Utafiti huu kwenye awamu ya pili
ulihusika katika miamba iliopo kwenye maeneo ya bahari.
Katika mwaka
2018, Serikali inaendeleza utafiti wa mafuta na gesi kwa kutegemea taarifa
itakayotolewa na wataalamu baada ya utafiti uliofanywa. Serikali itatoa taarifa
rasmi kwa wananchi kuhusu matokeo ya utafiti huu unaofanywa kwa maslahi ya
Zanzibar.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Hivi sasa huduma za
umeme zinapatikana katika shehia zote za Unguja na Pemba na wananchi
wananufaika na huduma hizi muhimu. Miundombinu ya huduma hizi imekamilishwa kwa asilimia 91 na mahitaji ya
umeme kwa Unguja na Pemba, yametekelezwa kwa asilimia 60, kwa kadri wananchi
walivyojitokeza kuunga umeme. Kwa mwaka
2016/2017 jumla ya vijiji 76 vimefikishiwa umeme na mwezi wa Julai, 2017 umeme
umefikishwa katika Kisiwa cha Fundo na tarehe 6 Januari, 2018 umeme ulizinduliwa
rasmi. Mpango wa Serikali ni kuufikisha umeme katika Kisiwa
cha Uvinje hapo 2017/2018, Kokota 2018/2019 na Njau 2019/2020. Hadi sasa tumeshafikisha umeme jumla ya
visiwa saba vya hapa Zanzibar. Kadhalika, Serikali itaendelea na juhudi zake za
kuufikisha umeme kwenye vijiji na vitongoji ambavyo bado havijapata umeme.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Wananchi
wanaendelea kupata fursa nzuri ya kuitumia ardhi kwa ajili ya kuendeleza maisha
yao kwa kilimo, ujenzi wa nyumba bora na kadhalika. Kinyume na wakati wa ukoloni, ambapo hata
kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa nyumba kikitozwa kodi, seuze kupata ardhi kwa
ajili ya kilimo.
Katika mwaka
2017, Serikali iliendelea na utaratibu wa kuwapatia wananchi na wawekezaji
nyaraka za kumiliki haki ya matumizi ya ardhi kwa matumizi mbali mbali, ambapo
hati zipatazo 1,400, zitatolewa hivi
karibuni. Aidha, zoezi la uhakiki
lililoanza kutekelezwa, litaendelezwa katika maeneo mbali mbali ya ardhi
yakiwemo ya kilimo, uwekezaji na ujenzi wa makaazi, ili kuona yanatumika
ipasavyo.
Katika mwezi wa
Disemba 2017, Serikali iliandaa Sera Mpya ya Ardhi ya Zanzibar, ambayo itaimarisha
utawala na usimamizi wa sekta ya ardhi.
Kuandaliwa kwa sera mpya ya ardhi kutapelekea kufanyiwa marekebisho
sheria nane za ardhi za Zanzibar.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Kwa kutambua
umuhimu wa kilimo; Serikali inaendelea kuwapa wakulima ruzuku ya asilimia 75 ya
pembejeo na huduma za matrekta. Hatua hiyo imepelekea, mavuno ya mpunga kuongezeka kutoka tani 33,655.06 za mpunga
kwa mwaka 2013 hadi tani 39,000 mwaka 2017.
Katika
kuwahudumia wakulima kwa msimu wa mwaka 2017/2018, tani 1,800 za mbolea, tani
350 za mbegu ya mpunga na lita 15,000 za dawa za kuulia magugu zimenunuliwa na
zitasambazwa kwa wakulima. Aidha, katika kuhakikisha kuwa huduma za matrekta
zinakua za uhakika, serikali imeanzisha Wakala wa Serikali wa Huduma za
Matrekta na zana nyengine za kilimo.
Mbali na matrekta ya zamani yaliyopo kwenye kiwanda cha matrekta Mbweni,
Serikali imetiliana saini Hati ya
Maelewano (MoU) na Kampuni ya Mahindra Mahindra ya India ya kununua
matrekta 100 na matrekta 20 kutoka Kampuni ya Mahindra Mahindra tayari
yameagizwa.
Serikali
imeziimarisha shughuli za utafiti wa kilimo, katika Taasisi ya Utafiti wa
kilimo Kizimbani. Katika mwaka 2017, Taasisi ya Utatifii wa Kilimo, Kizimbani
imefanya tafiti sita (6), katika zao la muhugo, mpunga, mikarafuu, migomba na
kunde. Utafiti huo umeonesha matokeo
mazuri na bado unaendelea.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Juhudi
zimefanywa na Serikali katika kuimarisha sekta ya uvuvi. Katika mwaka wa 2017, jumla ya tani 24,000.44
za samaki zenye thamani ya TZS milioni 109.17 zimevuliwa. Katika
kushajiisha ufugaji wa samaki, Serikali imeanzisha kituo cha Kutotolea Vifaranga vya Samaki kilichopo Beit
el Raas, kwa kushirikiana na Serikali ya Japan na FAO chenye uwezo wa kuzalisha
vifaranga milioni 10 kwa mwaka. Kituo
hiki kinatarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni.
Aidha, Serikali
imeanzisha Kampuni ya Uvuvi ya Zanzibar (ZAFICO), kwa mtaji wa TZS bilioni 7 na imeamua kununua
meli mbili za uvuvi kwa kuanzia shughuli hizo, hivi karibuni.
Ili kuongeza kasi ya ufanisi na kuongeza tija
katika kuiendeleza sekta ya mifugo, hivi karibuni Serikali imeanzisha Taasisi
mpya ya Utafiti wa Mifugo. Katika mwaka
wa fedha, 2017/2018, Taasisi hiyo imepatiwa TZS. milioni 500 ambapo imeanza
kufanya tafiti 6 ikiwemo athari za minyoo katika ng’ombe na matumizi ya mwani
kama chakula cha mifugo. Kadhalika,
jumla ya vikundi 18 vya wafugaji vimepatiwa ng’ombe 368 na mbuzi 720 wa maziwa
kwa mpango wa kopa ng’ombe lipa ng’ombe.
Vile vile, vijana 60 wamepatiwa elimu ya huduma za mifugo vijijini, ili
kuwasaidia wananchi katika vijiji vyao.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Serikali
inaendelea na ujenzi wa miundombinu ya barabara mpya katika maeneo mbali mbali ya Unguja na
Pemba. Ujenzi wa barabara ya Jendele -
Cheju - Unguja Ukuu (km. 11.7), kwa
kiwango cha lami na bara bara ya Kwarara
- Matumaini zimekamilika na zimezinduliwa rasmi jusi katika sherehe za
Mapinduzi. Vile vile, ujenzi wa Barabara ya Bububu - Mahonda -
Mkokotoni (km 31) unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa kwa mkopo wa
Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).
Mjenzi wa barabara hio tayari amekabidhiwa eneo la ujenzi huo.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Ujenzi wa
barabara ya Chwale (Madenjani) hadi Mzambarau Takao (km. 5.0) na
barabara ya Mgagadu hadi Kiwani (km 7.6), kwa kiwango cha lami huko Pemba nao
umekamilika na tayarinzimezinduliwa.
Vile vile, ujenzi wa barabara ya Ole - Kengeja, (km. 35) unaendelea
vizuri, ambapo kazi ya utiaji lami kutoka Ole hadi Vitongoji (km. 7)
umeshafanyika na jitihada zinaendelea.
Kadhalika, Serikali itazijenga kwa kiwango cha lami barabara mbali mbali za vijijini za Unguja na
Pemba katika mwaka 2018.
Katika
kuimarisha usafiri wa baharini na usafirishaji wa mafuta, tarehe 02 Disemba,
2017, Serikali ilitiliana saini na Kampuni ya “Damen Shipyard” kutoka
Uholanzi kwa ajili ya kuanza kutengeneza
meli mpya ya mafuta. Meli hiyo itakapomalizika itachukuwa nafasi ya Meli ya MT
Ukombozi. Utengenezaji wa meli hiyo utachukua
miezi 18.
Katika
kuimarisha usafiri wa anga, ujenzi wa jengo jipya la abiria linalojengwa kwenye
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, uliosita kwa muda mrefu
kutokana na sababu mbali mbali; utaendelea tena hivi karibuni baada ya
kusawazishwa kwa matatizo yaliyojitokeza na ujenzi utakamilika katika miezi 18
ijayo.
Kuhusu ujenzi
wa bandari mpya ya Mpiga Duri, ujenzi wake utaanza baada suala la mkopo wa
ujenzi huo kufanyiwa kazi na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na hatimae kujadiliana na Benki ya Exim ya
China, kuhusu mkopo huo.
Aidha, huduma
za bandari ya Malindi zimeimarishwa kwa kununuliwa vifaa vipya vya kuchukulia
na kupimia makontena pamoja na vifaa vya kukagulia mizigo na abiria wanaopita
kwenye bandari ya Malindi na Mkoani.
Katika mwaka 2017, bandari ya Malindi ilihudumia jumla ya tani za mizigo
mchanganyiko 366,918 na makontena 41,967. Bandari ya Mkoani ilihudumia jumla ya
tani 56,849.53 za mizigo mchanganyiko.
Lengo la Serikali ni kuzidi kuimarisha huduma za bandari zetu, ili
kuongeza ufanisi na kuchangia ukuaji wa uchumi wetu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Katika juhudi
za kuwaendeleza vijana na wanawake za kupambana na tatizo la ajira, juhudi
kubwa zimefanywa za kuwawezesha kiuchumi kwa kuwapatia mikopo kupitia Mfuko wa
Uwezeshaji Kiuchumi. Kuanzia mwaka 2014 hadi Disemba 2017, jumla ya Mikopo 1419
yenye thamani TZS. bilioni 2.5 ilitolewa kwa vijana, wanawake na vikundi mbali
mbali vya ujasiriamali. Katika mwaka 2017 jumla ya mikopo 221 yenye thamani ya
TZS. milioni 569.31 ilitolewa kwa wakopaji 3,149 Unguja na Pemba. Nafasi za ajira 949 zilitolewa Serikalini na
ajira 1,644 zilitolewa kwenye sekta binafsi katika mwaka 2017.
Kadhalika, Serikali imeimarisha ushiriki wa watu wenye
ulemavu katika harakati mbali mbali za kiuchumi na kijamii. Serikali ilianzisha Mfuko wa Watu wenye Ulemavu mwaka
2012. Mfuko huu wenye jumla ya TZS.
milioni 166 umekusudiwa kutumika kwa kuwapatia mikopo nafuu Watu
wenye Ulemavu kuendesha shughuli zao za kujiajiri wenyewe. Aidha, Serikali ipo katika hatua za mwisho za
kukamilisha Sera ya Watu wenye Ulemavu itakayotoa utaratibu mzuri wa
kuyashughulikia masuala yao. Kwa
kushirikiana na Washirika wa Maendeleo.
Kwa upande wa
wastaafu, Serikali imeongeza pensheni kwa viwango mbali mbali. Vile vile, pensheni jamii iliyoanzishwa na
Serikali kwa wazee wote waliofikia umri wa miaka 70, bila ya kuzingatia kazi
walizokuwa wakifanya, imeendelea kutolewa kwa mafanikio. Jumla ya wazee 27,627
wamelipwa jumla ya TZS bilioni 10.175 tangu utaratibu huo ulipoanzishwa, mwezi
wa Aprili, 2016, ambapo kila mzee analipwa TZS. 20,000 kwa mwezi.
Kuhusu
udhalilishaji wa Wanawake na Watoto, jumla ya kesi 177 za udhalilishaji
zilifunguliwa kupitia Operesheni Maalum iliyoanzishwa na Serikali mwaka
2016. Hivi sasa kesi 90 zinaendelea
kusikilizwa Mahakamani Unguja na Pemba.
Mpango wa Miaka Mitano wa Kupambana na Vitendo vya Ukatili na
Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto ulizinduliwa mwezi Julai, 2017. Serikali imejenga vituo vipya vya mkono kwa
mkono katika Hospitali ya Makunduchi na
Hospitali ya Micheweni kwa kushirikiana
na “Save the Children Fund”. Wito wangu
kwa wananchi, tuendelee kushirikiana katika vita dhidi ya vitendo hivi
vinavyoiaibisha na vinavyoidhalilisha
jamii yetu ambavyo vinafanywa kinyume na maadili yetu na haki za binadamu.
Katika mwaka
2017, Serikali imeimarisha shughuli za Mahkama katika ngazi mbali mbali ikiwemo Mahkama ya Ardhi na Mahkama ya
Watoto. Hivi sasa kasi ya usikilizaji wa
kesi imeongezeka baada ya Serikali kuongeza idadi ya Majaji na Mahakimu. Juhudi hizo zitaendelezwa kwa kuyafanyia
matengenezo makubwa majengo ya Mahkama, pamoja na kuanza ujenzi wa jengo jipya la Mahakama Kuu huko Tunguu. Ujenzi wa Mahkama hio unatarajiwa kuanza hivi
karibuni.
Kwa upande
wa Baraza la Wawakilishi, Baraza hilo
limeweza kutekeleza majukumu yake vizuri, ambapo katika kipindi cha Januari
hadi Disemba mwaka 2017, lilifanya mikutano minne ambapo jumla ya miswada 14
ilitungwa kuwa sheria. Vile vile, Jumla ya maswali 529 ya msingi
yaliulizwa na kupatiwa majibu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Kwa kuzingatia
umuhimu wa utumishi bora na nidhamu, Serikali imesimamia utekelezaji wa Sheria
Nam. 2 ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2011,
ili kuimarisha uwajibikaji, uwazi na nidhamu katika taasisi zote za
Serikali. Serikali imeongeza kasi ya kupambana na vitendo vya rushwa na uhujumu
wa uchumi. Jumla ya taarifa za uchunguzi
46 zimewasilishwa katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka kati ya mwaka 2016 na
2017 ambapo katika kipindi hicho tayari mashauri tisa kuhusu rushwa na uhujumu
uchumi yamepelekwa Mahkamani. Ni matarajio yangu kwamba wananchi wataendelea
kushirikiana na Serikali katika mapambano hayo dhidi ya rushwa.
Katika mwezi wa
Aprili, 2017 Serikali ilitimiza ahadi yake, ambapo ilipandisha mishahara kwa
watumishi wa umma katika ngazi mbali mbali, ikiwa ni mara ya nne
tangu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba ilipoingia
madarakani mwezi wa Novemba, 2010, tumepandisha mshahara mwaka 2011,2012,2013
na hatimae mwaka jana tumepandisha tena mara ya nne. Mshahara wa kima cha chini
umeongezwa kwa asilimia 100,kwa watumishi wote wa Umma, sambamba na kuimarisha
maslahi yao mengine. Vile vile,
nawapongeza waajiri katika sekta binafsi, kwa kutekeleza agizo la Serikali la kupandisha mishahara ya kima cha
chini kwa wafanyakazi wao. Serikali itahakikisha maslahi ya wafanyakazi katika sekta ya umma
na sekta binafsi, yanaimarika kwa kadri hali ya uchumi inavyoruhusu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Katika sekta ya
habari, Serikali imeendeleza jitihada za kuliimarisha Shirika la Utagazaji
Zanzibar (ZBC) kwa kuweza kuhama kutoka kwenye mfumo wa Analojia kwenda mfumo
wa Digitali. Hatua hii imeongeza kiwango
cha ubora wa matangazo ya ZBC TV.
Aidha, matengenezo makubwa
yamefanywa katika studio nne pamoja na kuziwekea vifaa vipya vya kisasa
vinavyoendana na mahitaji ya kidigitali zilizozinduliwa tarehe 9 Januari,
2018. Jengo la ZBC TV la Karume nalo
limefanyiwa matengenezo makubwa. Kwa upande wa ZBC Redio, Serikali imeanunua
vifaa mbali mbali vipya, kuzifanyia matengenezo studio tatu kwa ajili ya kuimarisha matangazo yake katika kituo cha
Rahaleo na Bungi. Ni matarajio yangu
kwamba wafanyakazi wa ZBC nao watatimiza wajibu wao, ili Shirika hili lipata
mafanikio makubwa.
Shirika la
Magazeti ya Serikali, ambalo linachapisha Gazeti la Zanzibar Leo,
limetayarishiwa mazingira mazuri kwa ajili ya wafanyakazi wake pamoja na
kupatiwa vifaa vya kisasa na ofisi yenye hadhi ya kufanyia kazi za gazeti
hilo. Hivi sasa Shirika la Magazeti la
Serikali kwa kushirikiana na Wakala wa Uchapishaji Zanzibar wamefanikiwa kuanza
kuchapisha Gazeti la Zanzibar Leo hapa hapa Zanzibar. Aidha, Shirika limefanikiwa kuliweka gazeti
hili katika tovuti yake jambo ambalo limewawezesha watu wengi zaidi kupata
fursa ya kulisoma. Nauhimiza uongozi wa
Zanzibar Leo uliendeleze gazeti hili, ili lifikie nafasi yake inayostahiki.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Jitihada za kuimarisha
michezo zimeendelezwa kwa dhamira ile
ile ya waasisi wa nchi yetu. Matunda ya
jitihada hizo yameanza kujitokeza ambapo Timu yetu ya Zanzibar Heroes,
imeonesha umahiri katika mashindano ya “CECAFA Challenge Cup” ya mwaka
2017. Kadhalika, timu yetu ya “Zanzibar
Sand Heroes” ambao wametuletea ushindi na kikombe katika mashindano ya Mpira wa
Ufukweni mwaka jana. Tunazipongeza kwa
dhati timu zote mbili. Ushindi wa Zanzibar Heroes umeipa heshima Zanzibar
katika michezo. Kwa mara nyengine natoa
shukurani kwa taasisi zote za Serikali
na watu binafsi waliotoa michango mbali iliyosaidia kuziwezesha timu zetu
kupata mafanikio tuliyoyashuhudia.
Serikali itaendelea kuimarisha
michezo kwa kuendeleza vipaji mbali mbali na kujenga miundombinu ya kisasa ya michezo kwa wakati. Na uwanja wa Mao Tse Tung nao umefikia hatua
kubwa ya ujenzi hivi sasa na utakuwa wa kisasa hapo utakapokamilika.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Maendeleo yetu
yanategemea sana kuwepo kwa amani na usalama nchini. Jukumu la kulinda amani na usalama wa nchi
yetu ni letu sote kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama. Navipongeza
vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kuilinda nchi yetu na mipaka yake. Napenda niwahakikishie wananchi na wageni
wanaoitembelea nchi yetu kwamba nchi yetu iko salama na kwamba Serikali zetu
mbili zitaendelea kutekeleza wajibu wao wa kikatiba na kisheria katika kulinda
amani, utulivu na maisha ya wananchi na mali zao.
Natumia fursa
hii kutoa pongezi zangu kwa Mheshimiwa Dk. John Pombe Joseph Magufuli katika jitihada zake za kuiongoza Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na watu wake pamoja na kupambana na vitendo vya rushwa,
ufisadi, uhujumu wa uchumi, dawa za kulevya na kuzilinda raslimali za nchi
yetu. Sote ni wajibu wetu tumuunge mkono
katika vita hivi kwa kuzingatia kuwa rushwa ni adui mkubwa wa haki na ni adui
wa jitihada zetu za kuleta maendeleo nchini.
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania katika kuuendeleza na kuuimarisha Muungano wetu. Vile vile, tutahakikisha kuwa tunashirikiana
katika mambo yasiyokuwa ya Muungano kama tunavyofanya sasa kwa faida ya pande
zote mbili za Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Mimi na Dk. John Pombe Joseph Magufuli tunatambua uzito wa dhamana
mliyotupa Watanzania, katika kuhakikisha kuwa Muungano wa Tanzania, unadumu na
unaimarika kwa dhamira ile ile ya viongozi wetu wa Awamu zilizotangulia. Nakuhakikishieni wananchi nyote, kwamba
Serikali zetu mbili, zitaendelea kuchukua hatua, ili nchi yetu iendelee kupiga
hatua kubwa zaidi na ibaki kuwa nchi ya amani na utulivu.
Waheshimiwa Viongozi na Ndugu Wananchi,
Namalizia
hotuba yangu kwa kutoa shukurani zangu tena kwa viongozi wote wa Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuungana nasi katika maadhimisho haya ya
Miaka 54 ya Mapinduzi. Nawashukuru
viongozi wastaafu, waheshimiwa mabalozi na wawakilishi wa Jumuiya za Kimataifa
na Washirika wetu wa Maendeleo na wageni wetu wote waliohudhuria. Tunaahidi kuendelea kushirikiana katika
utekelezaji wa shughuli mbali mbali za maendeleo, ili kuongeza ufanisi.
Natoa shukurani
na pongezi kwa viongozi wote wa Serikali ya Mapinduzi na watumishi wote kwa
jitihada zao katika kuwatumikia wananchi kwa moyo wa uzalendo hadi kuyafikia
mafanikio tuliyoyapata. Wito wangu ni
kwamba tuongeze kasi katika kutekeleza wajibu wetu kwa misingi ya haki,
uadilifu na utumishi bora na kuwatumikia wananchi katika kukabiliana na
changamoto zinazowakabili katika maisha yao.
Natoa shukurani
maalumu kwa Halmashauri ya Sherehe na Maadhimisho, inayoongozwa na Makamo wa
Pili wa Rais Mheshimiwa Balozi Seif Ali Idi, kwa uongozi wake mahiri, ambao
umezifanikisha sherehe hizi. Kadhalika,
shukrani zangu nazitoa kwa Makamanda wa vikosi vya ulinzi na usalama vya SMT na
SMZ pamoja na wapiganaji wote walioshiriki katika gwaride na kuzifanikisha
shughuli zote za Sherehe za Maadhimisho ya Miaka 54 ya Mapinduzi; ambazo
zimefana sana. Natoa pongezi kwa wananchi walioshiriki kwenye maandamano na
wafanyakazi wa vyombo vya habari, kwa
kuzitangaza shughuli na sherehe zetu tangu katika hatua za mwanzo za uzinduzi. Kadhalika, natoa shukurani nyingi kwa
wananchi kwa kuhudhuria kwa wingi hivi
leo kwenye kilele cha sherehe hizi.
Tuendelee kuiombea nchi yetu amani, umoja na mshikamano, ili tuzidi
kupiga hatua za maendeleo. Nakutakieni
nyote kila la kheri na mrudi nyumbani salama, usalimini.
MAPINDUZI DAIMA
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU IBARIKI TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment